NAJIVUNIA KUONA WANANCHI WA MJINI KIUYU WAKIKANYAGA BARABARA YA LAMI

 


                                        NA FATMA HAMAD, PEMBA

                                                                                                                          ‘’Ama kweli mwenye kutafuta haachi kupata’’

Msemo huo umesadilifu kwa Nassra  Salim Mohamed Diwani mstaaf wa wadi ya Kiuyu Minungwini wilaya ya Wete mkoa wa Kaskazini Pemba.

MAISHA YA NASRA

Baada ya kuzaliwa  1969, Nasra alianza kuisaka haki ya elimu ya msingi mwaka 1976 katika skuli ya msingi Piki wilaya Wete.

Akiwa darasani, Nasra hakuwa mtulivu na jinsia yake ya kike, wakati mwengine aliisahau kwa kule kujichanganya na wanafunzi wa kiume kwa ujasiri wa kutafuta elimu.

Ndio maana kwenye darsa alilosoma lililokua na wanafuzni zaidi  ya 80 waalimu wake hawakurudi nyuma na kumpa uongozi wa darasa.

Akiwa nyumbani kwake Kiuyu Minungwini na kujikunjulia utaji wa Kanga za kisutu, anasema uongozi wake ulipendwa na walimu.

‘’Pamoja na ufupi wangu na jinsia yangu ya kike, walimu waliniamini kunipa uongozi kuanzia darasa la kwanza hadi darasa la sita kwa wakati huo nilipofanya mtihani,’’anaeleza.

Ingawa kwa Nasra kuongoza wanafinzi 80 hakujua kua ni sehemu ya uongozi wala haikua matayarisho yake ya kushika hatamu ya uongozi, kama ilivyopita miaka 10 nyuma.

Miaka Arubaini iliyopita wakati akimaliza darasa la Kumi na moja kama elimu ya lazima kwa wakati huo, Nasra aliendelea kua kiongozi.

Anakumbuka vyema kuanzia darasa la Tisa, huku akili ya kitoto ikiwa ameshaiaga hamu ya kuongoza sasa imetawala kwenye akili yake.

‘’Hata nikirudi skuli ndugu na kaka zangu sikuacha kuwaongoza kwa baadhi ya mambo,’’ anaeleza Nasra.

Nasra aliyezaliwa miaka 57 iliyopita kijijini kwao Tondooni shehia ya Kisiwani kwa Binti Abedi iliyomo wilaya ya Wete, alikolea zaidi uongozi baada ya kumaliza masomo.

Akiwa nyumbani kwao suala la kutegemea wazazi kila kitu kwake lilikua mwiko, kuanzia mwaka 1990 alijiunga Chuo cha Ufundi JKU, ili awe mtaalamu wa kuzishona nguo.

‘’Lengo la kujiunga na Chuo cha ufundi kwanza ni kupata ukakamavu, ufundi wa kuzishona nguo kwa lengo la kuanza kujitegemea kama mtoto wa kike,’’ anasimulia.

Diwani huyo mstaafu baada ya kumaliza harakati za ufundi JKU, alirudi mtaani na kuanza kukushanya shilingi moja moja zilizotokana na kusukuma ringi ya Charahani kwa kuviunga vipande vya vitambaa na kuwa nguo yenye kuvalika.

Nasra alishazaliwa, mwaka 1969 la pili la mwanadamu la kufunga ndoa, ambapo  mwaka 1993  nae alipata wa kumtunza huku akiwa fundi mtaalamu wa ushonaji wa nguo mbalimbali.

‘’Wakati nafunga ndoa Nasra nimeshanza kujitegemea na kuwa na uhakika wa kupata visenti kwa ajili yangu, mume wangu, wazazi na ndugu wa karibu,’’anasema.

NASRA NA UJASIRIAMALI BAADA YA NDOA.

Akili, Fikra, mawazo na ndoto za Diwani huyu mstaafu kujua kwake kushona kumbe haikua mwisho wa kusaka visenti.

Ndio maana miaka 16 akiwa katika ndoa alijiunga na ujasiriamali wa utengenezaji wa mikoba ya ukili, katika kikundi cha Vuta heri.

‘’Kwasasa kikundi hicho kimebatizwa jina na kuitwa ‘’Nguvu yetu ni umoja’’kilichopo Kiuyu Minungwini wilaya ya Wete tukijishughulisha na utengenezaji wa sabuni za mwani, mafuta ya Mkaratusi na mapambo ya harusi,’’anasema.

Baada ya kuingia kwenye ushirika huo ujasiri, hekma na mbinu za kuwashirikisha wenzake uliwavutia na kumpa nafasi ya uratibu.

Kuanzai mwaka 2008 na miaka minne mbele Chama cha wandishi wa Habari wanawake Tanzania TAMWA Zanzibar ilitua kisiwani Pemba na mradi wa kuwawezesha wanawake kiuchumi, na Nasra akawa Mkufunzi.

Ndani ya uendeshaji wa Mradi huo Nasra alijifunza mambo kadhaa hasa ya uongozi, na namna ya utatuzi wa mogogoro, jambo lililompa nia ya kutaka nafasi zaidi za uongozi.

NASRA NA UONGOZI NJE YA ASASI

Hamu ya kutaka kuongoza wanakiuyu Minungwini ilianza kugagaa ndani ya akili yake mwishoni mwa mwaka 2014 alipoitangazia nafsi yake kuutaka Udiwani wa wadi ya Kiuyu.

Ndio maana mwaka 2015 haikua tu kwa wagombea Uraisi, Ubunge, na Uwakilishi bali hata Nasra Mohamed Salim nae alichukua fomu kutafuta ridhaa ya wananchi.

Harakati za kuchukua na kurejesha na kisha kampeni zilianza kwa mwanamke huyu shupavu, akishindana na wagombea wa zaidi ya vyama tisa woote wakiitaka wadi ya Kiuyu Minungwini.

Mwishoni mwa Octoba mwaka 2015 haikua siku tu ya furaha kwa walioshinda viti vya Uraisi pekee, hata Nasra Mohamed Salim alitokwa na machozi ya furaha baada ya waliommiminia kura kutaangazwa kuwa Diwani.

Kiongozi huyo wa Wadi ya Kiuyu minungwini kwa wakati huo, nahasa baada ya kukabidhiwa cheti cha ushindi makundi ya wanaCCM  wenzake yalivunjika na kua kitu kimoja na sasa ikawa nguvu zote ni kuvitanata vijiji vya wadi ya Kiuyu kimaendeleo.

‘’Nilipokua nagombea nafasi hii nakumbuka nilitoa ahadi mbalimbali, ikiwemo ujenzi wa Barabara kutoka Penjewani hadi Mjini Kiuyu, ili kuwapunguzia dhiki wapiga kura,’’anaeleza.

Anakumbuka vyema wakati akiwa Diwani siku aliyosimamishwa mbele ya Wananchi akiwepo Rais wa Zanzibar ndani ya Jimbola Kojani, alipotakiwa kuainisha changamoto zinzowakabili na kufanya hivyo bila ya kutetemeka.

‘’Kwakweli siku aliyokuja Rais wa Zanzibar na kusimamishwa ghafla nilikua mzito  kuanzia miguu hadi mikono, ingawa baada ya kufika kwenye kisemeo,(maiki) nilitiririka mithili ya maji yaliyokua mlimani,’’anaeleza.

Hawa kukosea wahenga waliosema kuwa mramba asali harambi mara moja, msemo huu umesadif kwa Diwani Nasra kwa kule wananchi kumrejesha tena nafasi hiyo mwaka 2020.

Mwenyewe anasema kuwa kuanzia mwezi wa tano 2020 wapo wanachama hatanje ya chama cha Mapinduzi waliomtaka kuchukua tena fomu ya Udiwani.

‘’Inawezekana ujasiri wangu utekelezaji wa ahadi na ushirikiano kwa wananchi wote ndio yaliyowasukuma hao wanachama kuniomba kuingia tena,’’anaeleza.

Kumbe kwa miongo zaid ya mitano Wadi ya Kiuyu haikua na barabara hata ya kifusi au shule ya kisasa, ingawa kelele za Diwani huyo ziliishawishi serikali kuu kutekeleza miradi mikubwa ikiwemo uimarishaji wa huduma za Afya.

Ndani ya miaka kumi enzi za Diwani huyo vipo vikundi 25 vilivyotengenezewa mazingira ya kujisajili na kutambulika rasmi, jambo lililoshindikana kwa miongo iliyopita.

USHUHUDA WA WANANCHI

Mbarouk Salim kaazi wa Mjini Kiyu anasema kabla ya ujenzi wa barabara hiyo, magari  yalikuwa hayawezi kufika katika maeneo yao hasa kipindi cha mvua.

 ‘’Tulikua tukipata mgonjwa hasa wakati wa usiku hatukijua tumfanye nini, kutokana nan a kukosa usafiri’, anasema.

 Fatma Khalfan mkaazi wa Kiuyu Penjewani, anasema wagonjwa na  wazazi walikuwa wakipata mateso wakati wa kusafirishwa kwenda hospitali.

 ‘’Siku moja mtoto wa jirani yangu alijifungulia njiani wakati alipo akipelekwa Hospitali, kutokana na ubovu wa barabara,’’anasema.

 Hamad Said Hamad miaka (70) ‘’Belfu’’  kutoka Tuliani anasema zamani wagonjwa wakiwabeba kwa vitanda hadi kufika barabara kuu, hali iliyotoa mwanya baadhi ya wagojwa pamoja na wajawazito kutibiwa majumbani.

 ‘’Wagonjwa tulikua tunawabeba kwa kitanda, tukaona hilo ni tatizo, tuliandika barua tukapeleka kwa Nasra, hakudharau siku ya pili alikuja na timu nzima ya serikali shehia na ya jimbo, tukajengewa njia hii,’’anasimulia.

 VIONGOZI WA SERIKALI

 Katibu Tawala wilaya Wete,  Mkufu Faki Ali, anasema maendeleo ya barabara hizo yamechangia kuboresha huduma za kijamii na shughuli za

kiuchumi.

 ‘’Barabara hizi zinasaidia wananchi wa vijiji hivyo,

wameondokana na shida ya usafiri ,’’ anasema.

 Naibu sheha Shehia ya Kiuyu Minungwini Haji Kombo Hamad anasema jumla ya wananchi 2682 wa Mjini kiuyu walikua na changamoto ya barabara  hio zaidi ya mika 30.

 ‘’Maendeleo na uchumi wa wananchi umekua,  wanasafirisha biashara zao na wanafikia huduma wanazozihitaji kwa wakati, mfano Hospitalini,’anaeleza.

 Diwani wa sasa wa Wadi hiyo ya Kiuyu Minungwini Hassan Khamis Hamad anasema kuwa ushiriki wa wanawake katika nafasi za maamuzi, unaendelea kuonyesha uwezo  sawa kati ya wanawake na wanaume, katika kusimamia maendeleo.

 Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum wa serikali ya Jamuhuri ya Mungano Mwanaidi Ali Khamis, anasema Tanzania inaendelea kutambua umuhimu wa Wanawake kwa kuwapatia fursa katika nafasi za Uongozi na Maamuzi.

Anasema mabadiliko hayo yanatokana na dhamira ya Rais wa Jamuhuri ya Mungano Dkt Samia Suluhu Hassan,  ya kuhakikisha usawa kati ya Wanaume na Wanawake, katika nyanja zote. 

"Serikali inaendelea kusimamia utekelezaji wa mikataba ya Kikanda na Kimataifa inayolenga kukuza  Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji Wanawake hapa nchini,’’anamalizia.

WANAHARAKATI 

 Mkufunzi kutoka Chuo cha Taifa Zanzibar (SUZA) Aimane Othman Duwe anasema wanawake wanapopewa nafasi za uongozi huleta mabadiliko, hutatua changamoto za jamii, hususan zinazohusu huduma za msingi kama afya.

 ‘’ Mwanamke ni mama, ni mtu ambae maranyingi hua karibu na jamii,anajua shida zinazowakabili, hivyo anapopata nafasi ni rahisi kuleta mabadiliko,’’anasema

 Afisa Programu wa masuala ya wanawake na uongozi kutoka Chama cha Wandishi wa Habari Wanawake TAMWA Zanzibar Khairat Ali anasema mchango wao wanaoufanya ni kutoa elimu na kuhamasisha wanawake wapewe nafasi za maamuzi.

 ‘’Mwanamke ni mama, na maranyingi mama hupenda afanye mazuri ili mtoto wake abaki salama,’’anasema.

 USHUHUDA WA VIONGOZI WANAWAKE WALIOFANIKIWA

 Mitandao ya kijamii kama X (zamani Twitter), Facebook, na YouTube imekua ikiripoti kwamba  mara nyingi Wanawake wana uwezo wa kuongoza kwa ufanisi sawa na wanaume.

 Rais wa Jamuhuri ya Mungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan Baada ya kuapishwa kuwa Rais mwaka 2021 alisimamia ujenzi wa miundombinu mikubwa, diplomasia ya kimataifa, na kuleta maridhiano ya kisiasa nchini.

 utafiti uliochapishwa mwaka 2023 kwenye jarida la Information, Communication and Society,  umeonyesha kuwa mawasiliano yake kupitia mitandao ya kijamii yalijenga taswira nzuri ya uongozi wa mwanamke.

 Bi Ellen Johnson Sirleaf  Rais wa zamani wa Liberia na mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, aliyefanikiwa kuleta amani na kujenga upya nchi yake iliyotoka kwenye vita vya wenyewe kwa wenyewe.

 Jacinda Ardern  Waziri Mkuu wa zamani wa New Zealand, aliyetambulika kwa uongozi wake thabiti na wenye huruma wakati wa majanga ya kitaifa kama shambulio la msikitini na janga la Uviko-19.

 TAKWIMU

Zanzibar wapo Madiwani wanawake  27 kati ya Madiwani wote 110 ambapo kwa mkoa wa Kaskazini Pemba Pekee wapo madiwani 34.

MIKATABA

Katiba ya Zanzibar ya 1984, Kifungu cha 21 kifunu  kidogo cha 3 kinaeleza kwamba, kila mzanzibari anayohaki ya kushika nafasi yoyote ya kazi na shughuli yoyote iliyoko chini ya mamlaka ya Zanzibar.

Mkataba wa  Umoja wa Mataifa wa kutokomeza  ubaguzi dhidi ya Wanawake (CEDAW) wa mwaka 1979, hususan Kifungu cha 7, kinachotaka wanawake washiriki kikamilifu katika maisha ya kisiasa na ya umma.

 Azimio la Beijing (Beijing Declaration and Platform for Action) la mwaka 1995, linalosisitiza kuongeza ushiriki wa wanawake katika nafasi za maamuzi.

 Itifaki ya Maputo ya mwaka 2003,  Kifungu cha 9, kinachohimiza ushiriki sawa wa wanawake katika mchakato wa kisiasa na maamuzi.

 MWISHO

 

 

 


Comments

Popular posts from this blog

WANDISHI WA HABARI ANDIKENI HABARI ZA UCHAMBUZI

HOFU YA UDHALILISHAJI MTANDAONI INAVYOWANYAMAZISHA WANAWAKE

UROHO WA MALI KWA WANAUME UNAVYONYIMA WANAWAKE ARDHI