HOFU YA UDHALILISHAJI MTANDAONI INAVYOWANYAMAZISHA WANAWAKE
NA FATMA HAMAD, PEMBA Katika ulimwengu wa kidijitali, mitandao ya kijamii imekuwa sauti ya wengi, ni mahali ambapo watu hujadili siasa, biashara, elimu na masuala ya kijamii. Ingawa kwa wanawake wengi, majukwaa haya yamekuwa pia uwanja wa matusi, vitisho na udhalilishaji unaowafanya waogope kujieleza hadharani. Mara nyingi mwanamke anapotoa maoni kuhusu suala la kijamii au kisiasa, hukumbana na mashambulizi yanayolenga jinsia yake badala ya hoja aliyoitoa. Matokeo yake, baadhi yao huamua kunyamaza, kufunga akaunti au kujiondoa kabisa kwenye mijadala ya umma. Kwa sasa Tatizo hilo linaonekana kuwa changamoto kubwa ya haki za kidijitali na usawa wa kijinsia duniani. Utafiti wa kimataifa uliofanywa na UNESCO kwa kushirikiana na International Center for Journalists (ICFJ) mwaka 2021, uliowahusisha wanawake wanahabari 901 kutoka nchi 125, ulibaini kuwa asilimia 73 walikuwa wamewahi kukumbana na vurugu au udhalilishaji mtandaoni kutokana na kazi zao. Utafiti ...