ZAMECO YAITAKA SERIKALI KUHARAKISHA MSWADA WA SHERIA YA HUDUMA ZA HABARI ZANZIBAR
NA FATMA HAMAD, PEMBA Kamati ya Wataalamu wa Masuala ya Habari Zanzibar (ZAMECO) imeiomba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuharakisha mchakato wa kuuwasilisha Barazani Mswada wa Sheria ya Huduma za Habari Zanzibar ili uweze kujadiliwa na hatimaye kuwa sheria, baada ya kusubiriwa kwa zaidi ya miaka kumi. Kwa mujibu wa ZAMECO, sekta ya habari Zanzibar bado inasimamiwa na sheria mbalimbali zilizotungwa katika nyakati tofauti, hali inayosababisha kuwepo kwa mfumo wa kisheria usioendana kikamilifu na mahitaji ya sasa ya sekta hiyo pamoja na maendeleo ya teknolojia ya habari na mawasiliano. Kamati hiyo imeeleza kuwa baadhi ya sheria zilizopo zimezipa mamlaka makubwa taasisi za Serikali katika kusajili na hata kufungia vyombo vya habari, jambo ambalo linaonekana kutokidhi kikamilifu misingi ya demokrasia, uwazi na utawala bora wa sheria. Ahadi za Muda Mrefu ZAMECO imekumbusha kuwa taarifa za kukamilika kwa Mswada huo zimekuwa zikitolewa na viongozi mbalimbali wa Serikali kwa nyakati t...