WANDISHI WA HABARI ANDIKENI HABARI ZA UCHAMBUZI

 


NA FATMA HAMAD, PEMBA

 MTAALAMU wa masuala ya Utafit kutoka Taasisi ya Utafiti wa Kiuchumi na Kijamii Tanzania (Economic and Social Research Foundation) Richard Ngilangwa  amewataka waandishi wa habari kuandika habari za uchunguzi na zenye ukweli ambazo zinazingatia takwimu na tafiti, ili zilete tija kwa umma.

 Mtaalamu huyo aliyasema hayo wakati akizungumza na waandishi wa habari katika mafunzo ya habari za Utafiti yaliyofanyika katika Ukumbi wa Ofisi ya ZRA Gombani Chakechake Mkoa wa Kusini Pemba.

 Alisema, Tafiti zinafaida kubwa kwa jamii, hivyo ni vyema kwa waandishi wa habari kujikita katika eneo hilo la uwandishi wa habari za utafiti na kuzichambua kwa ajili ya kufichua shida za wananchi ili zipatiwe kwa ufumbuzi.

 ‘’Tafiti zinazofanywa ni haki ya kila mmoja na sio kubakia Makabatini, hivyo zichukueni mzichambue na mziandikie zipate kujulikana, ili kama kuna jambo linahitaji kufanyika basi lifanyiwe kazi kwa urahisi na kwa wakati muafaka,’’alisema.

 Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Tafiti na Uratibu kutoka Tume ya Mipango Zanzibar Omar Juma Ali alisema, tafiti zinazofanywa zinamchango mkubwa wa kuwasaidia  wandishi wa habari kupata vyanzo sahihi vya  kuibua habari ambazo zitaleta maslahi bora kwa umma.

 Alisema, endapo waandishi wa habari watazitumia tafiti hizo kwa usahihi, zitasaidia kupatikana kwa taarifa na kufahamu matukio yaliyoibuliwa, kuifahamisha jamii na kusaidia kuchukua hatua juu ya jambo lililofanyiwa utafiti.

 ‘Ndugu zangu waandishi wa habari katika tafiti muna uwezo wa kupata vyanzo vya kuandika habari, hivyo mkizitumia kwa usahihi mtauwelewesha umma juu ya jambo lililoibualiwa baada ya utafiti,’’alisema.

 Alisema, imeonekana waandishi wa habari hawana uwelewa juu ya kuandika habari za tafiti, hivyo Tume ya Mipango Zanzibar kwa sasa imeweka mpango mkakati wa kuwaelimisha waandishi wa habari juu ya matumizi sahihi ya Takwimu kuzifahamu na kuzifanyia kazi, kwani kutasaidia kuibua kero zilizojificha, ambazo ni kikwazo kwa wananchi.

 Nao waandishi wa habari waliohudhuria mafunzo hayo walisema, mafunzo yamewafumbua macho huku wakiahidi kuyafanyia kazi kwa kuwandika vyema habari zinahusiana na takwimu na kuleta mafanikio kwa jamii yao.

  MWISHO.

 

   


Comments

Popular posts from this blog

HOFU YA UDHALILISHAJI MTANDAONI INAVYOWANYAMAZISHA WANAWAKE

UROHO WA MALI KWA WANAUME UNAVYONYIMA WANAWAKE ARDHI