WANDISHI WA HABARI IELIMISHENI JAMII MATUMIZI YA MITANDAO
NA
FATMA HAMAD,PEMBA
MTAALAMU
WA Masuwala ya Mitandao ua Kijamii kisiwani Pemba Mustafa Mohd Abdul Rabi Moyo
amewataka Wandishi wa Habari kuendelea kuielimisha jaamii hususani
ya wanawake, kufuata miko na
maadili ya mitandao, ili kuepuka kufanyiwa udhalilishaji mitandaoni.
Mtaalamu huyo ameyasema hayo wakati akizungumza na mwandishi
wa habari hizi huko Ofisini kwake Chakechake Pemba, alisema imeonekana jamii
haina elimu ya kutosha juu ya matumizi sahihi ya mitandao, hivyo ipo haja
wandishi wa habari kutoa elimu, ili kuepuka udhalilishaji huo.
Alisema kutokana na kuzuka kwa wimbi la udhalilishaji katika
mitandao ya kijamii kwa wanawake, ni budi jamii kuelimika na kufahamu madhara
ya udhalilishaji mtandaoni.
Alisema kwa sasa udhalilishaji ambao
unatumika zaidi katika mitandao ni wa
mashambulizi ya matusi, na huu unakuja pale mwanamke anapotuma picha za maungo yake yakiwa utupu.
‘’Niwambie tu dada zangu, licha kua mnatangaza biashara zenu ila
ni vyema mkavaa nguo za stara, zenye
heshima, msiweke picha ambazo zitawapa wahalifu fursa ya
kuwadhalilisha,’’alisema.
Akitaja moja ya athari ambayo anaweza kuipata mwanamke wakati asipotumia vizuri mitandao ya kijamii ni kujiondolea heshima na kupelekea kukosa fursa za maendeleo katika jamii.
‘’Inawezekana siku moja mwanamke akajakugombea nafasi ya uongozi hivyo kama atakua hatumii mitandao vizuri inaweza kuja kuwa sababu akakosa nafasi, kwani watu wanaweza kuangalia historia yako na ikaonekana huna historia nzuri,’’alieleza.
Alisema Teknolojia mpya ya Akili bandia (AI) inaweza ikatoa mwanya kwa wahalifu kupata fursa ya kuwadhalilisha wengine, hivyo wanawake wahakikishe wanatumia mitandao ya kijamii kwa uwangalifu na uwadilifu wa hali juu.
Alisema asilimia 70 ya wananchi wa Pemba wanatumia mitandao ya kijamii kwa shughuli zao mbalimbali, hivyo ipo haja kuendelea kuitumia mitandao kwa uwangalifu, ili kuendelea kunufaika na fursa zilizomo mitandaoni.
Kwa upande wake Mrakibu wa Polisi Out Gromic Abock ambae ni mkuu wa Polisi jamii Kaskazini ali sema ipo haja Jamii kuzingatia matumizi sahihi ya mtandao, kwa kuepuka kuangalia maudhui yaliokinyume na kanuni na Sheria za Nchi.
Aidha alisema ni jamii kujifunza Sheria ya makosa ya mtandaoni ya mwaka 2015, ili kuepuka kufanya vitendo vinavyokwenda kinyume na Sheria hiyo.
Mwanaharakati kutoka Jumuia ya Wasaidiz wa Sheria wilaya ya Micheweni Saleh Hamad Juma, alisema Ili kudhibiti vitendo hivyo, ni vyema kukaimarishwa kwa sheria za kukabiliana na unyanyasaji mtandaoni, kuongeza elimu ya matumizi salama ya mitandao ya kijamii na kuwawajibisha wanaowadhalilisha wengine.
Sheria ya Maudhui ya Mtandaoni ya 2020: Inakataza kurusha picha, video za utupu, au kutumia lugha za matusi na kejeli zinazodhalilisha utu.
MWISHO.
Comments
Post a Comment