Wanawake wanaolima kilimo msitu Mchanga mdogo walia kukosa ardhi

 


                 NA FATMA HAMAD, PEMBA

WANAWAKE ambao ni wakulima wa kilimo msitu, shehia ya Mchanga mdogo wilaya ya Wete Pemba, wamesema wanakabiliwa na changamoto ya umiliki wa ardhi, jambo linalowalazimu kuzitumia za wenzao wao.

Walisema hawana mashamba yao,  na badalayake hulima katika ardhi za waume zao, jambo linalowapa hofu juu  ya kuendeleza kilimo chao hicho ama kinyume chake.

Wakizungumza na mwandishi wa habazri hizi kwa nyakati tofauti juu ya maendeleo ya kilimo chao, walisema hilo haliwapi uhakika wa kilimo hicho, kutokana na hofu ya kibinaadamu.

 Walisema licha ya matamko mbalimbali za kisheria na  kidini, kuelezea haki zao juu ya umiliki wa ardhi, lakini bado jamii hawajalipa kipaumbele na kuendelea kutumia ardhi za watu wingine.

Mmoja kati ya wakulima hao,  Fatma Hamad Bakar, alisema kwa mwaka wa pili sasa, anaendeshe kilimo hicho, katika shamba la aliyekuwa muume wake, ambae hadi sasa hawajarithi.

Nae Zaituni Khamis, alisema kwa hakika ndoto za maisha yao kwenye kilimo msitu, huwa hazifikiwi kutokana na kutokuwa na ardhi ya uhakika.

Alifafanua kuwa, umaskini wa kipato ni moja ya jambo linalochochea kukosa aradhi, na kuwaacha kwenye njia ya panda ya ndoto zao za kufanikiwa kimaisha.

‘’Lakini jingine ambalo linatukosesha ardhi, ni baadhi ya wanaume kuendelea kuzikalia mali za urithi, na kuwa wazito kutekeleza sheria hiyo,’’alifafanua.

kwa upande wake Asha Khamis mkaazi wa Gombeume Mchanga mdogo, alisema yeye alifanikiwa kununua ardhi miaka mitatu iliyopita, baada ya kujichanga kidogo kidogo.

Alisema, ijapokuwa lipo shamba la familia na anaweza kuendesha kilimo msitu, lakini aliona njia ya kufikia ndoto zake ni kujipanga na kununua ardhi yake.

‘’Kwa sasa naendesha kilimo cha msitu chenye miti mchanganyiko kama mparachichi, michungwa, migomba pamoja na minanasi, nikiwa kwenye shamba langu bila ya hofu,’’alisema.

Mpema mtetezi wa masuala ya wanawake kutoka Jumuia ya Uhifadhi wa misitu kisiwani Pemba ‘CFP’ Sada Juma Segenya , alisema  bado umiliki wa ardhi kwa wanawake ni tatizo ndani ya jamii.

Alieleza moja ya changamoto inayowakabili katika mradi wao wa uhifadhi mazingira, ni baadhi ya wanawake kutomiliki ardhi, kwa ajili ya kuendeshea shughuli hizo za uhifadhi na kuongeza kipato.

‘’Mradi wetu wa uhifadhi wa mazingira, ambao tunautekeleza katika shehia za Chwale, Mchanga mdogo, Kambini na Mjini kiuyu, changamoto kubwa ni baadhi ya wanawake kukosa ardhi, na badalayake hutumia za waume zao,’’alisema.

Mkuu wa kitengo cha  mawasiliano kutoka Chama cha Wandishi wa Habari Wanawake Tanzania -TAMWA Zanzibar, Sofia Ngalapi, alisema kufuatia changamoto ya mabadiliko ya tabianchi, wameamua kuleta mradi wa kuwawezesha wanawake, kutunza mazingira na kuingiza kipato.

Alieleza kua mradi huo ni ushirikiano wao na Jumuia ya Uhifadhi wa Misitu Pemba ‘CFP’ na Jumuia ya uhifadhi wa Misitu ‘CFI’ kutoka Canada, ukiwa na lengo la kuwainua kiuchumi na kuepukana na athari za mabadiliko ya tabianchi. 

‘’Bado wanawake wanaachwa nyuma juu ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, kwani hawana maeneo ya kuhifadhia, na kuepukana na athari hizo,’’alifafanua.

 Naibu Mrajisi kutoka Kamisheni ya ardhi Pemba Asha  Suleiman Said alisema kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi namba 12 ya mwaka 1992, inaeleza kuwa ardhi ya Zanzibar ni mali ya umma, hivyo kila mwananchi anahaki ya kutumia ardhi.

Alisema katika Kifungu cha 7 cha sheria hiyo, kinaeleza wazi, kwamba haki ya kutumia ardhi ya Zanziba ni kwa wazanzibari wote.

Akitaja moja ya njia ambayo mtu anaweza kupata ardhi ni kurithi, kununua, kupewa kama zawadi na kuiomba serikalini.

Amirati kutoka Jumuia ya wanawae wa kiislamu Pemba (JUMA WA KIPE), Asya Amour Abrahman alisema, uislamu umemnyanyua mwanamke, na anayo haki ya kumiliki ardhi.

‘’Mwanamke ana haki ya kumiliki ardhi na akaweza kuitumia kwa shughuli za kilimo, maana sio kosa kuwa na uwezo na kipato,’’alifafanua.

Kiongozi wa Kanisa Katoliki lililopo Mkungu Malofa Chake chake, Robert Miguwa Ndalami, alisema mwanamke anahaki ya kumiliki ardhi, kama mwanamme.






 

Comments

Popular posts from this blog

KERO YA MAJI, TATIZO KWA WANAKIJIJI CHA GOMBEUME

HIVI NDIVYO UTELEKEZWAJI WA WATOTO UNAVYOATHIRI MALEZI, MAKUZI YAO

DNA YA THIBITISHA, MTUHUMIWA NDIE BABA MZAZA WA MTOTO