TIMU ZA WANAWAKE ZA PEMBA ZAOMBA KUSHIRIKISHWA KWENYE MASHINDANO YA KITAIFA
NA FATMA HAMAD-PEMBA
Kukosekana kwa uwanzishwaji wa ligi maalumu kwa wachezaji wanawake, imekua ni kikwazo kikubwa kinachokwamisha Timu ya Mpira wa pete iliyopo Mchangamdogo Wilaya ya Wete Mkoa wa Kaskazini Pemba.
Hayo yamesemwa na Amina Kudra Ali Mchezaji wa timu ya mpira wa Pete ya Wete wakati wakizungumza na wandishi wa habari ikiwa ni ufuatiliaji wa tathmini ya mafanikio wa mradi wa michezo kwa maendeleo uliokua ukitekelezwa na Chama cha wandishi wa habari wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA), Chama cha wanasheria wanawake (ZAFELA) na CYD.
Anasema anahamu ya kua mchezaji mkubwa duniani, lakini anarudinyuma kwasababu tangu walipoanzisha timu hiyo hawajashirikishwapo mashindano ya ligi za aina yoyote na kuweza kukuza vipaji vyao.
‘’Huu ni mwaka wa tano tokea kuanzisha timu yetu hii ya mpira wa pete pamoja na Netball, lakini tunakata tama hatujashirikiswapo hata siku moja bonanza lolote ambalo limeandaliwa na Serikali,’’anasema.
Anasema michezo ni moja ya fursa inayomfanya mtu kujipatia ajira, hivyo ni vyema kwa Serikali pamoja na wadau wengine kuziunga mkono timu za wanawake zilizopo Pemba ili ziweze kufika mbali kimichezo.
Kwa upande wake mchezaji Zainab Rashid Said amesema tokea alipojiunga na timu hiyo alibahatika kupata safari mara moja ya kuenda kisiwani unguja kwa ajili ya kushiriki mashindano ya ligi kuu.
‘’Tumekua tukishuhudia wanawake wakisafiri na kuenda nchi za nje kwa ajili ya michezo, hivyo Tunatamani ufike wakati viongozi wawekeze kwenye timu zetu, ili na sisi vijana wa kike wa Pemba tuweze kutambulika duniani kupitia michezo,’alieleza.
Katibu wa timu hiyo Bimkubwa Maulid Othman amesema baada ya kupatiwa mafunzo juu ya umuhimu wa mwanamke kushiriki kwenye michezo, kutoka kwa Chama cha wandishi wa Habari Wanawake Tanzania TAMWA Zanzibar waliamua kuanzisha timu ya mpira wa pete, ili kuona wanawake wa pemba nawao wananufaika na fursa zitokanao na sekta ya michezo.
‘’Tumeamua kuanzisha mchezo huu kwa ajili ya kujenga afya zetu pamoja na kuonesha vipaji vyetu sisi kama wanawake,’’ameeleza.
Akitaja changamoto zinazowakabili katika timu yao ni kukosekana kwa uwezeshwaji pamoja na vitendea kazi.
Anasema wamekua wakichangishana wenyewe kwa wenyewe pamoja na viongozi wao wa majimbo na kuanzisha mabonanza ya shehia ili waweze kutoa hamasa kwa jamii juu ya umuhimu wa michezo kwa mwanamke na mtoto wa kike.
‘’Tumekua tukiwaomba viongozi wetu wa majimbo waweze kutuandalia japo ligi ndogondogo, ili tuweze kuonesha vipaji vyetu,’’ameeleza.
Amesema jamii imekua akiwachukulia kama ni wahuni kwa vile wamejiingiza kwenye michezo, hivyo ameiomba Serikali ya Mapinduzi kuangalia kwa jicho la pili ili kuona wanaungwa mkono na kuweza kujiajiri kupitia sekta hiyo.
‘’kama hakutokua na uwezeshwaji wowote tutakuja kukosa timu hata moja za wanawake na kuweza kushiririki mashindano mbalimbali endapo yatatokezea,’’amesema.
‘’Wanawake nawao wanahaki ya kushiriki michezo kama wanavyoshiriki watoto wa kiume, hivyo niwakati jamii kuamka na kuwaruhusu ili nawao waweze kupata ajira kupitia michezo,’’ameeleza.
Amesema kama TAMWA wataendelea kuwapa moyo wachezaji hao, waweze kuwa wachezaji wazuri, huku akiomba na wadau wengine wajitokeze kuwasaidia ili waweze kutimiza ndoto zao.




Comments
Post a Comment