WANAWAKE WENYEULEMAVU WASHIKA MKIA KWENYE KAMATI ZA SHEHIA

 


       NA FATMA HAMAD, PEMBA

WATU WENYE ulemavu, wana haki ya kushirikishwa katika nyanja zote za kiuchumi, kama raia wote, bila ya kujali ulemavu wao, maana kinachoangaliwa sio ulemavu bali ni haki zao na uwezo wao.

Na ndio maana, serikali, ikaweka muongozo maalumu, ili maendeleo ya nchi yasiwaache nyuma kwa kuimarisha muundo wa tasisi za watu wenye ulemavu.

 Tanzania imeridhia Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (CRPD), wa mwaka 2006 unahimiza serikali, kuhakikisha ushiriki sawa wa watu wenye ulemavu katika siasa na maamuzi.

Katiba ya Zanzibar ya 1984, Kifungu kidogo cha 3 kinaeleza kwamba, kila mzanzibari anayohaki ya kushika nafasi yoyote ya kazi na shughuli yoyote iliyoko chini ya mamlaka ya Zanzibar.

Sheria ya watu wenye ulemavu namba 8 ya mwaka 2022, kifungu cha 29 kinaeleza, umuhimu wa watu wenye ulemavu kufikia miundombinu pamoja na taarifa, mawasiliano na haki zote za kibinadamu.

Tathmini ya Utekelezaji wa Sera ya Maendeleo ya wanawake na Jinsia Zanzibar mwaka 2000, imebainisha upungufu na changamoto zilizoathiri utekelezaji wa Sera hiyo ikiwa ni pamoja na kutofikiwa kwa usawa wa kijinsia.

 Hali hii imethibitishwa na vipimo vya usawa wa kijinsia (Gender Inequality Index – GII na Social Institutions and Gender Index – SIGI, 2022) ambapo Tanzania, imepata alama 0.539 kwa ‘GII’ na 0.262 kwenye ‘SIGI’, ikiwa ni viwango vya chini vya kufikia usawa wa kijinsia.

Nchini China, takwimu zinaonyesha kwamba kipato cha wanawake wenye ulemavu ni sawa na asilimia 42.5 ya kipato cha wastani kwa mtu bila ulemavu.

 Bajeti ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na watoto Zanzibar ya mwaka 2024/2025 imebainisha kuwa, tafiti zinaonesha kuwa nchi zinazozingatia usawa wa kijinsia, zimeweza kuimarika kiuchumi kwa kasi kuliko nchi ambazo hazizingatii usawa huo.

Licha ya kuepo kwa miongozo hiyo bado ushiriki wa wanawake wenye ulemavi ni mdogo, katika ngazi za maamuzi, kuanzia ngazi ya familia,  shehia na hata Taifa.

Makala hii inatuonesha kwamba ni kwa kiasi gani wanawake wenye ulemavu wameshirikishwa katika kamati za masheha za shehia.

JEE HALI HALISI IKOJE KWENYE KAMATI ZA SHEHIA ZA MICHEWENI

Mkoa wa Kaskazini Pemba unaoundwa na wilaya mbili za  Wete na Micheweni, ambapo Micheweni pekee inazo shehia 25 zenye wajumbe wa kamati 260.

Kati ya wajumbe hao wa kamati 260 wanaume ni 150 wanawake wenye ulemavu ni watatu tu (3), kati ya wajumbe wanawake 110 sawa na asilimia 2.7 ya wanawake hao.

Sheha wa Tumbe Magharibi, Masoud Khamis Hamad anasema kamati yake inao wajumbe 12, ikiwa na idadi sawa  ya wanawake na wanaume

‘’Ni kweli ndani ya hawa wajumbe sita wanawake, hakuna hata mmoja, mwenye ulemavu, na nahisi sio kwamba hawawezi, bali nimekosa uzingatiaji,’’anakiri.

Hamad anasema hajamshirikisha mwanamke mwenye ulemavu  katika kamati yake, kwani anahisi hawatoweza kufanya kazi kutokana na hali zao.

Sheha wa Mtemani wingwi Mohamed Ali Kombo anasema kamati yake inayo wajumbe 10 idadi ya wanaume na wanawake ikiwa sawa, ingawa anae mmoja mwanamke mwenye ulemavu.

Sheha Mohamed anasema kati ya wajumbe hao wote 10, huyo mwenye ulemavu ndio ambae akimpa kazi ndie anaeifanyakazi kwa umakini na kwa wakati.

‘’Mjumbe huyo mwenye ulemavu nimemueka kama kumjaribu tu, ingawa naona mtndaji mzuri kuliko wajumbe wote, nimevutiwa na sasa ninampango wa kuongeza mwengine,’’anaeleza.

Sheha wa Chamboni Bikuu Juma Alawi anasema hajamshirikisha mwanamke mwenyeulemavu katika kamati yake, kwani alikua hana elimu kwamba wenye ulemavu na wao wana uwezo wa kufanya kazi.

‘’Muwandishi ushaniamsha na sasa nitamtafuta mwanamke mwenyeulemavu nimueke kwenye kamati yangu nafikiria ataweza,’’anasema.

Sheha wa Shumba vyamboni Time Said Omar anasema anao wajumbe tisa, kati ya hao anae mmoja mwanamke mwenye ulemavu na tena ameupata akiwa kashakua mwanakamati.

WANAKAMATI

Fatma Rashid Abdullah mwanakamati shehia ya Sizini anasema bado wanawake wenyeulemavu, hawajashirikishwa ipasavyo katika kamati hizo.

‘’Nikweli wanawake wenye ulemavu kwenye kamati zetu hizi tumewasahau, na nnaimani wakipewa nafasi watafanya vizuri kuliko sisi tusio na ulemavu,’’anasema.

Maryam Hassan Abdallah (23) mwenye ulemavu wa viungo  ambae ni mwanakamati ya Shehia ya Mtemani anasema mwanzoni amepatashida, ingawa kwasasa amekua akishirikiana na wenzake katika utekelezaji wa kazi zao.

‘’Sijatengwa, sijabaguliwa, nafanyakazi sawasawa na wajumbe wenzangu,’’anasema.

Ali Omar Ali ambae ni mmoja wa wanakamati hiyo ya Mtemani anasema mjumbe huyo mwenye ulemavu amekua akifanya kazi wakati wowote, haijalishi kuna malipo ama hakuna.

‘’Kwa kweli mwenzetu huyo ni mchapa  kazi, haangalii kama kuna malipo ama kuna nauli, nnaimani kama baadae huo usheha hatoupewa yeye,’’anafahamisha.

Katibu Tawala wilaya ya Micheweni Sheha Mpemba Faki anasema kamati zote zimekua zikifanya vizuri, ila kamati ya Sheha wa Mtemani imekua ikifanya vizuri kulikoa kamati zengine, huyu mjumbe mwanamke mwenye ulemavu ndie anaechangia hilo.

 ‘’Tunae mwanamke mmoja mwenye ulemavu katika Kamati ya shehia ya Mtemani, imekua ikifanya vizuri, sijawahipo hata siku moja kupewa kesi kwamba wamegombana na Sheha wao,’alieleza.

JAMII

Rabia Alei Salim (42) mwenye ulemavu wa ngozi mwananchi kutoka Wesha, anasema sio kamati za Micheweni pekee ambazo inaonekana wanawake wenye ulemavu ni kidogo, hata za wilaya nyengine, hali inafanana.

Anasema kamati ya Sheha wa Wesha inayowajumbe 10 ingawa hakuna hata mwanamke mmoja mwenye ulemavu wa aina yoyote.

 ‘’Binafsi sheha wangu, aliniambia anataka aniweke kwenye kamati, ingawa hakuniweka bado hawajatuamini, wanahisi sisi hatuwezi,’’anasema.

Maryam Nuhu Hamad Kutoka Ole anasema, ushiriki wa wanawake wenye ulemavu katika nafasi za uongozi, bado ni mdogo, kuanzia ngazi za chini, ikiwemo usheha hadi juu.

‘’Sio kwenye kamati tu bali hata ngazi nyengine bado mambo ndo hayohayo,’’anafahamisha,’’.

SERIKALI

Mwanaisha Ali Masoud Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na watoto Pemba anasema usawa wa kijinsia unahitajika kuanzia hata kwenye ngazi ya familia, ili kujenga miundimbinu rafiki ya ushirikishwaji.

‘’Tunatoa mafunzo mbalimbali kwa jamii, kuona wanawake wote wanapata uwelewa juu ya umuhimu wa ushiriki  wao katika ngazi zote za maamuzi,’anaeleza.

Salma Haji Saadat aliekua Mwenyekiti wa Baraza la watu wenye ulemavu Zanzibar anasema moja ya mkakati wa serikali nu kuondoa ubaguzi, na kuongeza ushirikishwaji wa watu wenye ulemavu katika ngazi za maamuzi kutoka asilimia 2 hadi 5 ikifikapo mwaka 2030.

Mashavu Juma Mabrouk ni Mratibu kutoka Baraza la watu wenye ulemavu Pemba, anasema bado wanawake wenyeulemavu hawajaonekana katika fursa hasa kwenye nafasi za maamuzi, ambapo hupelekea sikuzote kubaki mkiani na kuchelewa kufikiwa na maendeleo.

WANAHARAKATI

Juma Kombo Hija Katibu wa Jumuia ya wanawake wenye ulemavu (JUWAUZA) upande wa Pemba anasema hata katika ngazi za chini wanawake wenye ulemavu wamekua wakisahauliwa kwenye teuzi mbalimbali.

 ‘’Sio kwenye kamati peke yake hata hao masheha, kwa mfano katika masheha 25 wa wilaya ya Micheweni, na 32 wa wilaya ya Wete hakuna hata mmoja mwanamke mwenye ulemavu,’’ anasema.

Pia wilaya hiyo hiyo ya Micheweni inayo Madiwani 15 nane wa kuchaguliwa, watano wa kuteuliwa, na wawili viti maalumu, ingawa hakuna hatammoja mwanamke mwenye ulemavu.

Hata Madiwani wa Wilaya ya Wete wapo 19 ingawa hakuna hata mmoja mwanamke mwenye ulemavu.

 Ikiwa kwa  Zanzibar wapo masheha 388 wanawake 81 wanaume 307 huku madiwani wanawake wakiwa ni 27 kati ya Madiani wote 110.

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano kutoka TAMWA Zanzibar  Sofia Ngalapi anasema idadi ya wanawake wenye ulemavu ni ndogo katika yanja zote za maamuzi, na hii ni kutokana na mitazamo kwa baadhi ya watu juu ya watu hao.

‘’Wapo wenye ulemavu katika baadhi ya tasisi na wamekua wakifanya  vizuri zaidi kuliko na wasio na ulemavu,’’anaeleza.

Anasema kwa mujibu wa ripoti walioifanya inaoneonesha kwamba idadi ya wanawake Zanzibar katika maamuzi bado ni ndogo, kwani ni asilimia 38 tu.

 Sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 inaendelea kuwabeba wanawake kwani inaonesha wako  asilimia 51 ambao ni wengi ukilinganisha na wanaume

Huku wanawake wenye ulemavu Zanziba wapo asilimia 11.4 kati ya watu milioni 1.8.

Anaendelea kusema  kutokana na hilo wamekuja na mradi wa Wanawake Viongozi kwa ajili Usawa, Uwajibikaji na  Demokrasia (W-LEAD) unaolenga kuimarisha nafasi za uongozi na ushiriki wa wanawake, hususani wanawake vijana na wanawake wenye ulemavu, katika mifumo ya kidemokrasia na kushika nafasi mbalimbali za maamuzi.

Mradi huo wanautekeleza kwa ushirikiano na Jumuia ya wasiona (ZANAB), chuo kikuu cha  Taifa cha  Zanzibar (suza) na Zanzibar University (ZU)  chini ya ufadhili wa   Umoja wa Ulaya kupitia mpango wa Ushiriki wa wanawake na Vijana katika Demokrasia na  kuanza utakelezwaji wake  mwaka huu  2026 hadi 2027.

ATHARI YAKE

Hafidh Abdi Said Mkurugenzi mtendaji kutoka Pegao, anasema endapo wanawake wenye ulemavu hawatoshirikishwa kwenye maamuzi, watakosa mtetezi wa kuwasemea shida zao, na kupelekea siku zote kuishi kinyonge.

NINI KIFANYIKE

Hidaya Mjaka Ali mwenye ulemavu wa viungo anasema Ipo haja kwa sasa kuona wanawake wenyeulemavu  wanashirikishwa katika maamuzi, na kutetea kero zao na kupata haki zao,’’wanasema wanaharakati wa haki za watu wenye ulemavu.

MWISHO.

 

 

 

Comments

Popular posts from this blog

WANDISHI WA HABARI ANDIKENI HABARI ZA UCHAMBUZI

HOFU YA UDHALILISHAJI MTANDAONI INAVYOWANYAMAZISHA WANAWAKE

UROHO WA MALI KWA WANAUME UNAVYONYIMA WANAWAKE ARDHI