SAFARI YA WANAWAKE WENYE ULEMAVU KUELEKEA UONGOZI
NA FATMA HAMAD,PEMBA
Kadri Tanzania
inavyoelekea katika uchaguzi kuu kunakua na mijadala mingi kuhusu ushiriki wa makundi
maalum hasa Wanawake Wenye Ulemavu.
Kwani ni muda mrefu kundi hili linakuwa likipigania
nafasi sawa katika siasa, uongozi na maamuzi, safari yao inaendelea kuwa yenye
milima na mabonde, ingawa mwakahuu inaonesha matumaini.
Nasra Fakih Hassan mwanamke mwenye ulemavu wa mguu mzaliwa wa Kangagani Wete Pemba , ambaye
amejitosa kugombea nafasi ya uwakilishi viti maalumu, anasema mchakato wa
uchaguzi umewaonesha matumaini, ingawa bado unahitaji mageuzi kwa watu wenye
ulemavu
‘’Mara hii tunashukuru na ndio maana wanawake wengi wenye
ulemavu tumejitokeza kuchukua fomu na kuwania nafasi mbali mbali za uongozi, ingawa
si hayo tu bali hata kwenye kampeni tunashiriki kwa wingi na kusikiliza sera za
wagombea,’’anasema.
Nasra anabainisha kuwa, licha ya changamoto hizo, mwaka huu
anaona hatua za matumaini, hasa baada ya Baraza la Watu Wenye Ulemavu Zanzibar
kushirikiana na Tume ya Uchaguzi (ZEC) kutoa elimu ya uraia na kuhimiza
ushiriki wa watu wenye ulemavu.
Halima Suleiman Ali mkazi wa Mtambile amejitosa kuania udiwani Wadi ya Mtambile anasema
uchaguzi unaonesha mwanga kwao, kwani wanawezeshwa kimafunzo, amekua na
uthubutu, amejitokeza kwenye kinyn’ganyiro cha kuwania uongozi.
‘’Sijawahipo hata siku moja kuchukua fomu, ila
Kutokana na ushirikishwaji kupitia mashirika na jumuiya mbalimbali mwaka huu nimethubutu kujitupa jimboni na
kuusaka udiwani, ingawa sikufanikiwa”
Kwa upande wake Amina Abdala Saidi mwenye ulemavu wa viungo mteule
wa nafasi ya udiwani viti maalum, kupitia Chama cha ACT WAZALENDO Wadi ya
Changaaweni Mkoani Pemba, anasema uchaguzi wa mwaka huu 2025, baadhi ya mambo
yamebadilika, na ndio maana akafanikiwa kupata nafasi hiyo.
‘’Nashukuru sijabaguliwa wananiona nafaa, na hata
kwenye kampeni nachukuliwa siku zote, bila vikwazo vyovyote,’anafahamisha
Amina anasema yapo mambo kadhaa ambayo yanafanya Wanawake Wenye
Ulemavu kuonekana hawawezi kushiriki kikamilifu kwenye chaguzi, Kuanzia gharama
za uchukuaji wa fomu, kampeni hadi upigaji kura.
‘’Katika chaguzi zilizopita hata baadhi ya vituo vya uchaguzi havikua na mazingira rafiki kwa Mtu Mwenye Ulemavu,
ingawa uchaguzi huu tunaimani mambo yatabadilika,’’anasema.
JAMII
Katika mazungumzo na baadhi ya wakazi wa Unguja na Pemba, wengi
wanakiri kuona hamasa kubwa ya wanawake wenye ulemavu kushiriki katika harakati
za kisiasa.
Ali Otman Bakari mkaazi wa Unguja na Asha Ali mkaazi wa Ziwani
Pemba, wanasema kundi la Watu Wenye Ulemavu linaonekana kwa wingi kwenye
kampeni.
Wanasema moja ya sababu inayochangia kushiriki kwenye kampeni
hizo ni mazingira rafiki ya Uchaguzi ya kupewa elimu kufahamu haki zao,
sambamba na Amani na utulivu uliopo.
“Ni vizuri kuona kundi la
watu hawa wanashiriki harakati zote za chaguziji, kwani wanaonyesha uwezo wao,
ingawa bado jamii yetu inahitaji elimu zaidi juu ya kuzifahamu haki, fursa za
watu Wenye Ulemavu,”wanaeleza.
WANAHARAKATI
Hidaya Mjaka Ali, mwanaharakati kutoka Jumuia ya Wanawake Wenye Ulemavu
Zanzibar JUWAUZA anasema uchaguzi wa 2025, mambo yamebadilika, na kupelekea jumla ya
Wanawake Wenye Ulemavu 12 kujitosa na kuchukua fomu za kuwania uongozi, ambapo
haijawahi kutokea.
“Ni kweli, Tume ya uchaguzi Zanzibar ZEC wanaanza kujumuisha
vipengele vya upatikanaji wa huduma kwa Watu Wenye Ulemavu kwenye sera zao za
uchaguzi, ingawa utekelezaji wake bado ni changamoto,’’anasema.
Kampeni zimekua za kistarabu hakuna vurugu, jambo linalowapa
hamasa Watu Wenye Ulemavu kushiriki kwa wingi kwenye kampeni kusikiliza sera za
wagombea, ambao ni nadra kwa chaguzi
zinazopita.
Mashavu Juma Mabrouk kutoka Baraza la Watu Wenye Ulemavu
Zanzibar Ofisi ya Pemba, anasema hali ya mwaka huu inaonyesha mabadiliko,licha
kwamba bado kuna ukakasi.
“Wakati mwingine wananyimwa nafasi si kwa sababu hawawezi, bali
jamii haijaamini uwezo wao, hilo ndilo tunalopigania kulibadilisha mwaka huu,”
anafahamisha.
Chama cha Wandishi wa Habari Wanawake Tanzania TAMWA
Zanziba kimekua kikichukua hatua mbali
mbali, kuona wanawake wenyeulemavu wanapewa nafasi sawa, mafunzo na katika
michakato ya kampeni na uchaguzi.
‘’Tumeona marahii hali inaonesha matumani, uzuri zaidi ni kuona
kuna baadhi ya vyama vya siasa vikichukua wakalimani katika kampeni, jambo
ambalo linapaswa kuigwa kwa vyama vengine,’’anasema Amina Ahmed kutoka Tamwa
Zanzibar Ofisi ya Pemba.
Anasema huu ni mwaka wa mabadiliko wamechoka kuona wanawake
wenye ulemavu wakitazamwa kama wakulima wa pembezoni, wanataka wawe viongozi,
wabunge, wawakilishi, na hata mawaziri.
Afisa mfawidhi kutoka Tume ya Haki za
Binadamu Ofisi ya Pemba Suleimana Salim
Ahmad anasema kufuatia mabadiliko
yanayofanywa na kuona ushiriki mzuri wa watu wenye ulemavu katika upigaji
kura,ni vizuri vyama vya siasa kuweka ujumuishi wao katika kampeni
zinazoendelea.
‘’Pamoja na jitihada zinazofanywa, bado
baadhi ya vyama vya siasa, havijazingatia ipasavyo mahitaji ya watu wenye
ulemavu katika mikutano yao, suala ambalo linawanyima haki yao ya msingi ya
kufuatilia sera za vyama zitakazo wasaidia
kufanya maamuzi sahihi ya kura zao,anasema.
Anasema mazingira mazuri katika mikutano ya kampeni, inasaidia
kufuatilia sera zinazotolewa na vyama vya siasa katika nafasi za Ubunge,
Uwakilishi na Udiwani, ambapo itasaidia
kuwachagua viongozi wanaowataka.
VIONGOZI WA VYAMA VYA
SIASA
Mgombea Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya chama cha Alliance for Democratic
Change ADC Hamad Rashid Moh’d anasema katika chama chake wameweka
miundombinu maalumu kwa watu wenye ulemavu,ili washiriki mikutano ya kampeni
ikiwemo, usafiri.
Pia
anasema katika mawakala wao watakaosimamia uchaguzi mkuu, wameweka nafasi
maalumu kwa watu wenye ulemavu.
KAULI YA RAIS
Mgombea wa Urais wa Zanziba kupitia chama cha
Mapinduzi CCM ambae pia ni Rais wa Zanzibar Ali Hassan Mwinyi anasema wakati
atakapopata ridhaa na kuingia madarakani, ataimarisha ustawi wa jamii,
kupunguza ubaguzi, na kujenga Zanzibar inayompa kila mtu nafasi ya kufikia
ndoto zake bila kikwazo, kulingana na hali yake ya kimwili na mahitaji yake.
Pia anasema ataongeza nafasi
za ajira na uteuzi kwa watu wenye ulemavu, ili nao wawe sehemu ya maamuzi.
TUME YA UCHAGUZI ZANZIBAR
Juma Msanif Sheha Mkuu wa Programu kwa wapiga kura na msimamizi kutoka
Tume ya Uchaguzi Zanzibar ZEC anasema ili kuona Watu Wenye Ulemavu wanashiriki kwenye harakati zot za uchaguzi
wamekua wakiwapatia elimu, kufahamu haki na wajibu wao katika kipindi chote cha
chaguzi.
‘’Tunawapa elimu ya uraia, wafahamu haki zao, kuona hawaachwi
nyuma katika harakati zote za uchaguzi.
Sambamba na hilo anasema wamejipanga kuweka wakalimani, mashine
ya nukta nundu vitambulisho maalumu kwa ajili ya Watu Wenye Ulemavu katika vituo
vyote vya kupigia kura, ili kuwarahisishia kupata haki yao ya kikatiba ya
upigaji kura bila vikwazo.
TAKWIMU
Jumla ya Watu 7891 Wenye Ulemavu wanatarajiwa kupiga kura, ikiwa
Wenye Uwalbino ni 100, Wasiona 655, Viziwi 1573 na Uoni hafifu ni 2325.
Ambapo wenye Ulemavu wa
viungo ni 1998, huku Wenye Ulemavu mchanganyiko ikiwa ni 1240.
MIKATABA
Sheria
ya Watu Wenye Ulemavu Zanzibar Namba 8ya mwaka 2022, kifungu cha 20 kinaeleza
umuhimu wa watu wenye ulemavu kuweza kufikia miundombinu mbali mbali, pamoja na
taarifa, mawasiliano na haki zote za kibinadamu na za msingi.
Aidha, Tanzania
imeridhia Mkataba wa Umoja wa
Mataifa wa Haki za Watu Wenye Ulemavu (CRPD), unaohimiza serikali
kuhakikisha ushiriki sawa wa Watu Wenye Ulemavu katika siasa na maamuzi.
Hata
Mkataba wa kimataifa wa haki za kiraia na haki za kisiasa ya mwaka 1966 kifungu
cha 25, kila raia ana haki ya kupiga kura na kuchaguliwa katika uchaguzi wa
kweli, wa haki na wa mara kwa mara, uliofanywa kwa kura ya siri na kuhakikisha
uhuru wa wapiga kura.
Hata Katiba ya Zanzibar
ya 1984, ambayo ndo sharia mama, kupitia kifungu chake cha 21(1) nacho kinatambua haki ya kila raia
kushiriki katika shughuli za utawala wa nchi bila ubaguzi.

Comments
Post a Comment