KAMPENI ZA UCHAGUZI 2025, FURSA MPYA KWA WANAWAKE PEMBA

 


               NA FATMA HAMAD, PEMBA

WAKATI kampeni za uchaguzi mkuu wa 2025 zikiendelea kupamba moto kila kona kisiwani Pemba, wananchi wanamiminika kwa wingi kusikiliza sera za viongozi wao, huku wakiwa na biashara zao ndogo ndogo.

Hiyo inaonesha wazi kwamba siasa siyo tu mjadala wa kura na wagombea, bali pia ni chanzo kipya cha ajira na kipato kwa wanawake.

Fursa mbali mbali za kibiashara zinapatikana katika mikutano ya kampeni kwa wauzaji wa chakula, mafundi vyarahani, hata kwa wanawake wanaofanya kazi kwenye sekta za utalii na huduma.

Kwani, wengi wanasema kampeni zimewafungulia milango ya biashara na kuleta matumaini katika mifuko yao.

Kipindi cha kampeni kila mkutano ni fursa ya kipato kwani watu hupata kusikiliza sera za wagombea, huku wakiwa na biashara zao mikobani.

Katika mkutano wa kampeni wa chama cha Alliance for  Democratic Change ADC uliofanyika Mchangamdogo, mwandishi alikutana na muuza juisi na malai Asha Khamis Sheha mkaazi wa Gombeume, anasema ni kawaida yake kufanya shughuli zake hizo za biashara katika mikutano ya kampeni.

‘’Mara nyingi nakwenda kwenye mikutano ya kampeni kusikiliza sera za wagombea, lakini huwa nachukua biashara zangu, nashukuru kwa sababu imenisaidia sana kupata pesa za matumizi,’’ anasema.

Raya Ali Mohamed mkaazi wa Chake Chake ambae ni mjasiriamali wa kuuza vyakula kama maandazi, chapati, supu na ugali, anasema kampeni kwake zimekua zimemchanyua kiuchumi kwani zimekuwa msimu wa mavuno kwake.

‘’Natamani hizi kampeni zisimalize, kwani mauzo ya biashara zangu yameongezeka, kwa siku nauza mpaka laki 500,000, ambapo kabla ya msimu huu napata laki mbili ama tatu tu,’’ anasema.

Kutokana na wageni wanaoingia kwa ajili ya shughuli za kampeni, uuzaji wa bidhaa umeongezeka, hivyo kampeni zimeinua kipato chao kwa asilimia kubwa.


Hamad Omar Othman mkaazi wa Sizini Kijichame mwenye umri wa miaka 25, yeye anauza biashara ya karanga (njugu nyasa) anasema, mikutano ya kampeni ni fursa kubwa kwake ya kujiinua kiuchumi.

Anasema, tangu zilipoanza harakati za kampeni, ameshauza karanga za zaidi ya shilindi laki moja, ambapo zamani zilikuwa hazinunuliwi sana.

‘’Sio wanawake pekee wanaonufaika na uuzaji wa bidhaa kwenye mikutano ya kampeni bali hata sisi pia zinatusaidia kuinua kipato, kwani biashara zetu zinapata sokola uhakika,’anasema.

Hamad anasema, matumaini yake hata zikimaliza kampeni ni kuwa na mtaji mkubwa wa kufungua genge, ili aongeze biashara nyengine.



MAFUNDI VYARAHANI

Hadia Faki Juma mkaazi wa Micheweni anasema tangu kuanza kwa kampeni, kazi za ushonaji zinaongezeka mara dufu.

“Kampeni zimekua na baraka kwangu, kwani naletewa matenge nashona mashati, madira na suruali, imenisaidia kulipa kodi na shida zangu nyengine najitatulia mwenyewe,” anasema kwa tabasamu.

Hata vijana wanaofanya kazi za kuchapisha mabango, bendera, mikoba ya wagombea na fulana nao wanasema wanapata kipato kizuri kuliko miezi mingine ya kawaida.

Khamis Khamis mkaazi wa Chake Chake ambae anachapisha mabango, bendera na fulana anasema, kampeni imeinua kipato chake, kwani kwa kipindi hiki kazi za uchapishaji zinaongezeka.

‘’Hata kampeni zikimalizika nategemea kuzikamata zaidi ya shilingi milioni mbili na fedha hizo nategemea kununua mashine nyengine kubwa ya kuchapishia, ili biashara iendelee kukua,’’ anasema.

Anasema, kampeni sio tu kwa ajili ya chaguzi bali ina fursa nyingi, kwani wanawake wengi wameanzisha biashara, hivyo wameondokana na utegemezi.

SEKTA YA UTALII NAYO YAFAIDIKA

Mratib wa Idara ya Makumbusho na Mambo ya Kale Pemba Saleh Hamad Juma anasema, katika kipindi cha kampeni wanajivunia, kwani idadi ya wageni inaongezeka siku hadi siku na kuingiza kipato.

‘’Kampeni zina faida nyingi, zinachangia uchumi wa wananchi na Taifa, idadi ya wageni inaongezeka siku hadi siku, hii ni kutokana na amani iliyopo licha ya kua ni kipindi cha uchaguzi, hii ni fursa ambayo hatujaiona muda mrefu,’’ anasema.

Anasema, Hoteli zimejaa, migahawa inafanya kazi usiku na mchana, hivyo wanawake wanaofanya kazi katika sekta ya malazi na chakula wanapata kipato kizuri.

‘’Mbali na hayo hivi sasa tumeshapokea barua kwamba Oktoba 27 mwaka huu kuna meli ya wageni zaid ya 300 ambao wanakuja kutembea hapa kwetu Pemba,’’ anamalizia.

VIONGOZI WA SERIKALI

Mwanaisha Ali Masoud ni Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto Pemba, anasema Serikali inatoa mikopo kwa wanawake, ili wafanye biashara kwa ajili ya kuinua kipato chao.

‘’Kuna mikopo maalumu ambayo inaletwa na Dk. Hussein Ali Mwinyi ambao unawasidia wanawake kufanya biashara zao ndogo ndogo na kwa sasa wanauza mpaka kwenye mikutano ya kampeni,’’anasema.

Afisa huyo anafafanua, licha ya hayo bali wanatoa elimu kwa wanawake juu ya kujikinga na vitendo vya udhalilishaji, ambavyo vinakua vikijitokeza katika kipindi cha kampeni.

“Kupitia kampeni, tunapata fursa ya kuzungumza na wanawake wengi wa vijijini, wa mjni, kujikinga na vitendo vinavyochochea vya udhalilishaji, ikiwemo kuvaa nguo za stara wanapokwenda mikutanoni,’’anasema.

SHUHUDA WA MKOPO

Habiba Jabu Dawa mama wa watoto sita mkaazi wa Sizini Micheweni Pemba anasema, amepata mkopo wa shilingi laki tano ambapo anatengeneza Juisi, ubuyu, kachori ambazo anauza dukani kwake na kwenye mikutano ya kampeni.

‘’Uchumi wangu unakua kipindi hichi, kwani biashara zangu zinatoka zote, soko langu kubwa ni kwenye mikutano hii ya kampeni,’’anasema.

Anasema, hata zikimaliza kampeni anatarajia kuwanunulia  watoto wake nguo za skukuu, pamoja na vifaa vya skuli kama vile sare na viatu.  

ZEC

Juma Msanif Sheha Mkuu wa Programu kwa wapiga kura na msimamizi kutoka Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) anasema, uchaguzi na kampeni inatoa fursa mbali mbali kwa wanawake na makundi yote kiujumla.

‘’Tunatoa mafunzo mbali mbali kwa wanawake na kwa wananchi wote kiujumla, wafahamu haki na wajibu wao katika masuala ya uchaguzi,’’ anafahamisha.

Anasema, watahakikisha wanazingatia usawa wa kijinsia, wakati watakapota ajira za muda za usimamizi wa uchaguzi, ili kupata uzoefu utakaowasaidia hata baada ya uchaguzi.

WANAHARAKATI

Amina Ahmed Mohamed Kaimu Mratib wa Chama cha Wandishi wa Habari Wanawake (TAMWA) Zanzibar anakiri kwamba kampeni zina fursa ambazo zinasaidia kuinua uchumi wa wanawake, ingawa wapo waliokua hawajawa na muamko wa kuzitumia nafasi hizo.

‘’Wapo wanawake wanaokwenda kusikiliza sera za wagombea huku wakiuza bishara, ambazo zinawainua kiuchumi, ijapokua bado kuna kundi kubwa ambalo halijafahamu, bali wanakwenda kwa ajili ya burudani tu,’’anasema.

Anasema, wamekua wakitoa elimu kwa wanawake wa maeneo ya Pemba kuona wanaitumia fursa hiyo kwa kuwania nafasi za uongozi, kuhudhuria kwenye kampeni kusikiliza sera, sambamba na kuuza biashara na kupata pesa za kujiinua kiuchumi.

 Mwanaharakati Hafidh Abdi Said kutoka Jumuia ya PEGAO anasema, kampeni za mwaka huu zinaonyesha picha mpya ya mwanamke wa Pemba.

“Wanawake sasa si watazamaji tena, wanauza bidhaa, wanapanga shughuli zote za mikutano, siasa zinawapa kipato na ujasiri,” anasema.

Anaishauri Serikali na vyama vya siasa visiwaache baada ya uchaguzi, bali viwashirikishe.

“Wakitambuliwa rasmi, hawa wanawake wanaweza kubadili uchumi wa Pemba kabisa,” anaongeza.

Anaendelea kusema, kampeni za uchaguzi mkuu 2025 zimekuwa zaidi ya siasa, kwani imekuwa darasa la uchumi kwa wanawake wa Pemba, zinawafunza kuishi kwa kujitegemea, kushirikiana na kuthamini nafasi yao katika maendeleo.

               

 

Comments

Popular posts from this blog

KERO YA MAJI, TATIZO KWA WANAKIJIJI CHA GOMBEUME

HIVI NDIVYO UTELEKEZWAJI WA WATOTO UNAVYOATHIRI MALEZI, MAKUZI YAO

DNA YA THIBITISHA, MTUHUMIWA NDIE BABA MZAZA WA MTOTO