Naibu Chauma asema: ‘’Chagueni viongozi wenye imani na Nchi yao’’
Wananchi
wametakiwa kuwachagua viongozi
ambao wanauthubu na wenye
uzalendo na nchi yao, wanaoweza kusimama na kutetea shida zinazowakwaza
wananchi wao.
Kauli hiyo imetolewa na Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha
Ukombozi wa Umma Chauma Zanzibar, Mohamed Masoud Rashid wakati akizungumza na wanachama na wananchi wa
chama cha Chauma, katika uzinduzi wa kampeni za wagombea wa Ubunge, Uwakilishi
na Udiwani huko Tumbe wilaya ya Micheweni kisiwani Pemba.
Alisema wakati umepita wa kuchagua viongozi kwa ajili ya
chama ama kwa cheo chake, bali ni vyema kuhakikisha wanawachagua ambao
wanauchungu na nchi yao na wanauwezo wa kutetea kero za wananchi, sambamba na
kuwaletea mabadiliko.
‘’Nduguzangu wanatumbe badilikeni msichague viongozi ambao hawana
maendeleo, isiwe wanaishia kupiga kofi tu kwenye meza,’’alisema.
Aidha alisema endapo chama chao kitaingia madarakani, jambo
la kwanza watakalolifanya ni kushusha bei za vyakula, ili kuona kila mwananchi
anakula mlo uliotimia.
‘’Bado wananchi wetu wanakabiliwa na tatizo la lishe duni,
hivyo mkituchagua tutahakikisha kila mwananchi anapata chakula cha asubuhi,
mchana, usiku na kilichokamilika,’’alieleza.
Mapema Mwenyekiti wa Vijana wa Chauma Zanzibar Fatma Omar
Salim, aliwataka vijana kuwachagua viongozi wa Chama hicho, ili wawaletee
mabadiliko.
Alisema vijana wengi wamekua wakizurura ovyo mitaani kutokana
na kukosa ajira, hivyo endapo watakipigia
kura chama cha Chauma, kitaondosha ubaguzi na kuleta miradi ya maendeleo
ambayo itatoa ajira, na vijana watajikomboa kiuchumi.
‘’Chama cha Chauma ndio mkombozi pekee kwa vijana, hivyo
kichagueni ili mjemfaidi matunda yake,’’alieleza.
Fatma Yussuf Mohamed Katibu Mkuu Ngome ya wanawake Zanzibar
alisema Sera za Chama chao zimeonesha
dhamira njema za kutaka kuwakomboa wananchi na janga la njaa, umasikini.
Alisema endapo wananchi watakiunga mkono kwa kukipa kura za
ndio, suala la umasikini wa kipato kwa mtu mmoja mmoja litabakia historia.
Kwa upande wake Makamo Mwenyekiti wa Chama cha Chauma
Zanzibar, Issa Abass Hussein aliwanasihi
wananchi kuhakikisha wanawachagua viongozi ambao ni wazawa, wanaozifahamu shida
zilizomo kwenye majimbo yao, na sio kuwachagua kwa sababu ya kipato chao.
‘’Niwaombe ndugu zangu asije mtu akawadangaja kwa pesa ya
maramoja, wachagueni nduguzenu wanazijua kero zenu, ili wapate kuzisemea na
kutatuliwa,’’alisisitiza.
Aidha kwa upande mwengine aliwataka wananchi hao kuwapigia
kura viongozi wanawake katika majimbo yao wawaletee mabadiliko, kwani wao ni
wapenda maendeleo, Amani na ushirikiano na ni waaminifu.
Walisema walishachokana na ahadi za uongo ambazo wamekua
wakiwekewa na viongozi waliopita, hivyo watahakikisha wanakipa kura Chama
hicho, kiweze kuwapatia mahitaji yao wanayoyahitaji ikiwemo ajira.
.jpg)

Comments
Post a Comment