KISIWAPANZA WALILIA HUDUMA ZA MAMA NA MTOTO
NA FATMA HAMAD, PEMBA
WANANCHI
WA Kisiwapanza wilaya ya Mkoani Mkoa wa Kusini Pemba, wamelalamikia juu ya
ukosefu wa huduma za uhakika kwa wajawazito katika kituo chao cha afya, jambo linalopelekea kuhatarisha maisha ya
mama na mtoto wakati wa kujifungua.
Walieleza kuwa katika kituo
chao huduma za mama na mtoto bado hazijakua rafiki kwao, kwani kituo kizima kuna muhudumu mmoja tu ambae
anazalisha, na huenda wakati wa mchana tu.
Walisema endapo mzazi atapata
tatizo wakati anapokwenda kujifungua kituoni hapo, ama atakapoumwa na uchungu
wakati wa usiku hulazimika kuvuushwa baharini na kupelekwa Hospitali kuu ya
Abdallah mzee Mkoani, ambapo wengi hujifungulia
ndani ya boti, hali inayopelekea kuhatarisha usalama wa mama na mtoto.
‘’Kituo kizima daktari
anaezalisha ni mmoja ivo vifaa vyenyewe navyo havipo vya kutosha, na ikifika
jioni anaondoka ikitokezea mjamzito akiumwa usiku inabidi tumtie kwenye kidau
ama kiboti tuvuuke nae tumpeleke Abdala mzee, ambapo wengi huzaa humo baharini
hawawahi kufika huko Mkoani,’’walieleza.
Wananchi hao walitoa kero hiyo
mbele ya mwandishi wa Habari hizi huko kijijini kwao kisiwapanza, walisema ingawa kituo cha afya kipo lakini
bado huduma za kujifungulia kwa mama
wajawazito bado hazijaridhisha.
Khadija Othman Haji ambae ni
mmoja wa shuhuda aliepata tatizo wakati wa kujifungua, alisema kutokana na kukosekana kwa huduma ya uhakika
kituoni hapo kulimsababishia kupoteza damu nyingi wakati wa kujifungua, jambo
ambalo lilipelekea kukimbizwa katika Hospital kuu ya Abdalla Mzee.
Hivyo kutokana na kadhia hiyo
ambayo imekua ikihatarisha maisha yao na vizazi vyao, ameiomba serikali kupitia Wizara ya Afya kuwapatia
madaktari wa kutosha katika Hospitali hiyo ili wapate huduma ya kujifungulia.
Sheha wa kisiwapanza Haji Ali
Shaali amekiri kuwepo kwa changamoto hiyo
kwa akina mama kujifungulia mbali na kituo hicho.
Alisema tayari ameshachukua
hatua ya kufikisha maombi katika sehemu
husika kwa lengo la kupatiwa utatuzi wa changamoto hiyo.
Kwa upande wake Muhudumu wa
Afya wa kituo hicho Haroub Makame ameiomba
serikali kuweka kipaombele chao katika Kijiji cha kisiwa panza, sambaba na kuwapatia
madaktari wa kudumu ambao ni wazawa wa shehia hiyo.
‘’Kwa kwaeli wanawake wa
kisiwapanza wanateseka, tunaomba serikali ilete madaktari kwa ajili ya kutoa
huduma za mama na mtoto, ili kuepusha vifo vitokanavyo na uzazi,’’.
Nae Afisa Mdhamini wizara ya
Afya Khamis Bilali Ali amekiri kuepo kwa tatizo hilo kisiwani
humo.
Allisema kisiwa hicho kimo
katika mpango wa kujengewa kituo chengine ambacho kitakua kinatoa huduma za
mama na mtoto kwa masaa 24.
‘’Tunategemea mwishoni mwa
mwaka huu ujenzi wa kituo chengine
ambacho kitakua na madaktari wa kutosha wa huduma za mama na mtoto, ili
kuondosha usumbufu huo kwa wananchi hao,’’alisema.
Alisema kituo hicho kitakua na
nyumba za madaktari, ambao watalala hapohapo ili huduma za mama na mtoto ziwe
zinapatikana kwa wakati wote.
Alisema pia kutakuwepo na
Maboti maalumu ya dharura, ambayo yatabeba wajawazito ambao watakua na tatizo
la kupelekwa Hospitali kubwa ya Abdala Mzee Mkoani.
Moja ya kipaumbele cha Bajeti ya Wizara ya Afya ya mwaka
2024/2025, ni kuimarisha miundombinu ya Afya katika ngazi zote za utoaji wa
huduma za afya.
Pia moja ya mpango mkakati wa Sera ya Afya Zanzibar
Kupanua dhana ya afya ya msingi na kuwa na huduma bora za afya zinazoendana na
wakati, endelevu na zinazowafikia wananchi wote.

Comments
Post a Comment