WAJASIRIAMALI WATAKIWA KUJIUNGA NA MAJUKWAA YA WANAWAKE
NA, FATMA HAMAD-PEMBA
Mkurugenzi Idara ya Maendeleo ya Jamii Jinsia wazee na Watoto Zanzibar Siti Abasi Ali amewataka Viongozi wa Majukwaa ya Wajasiriamli Wanawake Kisiwani Pemba kuhakikisha wanavishajihisha Vikundi Vya Ujasiriamali kujiunga na Majukwaa hayo ili viweze kuwezeshwa kwa kupatiwa mikopo ya kujiendeleza kiuchumi.
Mkurugenzi huyo ametoa kauli hiyo wakati akizungumza na Wenyeviti wa Majukwaa wa wilaya Nne za Pemba katika hafla ya ufunguzi wa Mafunzo ya kuwajengea uwezo wajasiria mali hao.
Alisema Vikundi vitakapo jiunga na majukwaa hayo itakuwa rahisi kupatiwa mikopo ya kujiendeleza katika harakati zao .
Alisema Serikali imeaanzisha majukwaa ya Wajasiriamali wanawake kwa ajili ya kuwaunganisha Pamoja na kuwa na sauti moja ili waweze kujadili shida walizonazo .
Alisema hatua hiyo itakuwa rahisi kuweza kuwafikia kwa wepesi katika kuwasidia kwa kuwapatia mitaji ya kujiendeleza kiuchumi, ili waondokane na utegemezi na unyanyasi wanaoupata katika jamii au kwenye ndoa zao.
Aidha alisema Mafunzo hayo yanalenga kuwajengea uwezo juu ya namna bora ya kuendendesha biashara zao baada ya kupatiwa mikopo wajasiriamali hao.
Alieleza kuwa baadhi ya wajasiriamali hawana elimu ya kutosha katika kuendeleza biashara zao na ndio maana wakatoa mafunzo hayo waweze kujiendesha baada ya kupatiwa ruzuku.
Hata hivyo aliwatahadharisha akina mama hao wakati watakapo patiwa mikopo wahakikishe wanazitumia kwa misingi iliyokusudiwa na sio kuwachia waume zao kuongeza wake.
Kwa upande wao washiriki wamafunzo hayo walisema watayatumia vyema huku wakiahidi kuongeza Vikundi kwenye jukwaa hilo ili viweze kunufaika na ruzuku inayoweza kutokea.
Raya Mohamed Khamis ni miongoni mwa washiriki wa mafunzo hayo alisema mafunzo hayo yamewafumbua macho katika namna ya kujiendeleza kiuchumi na kuahidi kuyatumia ipasavyo.
Mafunzo hayo yamewashirikisha wenyeViti wa Majukwaa ya Wajasiriamali wanawake kutoka Wilaya Nne za Pemba.

Comments
Post a Comment