HIVI NDIVYO UTELEKEZWAJI WA WATOTO UNAVYOATHIRI MALEZI, MAKUZI YAO

 


               NA FATMA HAMAD, PEMBA

UTELEKEZAJI ni ile hali ya wazazi kukwepa majukumu yao ya kutoa matunzo kwa familia zao.

Wengi wa wananchi wanadai kwamba, sababu kubwa inayopelekea utelekezaji ni baadhi ya akinababa wanapoamua kuoa mke zaidi ya mmoja, maranyi huwa hawatimizi wajibu wao.

Ingawa wapo wengine, hudai kukumbwa na sababu, ya kutafuta maisha kutoka sehemu moja kwenda nyingine, mfano wa wavuvi au wafanyabiashara.

Hayo yakifanyika, mafundisho ya dini yanafundisha kuwa, mzazi wa kiume ndio mwenye jukumu kubwa la kutoa matunzo kwa familia yake.

Lakini ulimwengu wetu wa leo, kumeibuka wimbi kubwa la baadhi ya wanaume kukwepa majukumu  yao na kuwabebesha mzigo wa malezi wanawake peke yao.

Hali hiyo ya wanaume kutokushughulikia familia zao, inasababisha watoto kuishi kwa simanzi na huzuni, kana kwamba wamefiwa na wazazi wao na kukosa familia ya kuwatunza.

Kiongozi wa Kanisa Katoliki lililopo Mkungu Malofa Chakechake, Robert Miguwa Ndalami, anasema dini imeelekeza kwamba, wanaume ndio wanaotakiwa kutoa huduma stahiki kwa familia zao.

“Baba ndio kichwa cha familia, hivyo yeye ndie anaetakiwa kuhudumia na sio kumuachia mama aleye peke yake,’’nanukuu.

Sheikh Said Ahmed Mohamed anasema, kisheria mwanamme ndie mwenye jukumu la kutoa matunzo kwa familia yake, na sio vyenginevyo.

Anasema ijapokua wanandoa wameamua kuachana au kutengana, bali ni jukumu la mwanamme kuhakikisha anawahudumia watoto, na sio kuwatia  adabu kwa sababu ya ugomvi wao.

‘’Hatakama mtaamua kuachana ama kutengana kila mmoja kuishi sehemu yake, bado baba jukumu lake ni kuwahudumia watoto, msiwaingize kwenye ugomvi wenu, wao hawahusiki,’’anasema.

"Inatosha mtu katika dhambi kuwatupa wale ambao anawajibika yeye kuwapatia matumizi"

WATOTO WANATHIRIKA VIPI WANAPOTELEKEZWA

Mwanafunzi wa darasa la tatu skuli ya Msingi Micheweni anasema, anahamu ya kusoma na kufika hadi elimu ya juu, ingawa anashindwa, kwani hana mtu wa kumuhudumia kupata vifaaa vya masomo.

Anasema kitendo cha kukosa huduma kutoka kwa wazazi wake wawili, kimemuathiri, kwani anashindwa kupata huduma stahiki, ambazo anaamini zingekuwa sababu ya kufika mbali.

Kumbe babayoa amewatelekeza, ameoa mke mwingine, hawaulizi kwa chakula wala kwa matibabu, hivyo anashindwa kusoma kwa bidi.

Mtoto mwengine ambae ameshafikia umri wa kuanza masomo ya mandalizi, anasema hajapelekwa kwani, mama yake hana uwezo wa kumtafutia vifaa kwa ajili ya kusomea.

‘’Nimekaazangu tu nyumbani sijapelekwa masomoni, nasubiri mama akipata uwezo anipeleke na mimi ili nisome,’’anasema.

Bilali Mohamed Rashid (16) anaesoma darasa la kumi, anasema ndoto zake ni  kua waziri wa Fedha, hapo baadae.

Ingawa, kitendo cha kukosa huduma kutoka kwa baba yake kinamuathiri, kwani anashindwa kupata huduma anazotakiwa.

‘’Tunakwenda skuli hatuna viatu mvua kama hizi, hatuli chochote, na tukirudi tunakuta hamna kitu, kwa kweli hilo linaniathiri na kuvuruga ndoto zangu,’’anasema.

WAZAZI NA JAMII WANALIPI

Bikombo Makame Shaame wa Chamboni Michewni ambae ana watoto watano, anasema huduma zote anajitegemea mwenyewe, licha kama bado yupo kwenye ndoa.

‘’Huu ni mwezi wa sita, hajawaletea watoto chochote, amenifanya nimekua kama ombomba, nikimpigia simu hanipi jawabu nzuri maana hivi karibuni aliongeza mke,’’anaeleza.

Anakiri kuwa, watoto wanathirika kwani, wanaondoka asubuhi wanakwenda masomoni hawali chochote na wakirudi ndio vivyo hivyo.

Bikombo Khamis mkaazi wa Mjini wingwi anasema, mume wake huondoka kwenda uvuvini Dar -es Saalam na kurudi kipindi cha mwezi wa ramadhani pekee.

‘’Ananiachia watoto wanane, haniulizi kwa chochote, nivunje kokoto ndio nipate fedha kwa ajili ya huduma za ndani, kinyume chake ni kulala na njaa,’’anasema.

Mwengine ni Rehema Salum Issa mkaazi wa  Madenjani wilaya ya Wete Pemba, anasema mume wake, amemuacha na watoto saba, na kumuachia mzigo wa malezi.

Salma Ali kutoka Machomane, anasema kwa hakika, mwanamke anapotelekezwa na watoto wanahangaika, na hususani akiwa hana shuguli za kujiingizia kipato.

‘’Mimi bado niko kwenye ndoa, tunashirikiana, lakini kuna siku tunakosa kuwatimizia watoto wetu mahitaji ya lazima, kama sare za skuli, inatubidi tuyazungumze,’’anaeleza.

Mohamed Rashid ni mstaafu wa JWTZ, ni miongoni mwa mzazi anayedaiwa na mwenzake wake kuitelekeza familia yake, ingawa anasema hali ngumu ya maisha ndio sababu.

‘’Ni kweli mimi mstaafu, ingawa ninachokipata, hakitoshelezi kukigawa nyumba mbili, nilishamtaka watoto anikabidhi, ingawa amegoma,’’anasema.

Said Kombo Kassim ni mkaazi wa Chakechake anasema kuoa wake zaidi ya mmoja, haisababishi mtu atelekeze familia yake, bali ni tabia mbaya walio nayo baadhi ya wanaume.

 ‘’Mimi nina wake wawili miaka 10 sasa, ila sijawahi hata siku moja  kunyima  familia  zangu huduma, na nikikosa tunakaa chini kuyazungumza,’’anasema.

 WANAHARAKATI

Amina Ahmed Mohamed ni mwanaharakati kutoka Chama cha Wandishi wa Habari Wanawake Tanzania TAMWA Zanzibar Ofisi ya Pemba, anasema ipo haja kwa viongozi wa dini kushirikiana na wanaharakati, kutoa elimu kwa wanaume.

Mratibu wa wanawake na watoto shehia ya Chamboni Micheweni Bizume Omar Faki, anasema watoto wengi wanaotelekezwa na wazazi wao, ndoto zao za kusoma huishia njiani.

‘’Wengi hujingiza kwenye uvuvi, uparaji samaki na kuuza biashara, ili kujipatia mahitaji yao na nyumbani kwao,’’anaeleza.

Dokta Rahila Salum Omar ambae ni msimamizi wa vituo vya kutoa huduma kwa watu wenye ‘VVU’ anasema, watoto wanapotelekezwa, huathirika kiakili na hukosa uwezo wa kufuatilia, haki zao ikiwemo elimu.

SERIKALI

Mkuu wa wilaya ya Micheweni Khatib Juma Mjaja, anasema katika wilaya yake, bado suala la utelekezwaji wanawake na watoto, ninaendelea kuota mzizi siku hadi siku.

Anasema, jambo hilo linasababisha kundi la watoto, kushindwa kutimiza malengo yao waliojiwekea, ikiwemo haki yao ya elimu.

‘’Kwa hakika, wilaya yangu bado hali si nzuri, watoto wanateseka na suala hilo la utelekezwaji, kwa kule baadhi ya wanaume kuacha majukumu yao,’’anasema.

Juhudi wanazozichukua ni kutoa elimu kwa jamii  ili wawe na subra katika ndoa zao, sambamba na kuwataka wanaume kuoa wake ambao watakua na uwezo wa kuwahudumia.

Afisa Ustawi wa jamii wilaya ya Michewebi Bizume Haji Zume, anasema suala la utelekezaji wa watoto bado ni kilio katika wilaya yake.

‘’Baba wengi huondoka na kuwaaga wake zao wanakwenda kutafuta maisha, lakini mwisho wa siku hawarudi tena, na kuwaachia mzigo wa huduma,’’anasema.


WANASHERIA

Aliekua Hakimu wa Mhkama maalumu ya kupambana na udhalilishaji Wete, Mumin Ali Juma anasema utelekezwaji unachangia kwa watoto kufanyiwa vitendo vya udhalilishaji, ikiwemo ubakaji na ulawiti.

‘’Unamuacha mwanamke na watoto watano ama saba, humpi huduma yoyote, umetegemea nini afanye,’’aliuliza.

Anasema maranyingi kesi zinazofikishwa Mahkamani za waliofanyiwa udhalilishaji ni watoto ambao wamekosa malezi ya pamoja kati ya baba na mama.

Mwendesha Mashtaka wa serikali kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Juma Mussa Omar anasema, sheria zote zinapinga utelekezaji watoto kutokana na msingi kwamba, bado wanategemea malezi na huduma.

Anasema matunzo ya watoto au matendo mabaya dhidi ya watoto yanaongozwa na sheria za kimataifa, za kikanda na sheria za nchi.

 Akatoa mfano kama Sheria ya mtoto Zanzibar, namba 6 ya mwaka 2011, Kifungu cha 9 (1) kinaelekeza haki ya mtoto kuishi na wazazi wake, walezi au familia ili akue kwa upendo na mazingira salama.

 Kifungu cha 71, kinaelekeza kumtoza faini mzazi  atakaeshindwa kutoa matunzo kwa mtoto,  ikiwa amri hiyo ya matunzo imetolewa chini ya kifungu cha 69 cha sheria hiyo.

Ripoti ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee, na Watoto ya mwaka 2024/2025 inaarifu kuwa, kulipokelewa  malalamiko 691 Unguja 313 na Pemba 378, yanayohusu ukiukwaji wa haki za watoto, mivutano ya malezi.

 Ambapo kwa upande wa Pemba kuanzia mwaka 2022 hadi 2024 malalamiko 1013 ya utelekezwaji wa watoto yalirpotiwa katika Idara ya Ustawi wa Jamii.

Wapo watoto waliotelekezwa ni 2183, wanaume ni 1096 na wanawake ni 1087.

Kwengeneko, ripoti ya uchunguzi uliofanywa hivi karibuni na shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia Watoto ulimwenguni (UNICEF), takwimu zinaonyesha kwamba idadi kubwa ya watoto wanaishi katika mazingira magumu.

Inasisitiza kwamba takriban watoto milioni 160 ulimwenguni kote, wanakabiliwa na hali ya kutengwa au kutelekezwa.

Ambapo kwa idadi hiyo, sawa na wastani wa watoto 13, 333 kwa mwezi, sawa na watoto 111 kwa siku hutelekezwa duniani kote, kutokana na sababu mbali mbali ikiwemo ya wazazi kuacha familia moja na kutafuta nyengine.

MIKATABA

Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 kifungu cha 12 (1) kinaeleza, watu wote ni sawa mbele ya sheria, na wanayo haki, bila ya ubaguzi wowote, kulindwa na kupata haki sawa.

Mkataba wa Kimataifa wa haki za Watoto duniani wa mwaka 1989, ulioanza kutumika mwaka mmoja baadae, kifugu cha 9, kinasisitiza nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa, kuhakikisha watoto hawatelekezwi.

 UNICEF ikabainisha kuwa, wasitenganishwe na  wazazi wao, isipokuwa kwa amri ya mahakama au taasisi, inayohusikia maslahi bora ya mtoto.

Mkataba wa haki na Ustawi wa Watoto wa Afrika wa mwaka 1999, kifungu cha 19, kikalazimisha kuwa, kila mtoto anayohaki ya kufurahia na kunufaika na malezi bora kama msingi mkuu wa kupata haki

Mkataba huu unasisitiza nchi wanachama kuhakikisha zinaondoa mila na tamaduni potofu zinazoathiri ustawi, utu, makuzi na maendeleo ya mtoto Afrika.

 



 

 

 

 

 

 

 

 

 


Comments

Popular posts from this blog

KERO YA MAJI, TATIZO KWA WANAKIJIJI CHA GOMBEUME

DNA YA THIBITISHA, MTUHUMIWA NDIE BABA MZAZA WA MTOTO