WANASIASA WANAOGOPA KUTUMIA UHURU WA KUJIELEZA

 


                     NA FATMA HAMAD-PEMBA

Kila Raia ana haki ya kutoa maoni na kuwa na uhuru wa kujieleza

Kifungu cha 18 (1) cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 kinaeleza kuwa ‘’Bila ya kuathiri Sheria za nchi, kila mtu yuko huru kuwa na maoni na mawasiliano yake bila kuingiliwa kati.”

Na hata Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 ibara ya 42 inaeleza kwamba, kila mtu anastahili kuwa huru bila kuathiri sheria za nchi.

Kwa Zanzibar viongozi wa vyama vya siasa wanasema, wamekua wakikosa kutumia uhuru wao wa kujieleza, licha ya kuwa ni haki yao kikatiba.

Hivyo basi, makala hii imezungumza na wadau mbali mbali pamoja na wanasiasa  ili kufahamu ni kwa nini wanasiasa wanaogopa kutumia uhuru wao wa kujieleza.

WANASIASA

Maryam Nassor Juma ambae ni Katibu wa Chama cha Chauma mkaazi wa Vitongoji Chake Chake Mkoa wa Kusini Pemba anasema, wanaogopa kutumia uhuru wao wa kujieleza kutokana na mifumo pamoja na sheria zilizopo za habari  pamoja na za uchaguzi zinaminya uhuru wao.

Anasema, wamekua wakikosa ushirikiano na hata kwa waandishi wa habari kutoa kero zao, kwani hata kwani hata nahao wandishi wenyewe wanaogopa  kwa sababu  Sheria zilizopo za Habari  zinawanyima uhuru.

‘’Hata ukiangalia kwenye mikutano ya kampeni, waandishi wa habari wengi wanaripoti habari za chama tawala tu, lakini kwa nini hawaripoti habari za kwenye vyama vya upinzani, hivyo ni wazi kwamba uhuru haupo,’’ anaeleza.

Anasema katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020, walikatwa matokeo yao na walipojaribu kuwatafuta waandishi wa habari ili wawaelezee malamiko yao, walikosa ushirikiano, hivyo inaonesha wazi kwamba na wao wanaogopa.

Anaeleza, kwa mujibu wa kifungu cha 127 cha Sheria ya kufuta Sheria ya Uchaguzi Namba 11 ya mwaka 1984 na kutunga Sheria ya Uchaguzi ya mwaka 2017 na mambo mengine yanayohusiana nayo, kinanyima uhuru wao.

Kwa sababu kifungu hicho kinaeleza kwamba ‘’ni marufuku chama cha siasa, kutangaza matokeo ya uchaguzi kwa njia yoyote ya mawasiliano kabla ya matokeo ya uchaguzi kutangazwa rasmi na Tume ya uchaguzi.

Au kuitaka Tume itangaze matokeo ya uchaguzi kabla ya muda uliowekwa kumalizika, atakua ametenda kosa na akitiwa hatiani adhabu yake ni chini ya shilingi milioni mia moja’’.

Mohamed Haji Kombo ni Katibu wa Chama cha Wananchi CUF

 Wilaya ya Chake Chake, Mkoa wa Kusini Pemba anasema, uhuru

 wa kujieleza kwa vyama vya siasa upo, isipokua utekelezaji tu, haupo.

‘’Hatukamatwi, hatugombwi, ila hayo tunayoyasema hayapokelewi vizuri na wala hayatekelezwi, kwa hiyo wakati mwingine tunakaa kimya tu,’’ anaeleza.

Katibu wa Chama cha ACT Wazalendo Mkoa wa Chake Chake kichama Saleh Nassor Juma anasema, wanaogopa kutumia uhuru wao wa kujieleza, kwa sasbabu  haupo.

Anasema, licha ya kuwa uhuru wa kujieleza kikatiba umetajwa kwamba, ni haki ya kila Mzanzibari, ingawa bado kwenye vyama vya siasa hakuna uhuru wa kuzungumza, kwa sababu hata unapojaribu kutafuta vyombo vya  habari, ili kuelezea kero zako basi hazitolewi hewani, hususani kwa upande wa vyama vya upinzani.

‘’Kwakweli sisi vyama vya siasa hususani vya upinzani hatuna uhuru wa kujieleza, kwani tunapokua na malalamiko yetu wandishi wa habari hawatoi kwenye vyombo vyao, na atakae jaribu kuzitoa anaweza akaingia kwenye matatizo, ama chombo chake kinaweza kufungiwa,’’anasema.

Anaendelea kufafanua, siku zote unapojaribu kuzungumza kitu kinachukuliwa vibaya, unajikuta unaingia mashakani na kuambiwa ni mchochezi na unaikosoa Serikali.

Kwa mfano  mwaka 2001  anasema aliwekwa ndani kwa sababu aliambiwa ameshawishi wafuasi wa chama chake  kufanya mandamano ya kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu wa  mwaka 2000.

‘’Nilishawekwa ndani mara kadhaa, ikiwemo  mwaka 2001 kwa sababu tu, tulifanya mandamano ya kupinga matokeo ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2000, tukaonekana kama ni wachochezi na tumeikosoa Serikali,’’anasema.

Anaendelea kusema kuwa, alifukuzwa kazi, kwani katika uchaguzi wa mwaka 1990 walilalamika na kudai kwamba wanahitaji kuwapo uchaguzi utakaoshirikisha vyama vingi na sio wa chama kimoja.

‘’Mimi na wenzangu kadhaa tulifukuzwa kazi kwa sababu tu tulidai kuwapo na mfumo wa vyama vingi,’’ anaeleza.

Khamis Omar Juma Katibu wa Chama cha Mapinduzi CCM Wilaya ya Mkoani, Mkoa wa Kusini Pemba anasema uhuru wa kujieleza kwa vyama vya siasa upo.

Anasema, viongozi wote wa vyama vya siasa wamekua wakizungumza kero zao na kutoa malalamiko yao bila ya woga wowote.

 ‘’Kwa kweli uhuru tunao na tunazunguza kila ambalo tunaona linatukwaza, na wala hatupati tatizo lolote,’’ anasema.

WANANCHI

Batuli Mussa Sharif mkaazi wa Micheweni anasema, vyama vya siasa bado havina uhuru wa kutosha wa kutoa maoni yao, kwa sababu wanapozungumza jambo ijapokua lina maslahi kwa jamii wanaonekana wanataka kuleta vurugu, hususani vyama vya upinzani.

Anasema siku zote  wamekua wakishuhudia matukio kadhaa ambayo huwatokea viongozi wa vyama vya siasa, wakati wanapozungumzia kero zao.

‘’Kwa kweli wanasiasa uhuru wao wa kujieleza ni mdogo, hivyo ipo haja ya kuwekwa mifumo rafiki, ili kuona kila kiongozi wa chama chochote ana uhuru wa kutumia haki yake ya kikatiba ya kuwa na uhuru wa kujieleza bila kikwazo,’’ anaeleza.

Mohamed Khalfan mwananchi kutoka Mkoani Pemba anasema, vyama vya siasa vinaogopa kutumia uhuru wao wa kujieleza kwani bado huo uhuru wenyewe wa kujieleza haupo, yawezekana upo katika maandishi, lakini kihalisia haupo.

‘’Kwa kweli vyama vya siasa bado havipati kutumia uhuru wao wa kujieleza, ni vyema kungewekwa mifumo ambayo haingilii uhuru wao,’’ anaeleza.

MWANASHERIA

Khalfan Amour Mohamed Mwanasheria wa kujitegemea kutoka kisiwani Pemba anasema, wanachama wa vyama vya siasa wanaogopa kutumia uhuru wao wa kujieleza kwa sababu mifumo iliyopo bado inawakwaza.

Anasema, ndio maana wanawake wengi walio na elimu zao hawagombei nafasi za uongozi, kwa sababu wanaogopa, hali ambayo wanapokuwa wanasiasa hukosa uhuru na wakati mwingine wanaweza kukosa fursa za maendeleo.

‘’Vyama vya siasa vinaogopa kutumia uhuru wao wa kujieleza, kwani ukijaribu kuzungumza kitu chenye maslahi ya jamii na ikiwa kimewagusa watu wakubwa utakuta umeingia kwenye matatizo,’’ anasema.

Anasema, ipo haja kubadilishwa kwa mifumo iliyopo pamoja na Sheria mbali mbali zikiwamo Sheria za Habari, ili kuona kila mmoja anapata uhuru wake wa kujieleza kama Katiba ilivyoeleza.

WANAHARAKATI

Salim Said Salim ambae ni Mjumbe kutoka Tasisi ya  Watalamu wa Masuala ya Habari Zanziba (ZAMECO) anasema, bado vyama vya siasa havijakua na uhuru wa kueleza mambo yao hususan kwa upande wa vyama vya upinzani.

Anasema, uhuru wa kujieleza kwa vyama vya siasa haupo kwani  inaweza ikatokezea vyama vyengine vikaruhusiwa kufanya maandamano ya amani, ingawa baadhi ya vyama vikazuiliwa, na vyombo vya habari vikashindwa kuripoti kwa kuhofia nawao kuingia matatizoni.

‘’Bado mifumo pamoja na Sheria zilizopo za Habari  hazijawapa uhuru baadhi ya vyama vya siasa, bali zinawanyima,’’ anasema

Anasema kama vyombo vya habari vinaaminika  kwanini wandishi wa habari wasiruhusiwe kuripoti matokeo ya uchaguzi ambayo tayari yameshapachikwa kiambazani hadi mpaka isubiriwe tume itangaze.

Anasema, ingekua Sheria zilizopo ikiwamo ya Usajili wa Wakala wa Habari, Magazeti na Vitabu nambari 5 ya mwaka 1988 iliyofanyiwa marekebisho na Sheria Nambari 8 ya mwaka 1997 ,  wangeweza kuvitumia vyombo mbali mbali vya habari kuzungumzia kero zao.

Anasema ingelikuwa Sheria hizo ni rafiki kwao wangeweza kuondokana na malalamiko, kwani wangetumia  vyombo vya habari kuzungumza matatizo yao yanayowakwaza, na yakaweze kusikika na mamlaka husika.

Anasema, ni vyema Serikali ikabadilisha baadhi ya vifungu vilivyomo katika Sheria hiyo ambayo vinanyima upatikanaji wa uhuru wa wanahabari pamoja na vyama vyote vya siasa, na kuweka vyengine ambavyo vitatoa uhuru kwa  wote,

Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania Zanzibar (TAMWA), imekua mstari wa mbele kupigia kelele sheria zenye mapungufu hasa zinazogusa tasnia ya Habari ziboreshwe, ili kuhakikisha kila raia anapata haki yake ya kuwa na uhuru wa kujieleza.

‘’Tutahakikisha tunapaza sauti zetu juu ya Sheria hizi za Habari na ambazo zinagusa tasnia hiyo, ili tuhakikishe tunapata Sheria mpya na rafiki, ambazo zitawafanya wandishi wa habari waweze kutekeleza majukumu yao wakiwa na amani na bila ya hofu yoyote,’’ Mkurugenzi wa TAMWA Zanzibar  Mzuri Issa Ali anaeleza.


NINI KIFANYIKE

Ipo haja ya kurekebishwa kwa baadhi ya sheria kama vile Sheria za Uchaguzi, Sheria za Habari pamoja na mifumo iliyopo, ili kuona kila mtu anapata haki yake ya msingi ya kujieleza kama ilivyoeleza Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984.

                                 


Comments

Popular posts from this blog

KERO YA MAJI, TATIZO KWA WANAKIJIJI CHA GOMBEUME

HIVI NDIVYO UTELEKEZWAJI WA WATOTO UNAVYOATHIRI MALEZI, MAKUZI YAO

DNA YA THIBITISHA, MTUHUMIWA NDIE BABA MZAZA WA MTOTO