WADAU WALIA NA SHERIA ZINAZOKWAZA HAKI YA KUPATA HABARI

 



                       NA FATMA HAMAD - PEMBA

Baada ya kilio cha muda mrefu waandishi wa habari visiwani Zanzibar  wana matumaini makubwa juu ya kupata sheria mpya za habari ambazo hazina vikwazo kwao na zinazoendana na mazingira ya sasa.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi katika hotuba zake kadhaa amekua akizungumzia changamoto ambazo zimekua zikiikabili tasnia ya habari na kuahidi kuzitatua changamoto hizo, ili kuona vyombo vya habari vinatekeleza majukumu yake vikiwa huru.

‘’Tunatambua changamoto zinazovikabili vyombo vya habari pamoja na waandishi wa habari, hivyo Serikali itafanya kila jitihada kuviwezesha, ili kuona wandishi wa habari wanatekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi,’’alisema Rais Mwinyi

Dokta Mwinyi katika miaka minne ya uongozi wake amekua ni kiongozi  wa  mwanzo na wa mfano katika nchi hii kukutana mara kwa mara na waandishi wa habari Visiwani Zanzibar, amebeba matumaini makubwa ya wadau wa habari pamoja na wananchi wenye kuheshimu uhuru wa habari na haki ya kupata habari.

Bila shaka kufanya hivyo kumempa nafasi kubwa ya kusikiliza moja kwa moja vikwazo vinavyowakumba wandishi wa habari pamoja na vyombo vya habari hapa Zanzibar katika utekelezaji wa majukumu yao.

Kutokana na hayo waandishi wa habari ambao ndio watafutaji na wasambazaji habari wamekua na kiu na shauku kubwa ya kurekebishwa vifungu  vilivyomo  katika Sheria za Habari ambavyo vitawafanya wawe huru, ili waweze kutekeleza majukumu yao bila woga wala hofu yoyote, kwani ni muda wamekua wakipaza sauti zao ili kuona vifungu hivyo vinaboreshwa.

WAANDISHI WA HABARI

Mwandishi wa habari mkongwe Mohamed Khalfan kutoka kisiwani Pemba anasema vyombo vya habari vina wajibu wa kutoa taarifa mbalimbali kwa lengo la kuuhabarisha umma juu ya mambo yanayohusu nchi kiuchumi, kijamii na kisiasa.

Anasema ili waandishi waweze kufanya kazi zao bila ya hofu na woga, ipo haja ya kuwapo kwa sheria zinazotoa uhuru na fursa pana kwa wanahabari katika kutafuta, kuchakata na kusambaza habari bila ya kuwapo vikwazo vinavyotokana na sheria nyingine ambazo zinapingana na sheria mama ambayo ni Katiba ya nchi.

‘’Waandishi wana hofu ya kutumia uhuru wao wa kujieleza, hivyo ni vyema kuwapo na Sheria ambazo ni rafiki kwao na ambazo zinatoa uhuru, ili waweze kutekeleza majukumu yao bila hofu yoyote,’’anasema.

Mwandishi wa habari na Mhariri wa Mtandao wa Pemba Today Haji Nassor Mohamed anasema waandishi wa habari wamekua na hofu ya kutumia uhuru wao wa kujieleza kwani katika Sheria zilizopo bado kuna vifungu kadhaa vimekua ni kikwazo, na ni kandamizi ambavyo vinanyima uhuru wa habari na uhuru wa kujieleza.

‘’Baadhi ya sheria zinazosimamia sekta ya habari na nyingine ambazo zinaigusa sekta hiyo zinazuia mtiririko mzuri wa utafutaji na usambazaji wa habari, ambapo ni kinyume na kifungu cha 18 cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, ambacho  kinasema mwananchi kutafuta na kupata habari bila mipaka,’’ anasema.

Anasema kifungu namba18 (1) na (2) vinaeleza kuwa kila mwananchi amepewa uhuru wa kutafuta, kupokea na kusambaza habari bila ya vikwazo wala mipaka, ingawa bado zipo Sheria zinazoweka mipaka, jambo ambalo huwa ni kikwazo katika mchakato wa upashanaji habari.

Anasema miongoni mwa vifungu ambavyo vinanyima uhuru wa habari ni kifungu cha 123 cha sheria  ya kufuta  Sheria ya Uchaguzi  namba 11 ya mwaka 1984 na kutunga sheria ya mwaka 2017, ambacho  kinanyima fursa ya waadhishi wa habari kufuatilia harakati za uchaguzi hasa wakati wa kupiga na kuhesabu kura.

Anaendelea kusema katika sheria hiyo kuna vifungu ambavyo vimempa mamlaka Afisa Dhamana wa Uchaguzi kumnyima  kitambulisho mwandishi wa habari, jambo ambalo linaweza kupelekea Afisa huyo kutumia mamlaka yake vibaya kwa kuwakandamiza wanahabari hivyo kukwaza haki ya wanachi kupata habari za kweli kuhusu uchaguzi. 

‘’Vifungu hivyo vinatuonesha  kwamba hakuna  umuhimu  wowote  wa  kuwepo na waandishi wa habari hapa nchini ,’’

Pia anasema katika sheria hiyo kuna vifungu ambavyo vimetoa adhabu kubwa ikiwemo ya kifungo na faini au vyote viwili kwa pamoja kwa  mwandishi atakayekutikana na makosa yaliyoainishwa na sheria hiyo.

‘’Siyo vizuri kwa ulimwengu wetu huu ambao unahimiza haki, usawa na uwajibikaji, kuwapo vizingiti (vikwazo) ambavyo katika baadhi ya nchi  kama vile Kenya na Nigeria waandishi wa habari (vyombo vya habari) hutoa matokeo ya uchaguzi baada ya kupata  matokeo yaliyotangazwa na mamlaka husika kwenye majimbo,’’ anasema.


Naye mwandishi wa habari mwandamizi Mchanga Haroub Shehe anasema kutokana na kuwapo kwa vifungu hivyo ambavyo ni kandamizi vinasababisha waandishi wa habari kuwa na mazingira magumu ya kutekeleza majukumu yao.

Anasema ipo haja kwa waandishi wa habari kuhakikisha wanakua na fursa pamoja na elimu ya jinsi ya kuripoti masuala ya uchaguzi.

‘’Kama vifungu hivyo havijaangaliwa na kurekebishwa bado itaendelea kuwaweka katika wakati mgumu waandishi wa habari hasa katika kipindi cha uchaguzi,’ ’anamalizia Bi Mchanga.


WANANCHI

Juma Kombo Hamad mkaazi wa Micheweni anasema endapo waandishi wa habari hawatokua huru hakutoathiri wao peke yao, bali hata jamii itaathirika kwani itakosa kupata taarifa za matukio ambayo yanatokezea nchini.

‘’Waandishi wa habari ni watu muhimu katika nchi, hivyo kama watakua na hofu na hawatokua na uhuru wa kutekeleza majukumu yao, sio rahisi kupatikana kwa maendeleo,’’anasema.

Asha Omar Said mkaazi wa Machomane Chakechake Pemba anasema kutokana na kuwapo kwa Sheria za Habari ambazo zinawanyima waandishi wa habari uhuru wao wa kujieleza, ipo haja mamlaka zinazoshughulikia masuala ya kisheria kuhakikisha zinafanyiwa marekebisho ili kuhakikisha waandishi wa habari wanatekeleza majukumu yao wakiwa huru na bila ya khofu yoyote.

WANAHARAKATI

Salim Said Salim mjumbe kutoka Tasisi ya Zameco Zanzibar anasema kuwapo kwa uhuru wa habari ni jambo muhimu kwani inasaidia kwa kiasi kikubwa ukuaji wa maendeleo nchini.

Anasema endapo kutakuwa na sheria ambazo zinabana uhuru wa habari husababisha  kosekana  kwa  maendeleo ya wananchi.

‘’Kwanini waandishi wa habari wasiruhusiwe kupiga picha au kutangaza matokeo ya uchaguzi ambayo tayari yameshapachikwa kiambazani,’’ anasema.

Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari kisiwani Pemba Bakar Mussa Juma  anasema katika kipindi cha Uchaguzi waandishi wa habari walio wengi hukutana na mazingira magumu, licha ya kutekeleza majukumu yao kwa misingi ya kisheria.

Anasema ipo haja  ya mamlaka husika kuona umuhimu wa kuvifanyia marekebisho vifungu vinavyokwaza uhuru wa habari na kusababisha waandishi wa habari kushindwa kutekeleza majukumu yao ipasavyo, na kuendelea kuwaweka katika mazingira magumu kipindi cha chaguzi.

‘’Siyo jambo zuri mwandishi ashindwe kupata  taarifa  za matokeo mpaka yatangazwe na Tume ya Uchaguzi, hii ni kuidumaza tasnia ya habari,’’ anaeleza.

Zaina Abdala Mzee Afisa Programu kutoka Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA Zanzibar) anasema endapo vifungu vilivyotajwa katika Sheria hiyo ya Uchaguzi havitofanyiwa  marekebisho, kunaweza kukaja kukapelekea baadhi ya waandishi kuingia kwenye matatizo na wengine kushindwa kufanya kazi kabisa katika kipindi  cha Uchaguzi Mkuu.

‘’Ni vyema kukachukuliwa hatua za makusudi kuondoshwa vifungu hivyo ambavyo vinaonekana vinabana uhuru wa waandishi na kuwanyima wananchi haki yao ya kupata habari,’’ anashauri.

Zahran Mohamed Yussuf ni mwanasheria wa kujitegemea kutoka Chakechake  Pemba  anasema  waandishi  wa  habari ndiyo wenye  jukumu la kuuhabarisha umma juu ya mambo yanayotokea katika nchi yao, hivyo kama kutakua na sheria zinazowabana kunaweza kukatokea athari kubwa kwao na hata kwa jamii.

‘’Ili kuona waandishi wanatekeleza majukumu yao bila vikwazo na jamii inahabarishwa juu ya mambo yanatokezea, ni muhimu kuwekwa sheria ambazo ni rafiki na ambazo hazina mashaka,’’ anafahamisha.

VIONGOZI WA SERIKALI

Akitoa ufafanuzi juu ya sheria hizo katika kikao cha maafisa habari kutoka Zanzibar pamoja na Tanzania bara kilichofanyika visiwani Zanzibar Aprili mwaka huu, Waziri wa Habari Vijana Utamaduni na Michezo Tabia Maulid Mwita anasema wanatarajia kupeleka muswada wa Sheria mpya ya Habari katika Baraza la Mapinduzi.



    

 

 


Comments

Popular posts from this blog

KERO YA MAJI, TATIZO KWA WANAKIJIJI CHA GOMBEUME

HIVI NDIVYO UTELEKEZWAJI WA WATOTO UNAVYOATHIRI MALEZI, MAKUZI YAO

DNA YA THIBITISHA, MTUHUMIWA NDIE BABA MZAZA WA MTOTO