SHERIA ZA HABARI ZANZIBAR BADO KIZUNGUMKUTI

 


NA FATMA HAMAD - PEMBA

Katika sheria ya usajili wa uwakala wa habari, magazeti na vitabu namba 5 ya mwaka 1988 iliyofanyiwa marekebisho na sheria no 8 ya mwaka 1997 yapo maneno kadhaa yaliyotumika ambayo yanaonekana kuwa na mapungufu na ambayo yanakwaza uhuru wa vyombo vya habari.

Matumizi  hayo ya maneno yaliyotumika katika sheria hiyo yanaweza kuathiri  uhuru wa habari pamoja na waandishi wa habari ikiwa hayatofanyiwa marekebisho.

Katika makala hii  tutaangalia  sheria  ya usajili wa uwakala wa habari, magazeti na vitabu namba 5 ya mwaka 1988  iliyofanyiwa marekebisho na sheria no 8 ya mwaka 1997 ina muda wa  miaka 36 sasa,  ambapo katika vifungu vyake inayo maneno ambayo sio rafiki kwa vyombo vya habari na waandishi wa habari.

Miongoni mwa maneno hayo yenye kuleta ukakasi yanapatikana katika kifungu cha 30 cha Sheria  ya usajili wa uwakala wa habari, magazeti na vitabu namba 5 ya mwaka 1988 kama ilivyofanyiwa marekebisho na sheria No. 8 ya mwaka 1997 kwa mfano neno “endapo waziri ataona kuwa ni kwa manufaa ya umma au kwa maslahi ya amani na utulivu anaweza kuamuru kufungiwa kwa gazeti.

Hivyo ni dhahiri kwamba Kifungu hicho kimempa mamlaka makubwa Waziri wa habari, na kinaweza kumfanya akatumia vibaya madaraka yake kwa kuwakandamiza  wengine kwa kutokana na chuki zake  tu binafsi.

‘’Inawezekana waziri akawa wanaugomvi tu na Muandishi wa habari au Muhariri, hapo inawezekana akapata mwanya na kutumia mamlaka yake  na kumfungia mwandishi au chombo cha habari’’

Katika kifungu cha 27[2] kuna sentensi isemayo: “hakimu yeyote anaweza kutoa hati na kumuidhinisha afisa yeyote wa cheo cha inspekta kwa msaada au bila msaada kuingia na kupekua kazi yoyote ya habari. Jambo hili wadau wa habari linawakosesha usingizi, kwani kinawanyan’ganya haki ya kutoa habari kama ilivyoainishwa kikatiba.  

Kutokana na hayo wandishi pamoja na wadau wa habari wakapaza sauti zao  kuipigia kelele sheria hiyo ili iweze kuangaliwa tena upya kwa lengo la kuondoshewa  baadhi ya maneno hayo ambayo imeonekana hayaendani na uhuru wa habari na demokrasia.

WAANDISHI WA HABARI

Said Abdulla kutoka  Radio Istikama anasema neno  endapo ni neno ambalo halina uhakika, na linaingilia uhuru wa habari kwani mtu aliepewa mamlaka anaweza kumfungia mwandishi wa habari kwa kutokana na utashi wake mwenyewe tu.

‘’ Neno akihisi au akidhani au endapo sio maneno mazuri, kwani anaweza kumfungia  mwandishi au chombo cha  habari  akiwa  na chuki zake tu binafsi, anasema Said.

Mohamed  Khalfan mwandishi  redio Nnur anasema neono endapo, akidhani yeyote sio maneno rafiki hayaendani na mazingira, kwani yanatoa mamlaka makubwa na yanaweza kumpelekea mwenye mamlaka  aliepewa kuyatumia vibaya mamlaka hayo.

‘’Haiwezekani mtu mmoja tu akihisi, akidhani,  endapo akishuku tu  chombo fulani sasa hivi kinaandika habari mbaya aingie na kupekua, au afungie chombo cha habari, hilo ni tatizo kubwa kwani yeye ni binadamu kama wengine ana mapungufu yake hebu hilo liangalieni tena,anashauri.

Bakia Khamis  Faki kutoka Zenji tv  anasema maneno hayo yanaleta migongano na hayaendani tena na mazingira ya kihabari, hivyo wakati umefika kwa wadau wa masuala ya kisheria kukaa chini na kuipitia tena upya Sheria hiyo ya usajili wa uwakala wa habari, magazeti na vitabu namba 5 ya mwaka 1988 iliyofanyiwa marekebisho na sheria no 8 ya mwaka 1997 ili kuondosha istilahi zinazoashiria vikwazo.


WAMILIKI WA VYOMBO VYA HABARI

Suleiman Said Ali mmiliki wa Jicho letu Oline tv  anasema maneno yaliotumika katika Sheria ya Usajili wa Uwakala  wa Habari  Vitabu na Magazeti namba 5 ya mwaka 1988  yana ukakasi, kwa mfano  kifungu cha 30 sentensi “endapo waziri ataona kuwa ni kwa manufaa ya umma au kwa maslahi ya amani na utulivu anaweza kuamuru kufungiwa kwa gazeti.”

Hata kifungu cha 27[2]  kinachosema “hakimu yeyote anaweza kutoa hati na kumuidhinisha afisa yeyote wa cheo cha inspekta kwa msaada au bila msaada kuingia na kupekua kazi yoyote ya habari,” kifungu hiki sio rafiki kwa vyombo vya habari na kinahitaji kufanyiwa marekebisho au kiondoshwe kabisa,  kwani  inaweza ikapelekea wahusika kutumia mamlaka yao kwa utashi wao wenyewe.

Mgeni Kombo Khamis mmiliki wa Blog ya Habariportal anasema maneno hayo yaliyotumika katika Sheria siyo rafiki hayaendani tena na wakati wa sasa,  na yanawafanya waandishi wa habari kufanya majukumu yao wakiwa hawako huru.

‘’Kwa kweli maneno yaliyotumika katika Sheria yetu hiyo ya habari yana ukakasi  si ya kidemokrasia, na hayawapi hamu wandishi kuandika habari zilizojificha na hata sisi kumiliki vyombo vya habari,’’anamalizia Mgeni.

WADAU WA HABARI

Mustapha Mohamed Moyo kutoka Tasaisi ya Moyo media anasema endapo kama kutakuwa na Sheria ambayo ina maneno yenye ukakasi yatawatia hofu baadhi ya watu ambao wanaotaka kuwekeza kwenye sekta ya habari.

‘’Kwa kweli ukisema mtu  endapo, yeyote, atakapojisikia, atakapodhani, sio maneno mazuri, na yanawatia hofu wawekezaji katika sekta ya habari hivy wanarudi nyuma wanahisi hizo Sheria zipo kwa ajili ya maslahi ya wenye mamlaka,’’anafahamisha.

Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa habari kisiwani Pemba (PPC) Bakar Mussa Juma anasema maneno  hayo yaliyotumika katika Sheria hiyo yanaathiri uhuru wa waandishi wa habari jambo linapolopelekea waandishi wa habari pamoja na jamii  kukosa haki yao ya kikatiba ya kupata habari.

TAASISI ZINAZOSIMAMIA WAANDISHI WA HABARI

Afisa program kutoka Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania TAMWA ZANZIBAR Zaina Abdala Mzee anasema  Sheria ya habari imeshakua kongwe haiendani tena na mazingira ya sasa, inahitaji kufanyiwa marekebisho.

‘’Tunatamani siku moja kuona nasisi Zanzibar tumepata Sheria mpya ya habari ambayo haina maneno yenye kuleta mkanganyiko kwa waandishi wa habari,’’anasema.

Anasema wamekua wakiwajengea uwezo waandishi wa habari waweze kuipigia debe Sheria hiyo,  ili hatimaye kuona imefanyiwa marekebisho anasema Zaina.


WANASHERIA

Zahran Mohamed Yussuf ni wakili wa kujitegemea kutoka Wilaya ya Chakechake anasema ipo haja ya kufanyiwa marekebisho kwa Sheria hiyo ya habari, kwani inayo maneno/istilahi  ambayo siyo  rafiki kwa vyombo vya habari.

 ‘’Tujue kwamba waandishi wa habari ndio wanaoifanya nchi kuwa na amani na maendeleo, hivyo hivyo kama sheria zitakuwa na vipengele vinavyowabana kutekeleza kazi zao kwa ufanisi tufahamu kwamba maendeleo hayo hayatafikiwa, kwani wao wenyewe watakua na hofu katika utekelezaji wa kazi zao,’’ anasema Zahran.




Comments

Popular posts from this blog

HIVI NDIVYO UTELEKEZWAJI WA WATOTO UNAVYOATHIRI MALEZI, MAKUZI YAO

‘’KATIBU MKUU ELIMU ‘’TOENI ELIMU YA MALEZI BORA’’

UROHO WA MALI KWA WANAUME UNAVYONYIMA WANAWAKE ARDHI