Gharama za Uchaguzi zinavyokatisha ndoto za wanawake wanaogombea.

 

Wasema hali isiporekebishwa majimbo yataendelea kuwa magumu kwao

                            Na Fatma Hama, Pemba

‘’NATAMANI kugombea tena uongozi katika uchaguzi ujao wa mwaka 2025, lakini kila nikifikiria gharama…nakata tamaa,’’

Hayo si maneno ya mtu mwengine bali ni ya mwanamama Tumu Mwalim Massoud mwenye miaka 40 mkaazi wa Wingwi Limani wilaya ya Micheweni Pemba, ambae aligombea uwakilishi Jimbo la Wingwi kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM) kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2020.

Mwanamama huyo kiu yake ni kuwa mwakilishi ili aweze kutetea haki za wananchi, ingawa anakumbuka gharama zilizomtoka katika uchaguzi wa mwaka 2020 na hatimae kushindwa katika kura.

Anasema, kwa hali hiyo ndoto nyingi za wanawake wenye nia ya kugombea zitakatika na majimbo yataendelea kuongozwa na wanaume watupu, ambao kuna baadhi ya mambo yanaowahusu hawawezi kuyatetea.

Ni mwaka wa 23 tangu Tumu aingie kwenye harakati za kisiasa, lakini anaanza kupoteza matumaini kutokana na gharama kubwa asizoweza kuzimudu kwenye mambo ya uchaguzi.

Tumu anasilimulia kuwa, hakua na mtu wa kumsaidia gharama isipokua ni yeye mwenyewe pamoja na familia yake ambayo iliyoikimchangia pesa kwa ajili ya kufanyia kampeni.

‘’Unataka ufanye mikutano kwenye jimbo lako, unahitaji upate usafiri, vipaza sauti, wasanii, wandishi wa habari na vyote hivyo vinahitaji gharama ila sasa utazitoa wapi,” anauliza Tumu.

Chama chake kilimsaidia pesa kidogo mwishoni mwa kampeni, jambo lilimfanya akope fedha kwa ajili ya kuendesha kampeni zake,” anasema.

Baada ya kumalizika kwa uchaguzi na kushindwa, alianza kuuza mali zake na za familia yake ili apate fedha ya kulipa madeni.

‘’Kwa sasa najifikiria kugombea tena kwa sababu nakumbuka maumivu ya kulipa madeni, ingawa natamani niingie tena kwa sababu ndoto yangu ya kuwa kiongozi haijakamilika,’’ anasema.

Anasema, wanawake wengi wamekuwa na ndoto ya kuwa viongozi ingawa mwisho hukata tamaa na kushindwa kufanikisha malengo yao kutokana na kukosa pesa za kuendeshea shughuli za uchaguzi.

Tumu ana elimu ya ngazi ya diploma ya masuala ya Kompyuta (IT) na ana watoto Saba (7) ambao wanamtegemea.

Sio Tumu pekee mwenye kilio hicho bali kuna wanawake wengi ambao wanakwama kutokana na kukosa fedha za kujigharamia kwenye kugombea…

Ambapo mwanamama Ziada Khalfan Saleh mwenye miaka 48 mkaazi wa Machomane Wilaya ya Chake Chake nae ni miongoni mwa wahanga.

Yeye aligombea ubunge Jimbo la Ziwani zaidi ya mara tatu kupitia Chama Cha Tanzania Labour Party (TLP) huku akishindwa kufanya mikutano kutokana na ukosefu wa fedha.

‘’Ninachokifanya mimi ni kupiga hodi nyumba baada ya nyumba na kuomba kura, kweli kwa hali hii nitalipataje Jimbo wakati nyumba siwezi kuzimaliza na sina uwezo wa kufanya mikutano ya kampeni,’’ anaeleza.

Anasema, ni wakati sasa Serikali kutoa ruzuku kwa vyama vyote na sio tu kwa vyama vikubwa, ili ziwawezeshe wanawake kwenye kampeni ambapo itakuwa ni sababu ya wao kufanikiwa kuwa viongozi.

Hata mwanamama Asha Ali Mohamed miaka 45 aliewahi kugombea Jimbo la Wawi Wilaya Chake Chake kwa zaidi ya mara tatu kupitia Chama cha United Democratic Paty (UDP) nae alikumbwa na kadhia hiyo ambapo anasema gharama za uchaguzi ni kikwazo kikubwa kinachowanyima usingizi wanawake kisiwani Pemba.

‘’Kama ningekuwa ninapesa za kufanyia kampeni katika maeneo yote ya jimbo langu naamini ningeshinda, kwani kila nikigombea idadi ya kura huwa zinaongezeka,’’anasema mama huyo.

Kila siku zinapoendelea, wanawake wanaojitokeza kugombea wanakata tamaa, hivyo Serikali pamoja na Tume ya Uchaguzi ikiwa hawatoviangalia kwa jicho la pili vyama vya siasa hususani vidogo vidogo kutapelekea kutokuonekana majimboni.

Riziki Mgeni Juma mwenye umri wa miaka 42 mkaazi wa Mtambwe wilaya ya Wete Pemba ambae aligombea udiwani wadi ya Mtambwe kupitia Chama cha Demockrasia na Maendeleo (CHADEMA) alifanya kampeni ya nyumba kwa nyumba na maskani, ili awafikie wananchi 16,237 wa wadi yake.

‘’Sikuwa na uwezo wa kufanya mikutano na ndio maana nikaamua kupiga hodi nyumba baada ya nyumba kuomba kura, lakini sikuwafikia wote,’’ anaeleza.

WANACHAMA WA VYAMA VYA SIASA

 Arafa Ahmad Juma mkaazi wa Tundaua Chake Chake ni mwanachama wa Chama cha Civic United Front (CUF) anasema, wanawake wengi wanaogombea hususan wa vijijini wanakua ni maskini hawamudu Gharama za chaguzi

Juma Kombo Hamad mwanachama wa Chama cha Alliance for Change and Transpareny (ACT WAZALENDO) mkaazi wa Wingwi Micheweni, anasema suala la uchaguzi linahitaji gharama, kwani wanawake wengi wanaogombea hawana ajira rasmi.

‘’Kama Serikali hawajalikalia kitako, hio 50 kwa 50 ya usawa wa kijinsia kwenye ngazi ya mamuzi haitofikiwa,’’anasema.

Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 kifungu cha 21 (3) kinaeleza kwamba, kila mzanzibari anayohaki ya kushika nafasi yoyote ya kazi na shughuli yoyote iliyoko chini ya Mamlaka ya Zanzibar.

Sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 Zanzibar ina wanawake wengi ambao ni 974,281 sawa na asilimia 51.6 kuliko wanaume, ikiwa wao ni 915,492 sawa na 48.4 ambapo licha ya uwingi huo bado idadi kwenye ngazi za maamuzi ni kidogo.

Kati ya hao, ni asilimia 21.14 tu kwa wanawake 71 waliojitokeza kugombea udiwani.

Kwa nafasi ya uwakilishi wanawake waliogombea ni 251, wakiwemo wanaume 190 na wanawake 61, ambapo walishinda wanaume 42 na wanawake nane (8) sawa na asilimia 16, wabunge walioshinda wanawake ni wanne sawa na asilimia 8,

VIONGOZI WA VYAMA VYA SIASA

Abass Mohamed Khatib Mratibu wa Chama cha Demokrasia Makini (DP) kisiwani Pemba anasema, mara nyingi chama chao kimekua kikiwasaidia wagombea wanawake gharama za uchukuaji wa fomu tu na sio kwenye kampeni.

‘’Hatuna ruzuku yoyote tunayoipata kutoka Serikalini, hivyo hatuna msaada wowote wa kuwasaidia ili waweze kujigharamia kwenye kampeni wakati wa uchaguzi,” amekiri Abass.

Mohamed Haji Kombo ambae ni Katibu wa Chama cha Wananchi (CUF) Wilaya ya Chake Chake anasema, umasikini ni kilio kikubwa kinachowakosesha nafasi wanawake waliopo kwenye siasa kupata nafasi za uongozi.

 ‘’Tume ya Uchaguzi Zanzibar ni chombo kinachoendeshwa na Serikali, kwanini kishindwe kuwasaidia wanawake na kuonekana wameingia kwa wingi kwenye nafasi za Uongozi?’ amehoji Mohamed.

Katibu wa Chama cha Mapinduzi CCM Wilaya ya Micheweni Khamis Juma Omar anasema, chama chao kimekua kikiwawezesha wanawake kwa kuwapatia mitaji ambayo itawainua kwenye shughuli zao hizo za uchaguzi.

‘’Anaposimama mgombea, hasimami kama Asha wala Halima pekee, bali chama ndicho kinachomsimamia na kumuwezesha hata kwa pesa kidogo ili aweze kufanikiwa,’’ anasema KhamiS


WANAHARAKATI

Tatu Abdala Mselem ni Mratibu wa Jumuiya inayoshughulika na makundi maalumu wakiwemo wanawake, watoto wenye ulemavu, watoto yatima, vijana na wazee wasiojiweza (TUJIPE) anasema, wanawake wamehamasika kujitokeza kugombea, lakini wanashindwa kuchukua nafasi.

‘’Bado suala la kifedha ni gumu kwa wanawake, kwani wengi wao wanaogombea wanatoka kwenye mazingira ya kimaskini,” anafafanua Tatu.


Afisa Mkuu wa Mahusiano kutoka chama cha Wandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) kwa upande wa Zanzibar Sophia Ngalapi anasema, wamekua kiguu na njia kwa ajili ya kuwaelimisha wanawake waweze kuingia majimboni kugombea.

‘’Ndoto zetu ni kuona wanawake wanaingia kwa wingi kwenye vyombo vya maamuzi, lakini gharama za uchaguzi bado zimekua zikiwakosesha kufikia malengo yao,’’anasema. 


MSAJILI WA VYAMA VYA SIASA.

Abdul-Razak Said Ali ambae ni Afisa Sheria kutoka Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa Zanzibar amekiri kuwepo kwa gharama katika chaguzi na kusema, kwasasa baadhi ya kanuni zinazoonekana kuwa na ukakasi ingawa tayari zipo katika mchakato wa kufanyiwa marekebisho.

‘’Sasa hivi kanuni zipo katika hatua za mwisho za kufanyiwa marekebisho, hivyo tusubirie mabadiliko vipi Sheria itatoa kipaombele katika suala la gharama kwa wanawake,’’anafafanua Abdulrazak.

 GHARAMA ZA KUFANIKISHA KUWA MWAKILISHI.

Kwa mujibu wa utaratibu ulivyo, anaetaka kugombea uwakilishi anatakiwa alipie chamani shilingi laki 100,000 kwa kuchukua fomu.

Pia anatakiwa kulipa Tume ya uchaguzi shilingi laki 200,000, wakati huo huo ukitakiwa kuchukua fomu ya pingamizi ambayo ni shilingi 300,000.

Licha ya gharama hizo za kununua fomu ya uwakilishi ili uweze kugombea na kutambulika kuna mambo ya lazima mgombea anatakiwa ayafanye ambayo yanawakwaza.

Kwa mujibu wa utaratibu uliowekwa na chama lazima uprinti picha kwa ajili ya kupachika kwenye kuta katika jimbo lako, kuwalipa viongozi siku ambayo wanakwenda kupiga kampeni ya nyumba kwa nyumba.

Vile vile wanahitajika kununua nguo (Sare) yoyote itakayotolewa na chama, pamoja na kuwalipa mawakala ambao watasimamia siku ya uchaguzi.

NINI KIFANYIKE

Hadia Omar Ali mkaazi wa Micheweni anasema, ikiwa Serikali haitokipatia ufumbuzi kilio hicho siku zote wanawake wataendelea kushikia mkia tu kwenye mamuzi.

Mkaazi wa Finya wilaya ya Wete Khamis Mohamed Kombo anasema, ipo haja kwa Tume ya Uchaguzi (ZEC) kuweka ruzuku malumu ambayo itawasaidia wagombea hususan wanawake.

SERA

Sera na Sheria mbali mbali za Zanzibar zimeelekeza kutambua haki ya mwanamke kushiriki katika demokrasia na uongozi.

Kifungu cha 21 (2) cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 64 kimeeleza kwamba, kila mzanzibari anayo haki na uhuru wa kushiriki kikamilifu katika kufikia uamuzi juu ya mambo yanayomuhusu mwanamke na taifa lake.

ILANI YA UCHAGUZI YA WANAWAKE.

Ilani ya Uchaguzi ya wanawake, Uchaguzi wa Serikali za mitaa ya mwaka 2019 na Uchaguzi mkuu wa 2020, Madai ya mtandao wa wanawake wameitaka serikali kusimamia matumizi ya rasilimali fedha, hususani ruzuku zitokanazo na kodi ya Watanzania, ili kuhakikisha zinatumika kwa kuziba mapengo ya jinsia wakati wa uchaguzi.

ILANI YA CHAMA CHA MAPINDUZI.

Moja ya mkakati wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi CCM ya mwaka 2024 imesema, ni kuwawezesha wanawake kushiriki katika ngazi mbali mbali za mamuzi.

 









Comments

Popular posts from this blog

HIVI NDIVYO UTELEKEZWAJI WA WATOTO UNAVYOATHIRI MALEZI, MAKUZI YAO

‘’KATIBU MKUU ELIMU ‘’TOENI ELIMU YA MALEZI BORA’’

UROHO WA MALI KWA WANAUME UNAVYONYIMA WANAWAKE ARDHI