TIGO ZANTEL wautunisha mfuko wa fidia kwa wanaoanguka mkarafuu





                          NA FATMA HAMAD,PEMBA

Mtandao wa simu wa Tigo Zantel umechangia shilingi milioni 350 kwenye mfuko wa fidia kwa ajili ya watu wanaopata ajali ya kuanguka mkarafuu wakati wakiwa katika harakati za uchumaji wa zao hilo.

Akizungumza mara baada ya kukabidhi mfano wa hundi ya milioni 350, huko Makonyo Chake ghake  Pemba, Mkurugenzi wa mtandao wa Simu wa Tigo Zantel Azizi Said Ali alisema wameamua kuchangia fedha hizo, ili

kuuboresha mfuko huo ambao utawanufaisha wahanga.

‘’Kwa vile na sisi Tigo ni sehemu ya familia tumeamua kutoa mchango wetu ili kuona wanaopata ajali nawao wanaingizwa katika bima maalum,’’alisema.

Akifungua hafla hiyo ya ugawaji wa zawadi kwa washindi wa vuna na Tigo pesa, Waziri wa biashara na Viwanda Zanzibar Omar Said Shaban amewataka wakulima wa zao hilo kuendelea kutumia mfumo wa malipo wa Tigo pesa katika kuuza karafuu zao.

‘’Niwaombe wananchi wenzangu endelea kuunga mkono mfumo huo,msisikilize maneno ya wasiopenda maendeleo,’’alieleza.

Aidha aliutaka uongozi wa Tigo pesa katika msimu wa vuna na tigo pesa ujao, kuhakikisha wanatoa zawadi ya gari kwa wakulima watakaouza karafuu zao na kupokea malipo kupitia Tehama, ili kuwatia hamasa wananchi kuutumia mfumo huo.

Akiwasilisha mfumo huo wa Tehama Mkurugenzi mkuu wa Tehama kutoka shirika la Biashara la ZSTC Najma Nuhu alisema kuna hatua tano ambazo mkulima atazipitia kabla ya kupokea malipo yake.

Alisema miongoni mwa hatua hizo ni pamoja na Usajili, Kutoa daraja, Kuchunga ili kupata karafuu safi, Kupima na mwisho ni malipo.

Alifahamisha kwa kupitia mfumo huo mkulima atapokea ujumbe wake wa malipo kwenye simu yake kabla ya kuondoka kituo cha kuuzia karafuu.

‘’Mfumo wetu ni wa papo kwa papo mkulima atapokea malipo yake akiwa yupo pale pale kituoni,’’alisema.

Nao wakulima ambao wamepokea zawadi walisema utaratibu huo ambao wameufanya Tigo zantel wa kutoa zawadi, utawahamasisha wananchi kuuza karafuu zao kwa kutumia mfumo huo wa kisasa


Katika hafla hiyo jumla ya washindi 25 wa Vuna na Tigo pesa walizawadiwa zawadi, ambapo 20 wamezawadiwa simu janja, Watatu walipokea Baskeli na wawili walipatiwa Piki piki.  



 

 

Comments

Popular posts from this blog

KERO YA MAJI, TATIZO KWA WANAKIJIJI CHA GOMBEUME

HIVI NDIVYO UTELEKEZWAJI WA WATOTO UNAVYOATHIRI MALEZI, MAKUZI YAO

DNA YA THIBITISHA, MTUHUMIWA NDIE BABA MZAZA WA MTOTO