WANANCHI WAHIMIZWA KUTUMIA VYAKULA VYENYE LISHE BORA

 



NA SALIM HAMAD, PEMBA

WANANCHI  Visiwani Zanzibar,wamehimizwa kuwa na uataratibu wa Unywaji wa  maziwa ili  kujenga afya zao na  kujikinga na magonjwa  mbali mbali yanayoweza kuwapata ikiwemo  utapiamlo.

 Afisa Mdhamini Ofisi ya Rais Katiba Sheria Utumishi wa Umma na Utawala Bora Halima Khamis Ali alitoa kauli hiyo wakati akizungumza na wananchi katika hafla ya unywaji wa Maziwa huko Maonesho ya Chakula Chamanangwe Kisiwani Pemba.

Alisema Watu wengi hawana muamko wa unywaji wa maziwa jambo linalodumaza afya hasa kwa watoto wadogo, hivyo ni wajibu wa kila mwana jamii kutambua umuhimu wa suala hilo.

Alisema mbali ya kuwa jamii imehimizwa jambo hilo lakini wanapaswa kufuata utaratibu unaotolewa na maafisa wa afya katika utumiaji wa lishe hiyo.

‘’Kila mmoja kwa nafasi yake anawajibu wa kuihamasisha jamii umuhimu wa unywaji  wa Maziwa kwani yamekuwa yakisadia katika kujenga afya zao huku  yakiwa mazuri kwa wanafunzi kwani yanaongeza akili’’alisema.

Mapema Afisa Mdhamini Wizara ya Afya Pemba,Khamis Bilali Ali alisema Wizara hiyo imekuwa ikihamasisha utumiaji wa lishebora hasa kwa mama wajawazito ikiwemo utumiaji wa maziwa na kuwanyonyesha watoto wao  kwa kipindi cha  miezi sita baada ya kujifungua kabla ya kuwalisha kitu Chochote ispokuwa maziwa.

“ maziwa ya mama ndio chakula kizuri kwa watoto kwani kinajenga mwili na akili” alisema Mdhamini huyo.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Shirika la Chakula Duniani kwa upande wa Tanzania (FAO )Lela  Miraji  alisema  shirika hilo litaendelea kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar,katika kuboresha mifumo ya  upatikanaji wa Chakula Duniani.

Naye Mkurugenzi Maendeleo ya Mifugo Asha Zahran Mohamed alisema uzalishaji wa  maziwa kwa siku lita 25,019 huku akifafanua kuwa kwa mujibu wa takwimu ya maotokeo ya Sensa iliyofanyika hivi karibuni ilionesha ni asilimia ndogo wa Unywaji wa Maziwa katika Visiwa vya  Unguja na Pemba.

Alisema katika uzalishaji wa Maziwa kuna changamoto kubwa inayojitokeza kwa wafugaji juu ya  malisho ya Wanyama kutokana na maeneo madogo ya Ufugaji hapa Zanzibar .

 

Comments

Popular posts from this blog

KERO YA MAJI, TATIZO KWA WANAKIJIJI CHA GOMBEUME

HIVI NDIVYO UTELEKEZWAJI WA WATOTO UNAVYOATHIRI MALEZI, MAKUZI YAO

DNA YA THIBITISHA, MTUHUMIWA NDIE BABA MZAZA WA MTOTO