UZAZI WA MPANGO UNAVYOINUA WANAWAKE KIUCHUMI,


 NA FATMA, HAMAD PEMBA

KUPANGA kutamka au kufanya jambo kunasaidia kupata mafanikio mazuri au kupunguza hatari na athari za matatizo.

Umuhimu huu wa kupanga pia unaonekana katika uzazi kwa vile uzazi wa mpango umethibitisha kuwa na faida nyingi kwa mama, mtoto, familia na taifa kwa jumla.

Uislamu umeeleza wazi kuwa uzazi wa mpango sio unaplekea kuwa na afya njema ya mzazi na mtoto tu, bali pia furaha, amani na mapenzi katika familia.

Baadhi ya watu  katika jamii  wamekuwa na imani potofu kwamba,  uzazi  wa mpango unapunguza kizazi na kusababisha   matatizo  kama  vile  kansa na   kutokwa  na damu nyingi  wakati wa hedhi.

 Hili halina ukweli kwa sababu utafiti na ushuhuda wa wanawake waliojiunga na mpango huu unathibitisha kwamba hio ni dhana isiyokuwa na mshiko.

 Asha Khamis wa Micheweni, Pemba,  anafurahia uamuzi wake wa kujiunga na auzazi wa mpango na kueleza kwamba ulimsaidi kupata muda wa kulea vyema watoto na kufanya biashara yake ya kuuza uji na mandazi.

‘’Nilikuwa nikinyonyesha  mtoto wangu kwa muda wa miaka miwili, na hii ilinipatia muda wa kufanya shughuli zangu za biashara kwa ajili ya kuendesha maisha yangu,’’alisema huku akitabasamu.

Amina Omar  Mselem aliyejipatia watoto 7 waliozaliwa kwa kupishana muda mrefu kidogo alisema uzazi wa mpango ulimpa fursa ya kushiriki  katika harakati  mbali  mbali  za  kijamii.

‘’Nilikua nikitumia uzazi wa mpango  na hii ilinipa muda wa kupumzika vizuri na kwenda harusini,  msibani, Kwenye vikoba na huku nikufurahia kulea , kucheza na watoto na kuwa na maisha ya furaha na mume  wangu,’’alieleza Amina.

 Maryam Said  mama  wa  watoto  wa  4, alisema  alianza kutumia uzazi wa mpango  mara tu baada ya kupata mtoto wake wa kwanza.

‘’Nimekuwa  nikitumia  uzazi  wa mpango kwa muda mrefu na sjapata tatizo lolote la kiafya,’’ alieleza Maryam.

 

Utafiti na ushuhuda unaonyesha wazi kuwa uzazi wa mpango unamsaidia sana mzazi na watoto na ndio maana wataalamu wa afya wanaishajiisha jamii kutumia  mpango huu kwa vile ni salama na hauna madhara.

WATALAMU WA AFYA.

Mtaalamu   wa  afya  wa  ofisi  ya  huduma  za mama  na  mtoto  katika Hospitali ya Chake  chake,  Fatma  Suleiman Daud,  alisema  njia za uzazi  wa  mpango  hazina madhara bali  ni  tiba  kwa afya ya binadamu.

‘’Mtu yoyote atakaeugua  ugonjwa wa Kansa dozi yake ya mwanzo anayotakiwa kutumia ni  dawa ya uzazi wa mpango,’’alifafanua.

Alisema uzazi wa mpango pia unasaidia kuwa na  mzunguko mzuri wa hedhi kwa akina mama  ambao  hawaingiii kwenye siku zao.

Uzazi wa mara kwa mara unapelekea   kushuka na kupasuka  fuko la uzazi na hii huhatarisha maisha ya mama.

‘’Hali za wanawake wengi  wanaozaa papo kwa pao huwa na upungufu mkubwa  wa damu,’’alieleza.

Alisema yeye pia anatumia uzazi wa mpango  na kwa sasa anao watoto  wawili, wa kwanza  ana  miaka 7  na  wa pili  mwaka  mmoja  na  nusu.

 ‘’Mimi  nilijiunga  na  uzazi  wa mpango kwa kuanzia  njia  ya  kijiti na sasa  ninatumia  Kitanzi.’’alieleza.

Alisikitishwa kuona ndoa nyingi za watu wa Zanzibar zinapelekea mwanamke kujikuta na mke wenza kutokana na mwanamke kuzaa  mara kwa mara, jambo ambalo hupelekea kutokuwepo amani katika nyumba na hubidi mume aongeze mke mwengine,’’ alifahamisha.

 Mengi yanasemwa na kutumia visingizio mbali mbali, lakini ukweli ni kwamba uzazi wa mpango ulikuwepo  tokea enzi za Mitume.

 Maryam  Ali Said , Mratibu wa huduma  za mama na mtoto Pemba, amesema maradhi humpata  mtu yoyote, na  pasitafute kisingizio cha kusema  sababu ni uzazi wa mpango.

‘’Tunao watu wengi walioutumia uzazi wa mpango mpaka walipofikia umri wa uzee na hawajapata tatizo lolote la kiafya,’’ amesisitiza.

Amesema wanaume wengi wanapata ugonjwa  wa kansa na jee hii utasema sababu yake ni uzazi  wa  mpango, aliuliza.

Alifahamisha kuwa maziwa ya mama ndio chakula bora pekee kinacho mjenga mtoto   kuwa  na  afya  bora na kukuwa kimwili na kiakili.

‘’Kitaalamu  mtoto anatakiwa anyonye maziwa ya mama  kwa miaka 2, kwani maziwa ya mama ndio yenye virutubisho vinavyohitajika kwa ukuaji mzuri wa mtoto,’’amefahamisha.

Baadhi madhara ya uzazi wa mpango yanayotajwa na wanawake ni pamoja  na kupata ugumu wa kushika mimba baada ya kutumia uzai wa mpango, kutokwa damu mara kwa mara, kupungua au kuongezeka kwa mwili, kuongezeka hamu ya kula, kupotea kwa hamu ya tendo la ndoa, mabadiliko ya siku za hedhi na maumivu ya kichwa.

Lakini utafiti wa kitaalamu umeonyesha sababu zote hizo ni zaidi za nadharia kuliko hali halisi.

 

MTAALAMU  WA  AFYA YA UZAZI

Rahila Salim Omar,  mtalamu wa  afya  ya uzazi, amesema zipo njia nyingi  za kupanga uzazi ambazo  zote ni salama na  miongoni  mwao ni  zile  za kisayansi na za kisasa ambazo  hazina madhara.

Alisema miongoni mwa njia hizo ni kutumia Kitanzi [Kijiti]  kwa mama ambaye hajazaa sana, sindano, vipandikizi, mipira ya kiume na ya kike  [Kondom] na zote hizi ni salama, na hutolewa kulingana na afya ya mama.

‘’Sio kweli kwamba ukipanga uzazi unapata matatizo, Tusidanganyane kwani kitaalamu hilo halipo’’, alisistiza.

Wapo ambao hutumia njia za asili za uzazi, kama ya kutegemea kalenda. Hii hufuata mzunguko wa hedhi au kumwaga mbegu za kiume nje ya njia ya uzazi.


KIONGOZI WA DINI.

Sheikh  Abdalla   Nassor  Abdalla kutoka Jumuia ya Maimamu  Pemba  (JUMAZA)  amesema  Uislamu unaukubali uzazi wa mpango na kisheria  mtoto anatakiwa anyonye maziwa ya mama kwa miaka 2 na hapo ndipo mama abebe ujauzito mwengine.

Mwenendo huu, amesema, unasaidia kuimarisha afya ya mama na mtoto,.

Sheikh Abdalla alifahamisha kwamba njia za kufunga uzazi zipo kwa wanawake na wanaume, na sio kwa wanawake tu. Kwahivyo ni vyema wanaume nao pia wazitumie.

Kwa mujibu wa takwimu za kituo cha huduma za mama na mtoto Pemba wa kipindi cha  Januari hadi Juni mwaka huu, watu 4020 walijiunga na uzazi wa mpango. Kati yao wanaume ni 63 na wanawake 3957.

Katika Hospitali ya Mkoani wanawake ni 711, wanaume 17, Chake chake wanawake 1228, wanaume 18,Wete wanawake 1085,  wanaume 13, na kwa Micheweni wanawake ni 873 na wanaume 18.

Ripoti ya Umoja wa Mataifa juu ya matumizi ya uzazi wa mpango imeonyesha ongezeko katika baadhi ya nchi, ikiwemo Tanzania. Takwimu zinaonyeha  kwa sasa ni asilimia 27 ya Watanzania wanatumia njia hizo, zikiwemo sindano, vipandikizi na mipira ya kiume na ya kike.

Hofu ya njia za uzazi wa mpango                

 Utafiti mpya wa Shirika la afya Duniani (WHO) umebaini kuwa theluthi mbili ya wanawake wenye uwezo wa kubeba mimba na ambao wana nia ya kuchelewesha kupata ujauzito au kudhibiti idadi ya watoto huacha kutumia huduma za uzazi wa mpango kwa hofu ya madhara ya huduma hizo.

Uzazi wa mpango sio tu ni suala la haki za binadamu bali pia ni kitovu cha uwezeshaji wa wanawake, kupunguza umasikini na kufikia malengo ya maendeleo endelevu - SDG’s (Uzazi wa mpango ni haki ya binadamu: UNFPA11 Julai 2018 ).




 

                        




 





Comments

Popular posts from this blog

UTELEKEZAJI WA WANAWAKE UNAVYOKATISHA NDOTO ZA WATOTO.

Mkuu wa Polisi Jamii Kaskazini Pemba akerwa na wanao wafungia ndani watoto wenye ulemavu.

Mrajisi wa Mahakama Zanzibar ahidi kula sahani moja na Mahakimu wasio wadilifu.