UTELEKEZAJI WA WANAWAKE UNAVYOKATISHA NDOTO ZA WATOTO.
NA FATMA HAMAD, PEMBA
……………..SIRI ya mtungi aijuaye kata………
Wahenga
wametupa usia usemao ……Hasira hasara. Wakati mwengine hio hasira sio tu
huathiri aliyefanya na aliyefanyiwa, bali watu wa karibu, mbali na hata jamii
kwa ujumla.
Hili
linaonekana sana pale ndoa inapovunjika baada ya wana ndoa kuamua lipasuke
tugawane mbao, lakini misumari ya hizo mbao huwachoma na kuwaumiza wengi,
wakiwemo wana familia na hasa watoto.
Mara nyingi pale wazazi wakiwa wametengana baada ya ndoa kuvunjika watoto hukosa huduma muhimu za maisha na kuathirika kimwili na kiakili na kiza hutanda katika safari yao ya maisha.
Mwana harakati maarufu wa kulinda na kutetea haki za watoto kisiwani Pemba, Tatu Abdala Mselem, amekuwa mara kwa mara akiiomba jamii kuvunjika kwa ndoa isiwe sababu ya kila mzazi kufumbia macho wajibu wake wa malezi ya watoto.
Hii
ni kwa sababu mtoto anapokosa huduma za lazima sio tu huwa mnyonge
na kujiona kama yatima aliyekosa msaada, bali huwa hana furaha anapocheza, na
akili yake huwa haifuatilii vizuri masomo.
‘’Kama ndoa imevunjika, kwa nini watoto waingizwe katika shida wakati wao sio walioingia kwenye mkataba wa ndoa, wala kupelekea wazazi watenngane?,’’anauliza.
Shehk
Said Ahmad wa Chake chake aliwataka wanaume waseme na nafsi zao, watulize akili
zao na inapobidi ndoa kuparaganyika basi waelewe bado wanayo dhima kubwa ya
kuhakikisha watoto wanapata huduma zote muhimu na hawateseki.
’Ndoa
ikifikia mwisho wake kwa kuvunjika sio kuvunjika kwa wajibu wa kulea
na kuhudumia watoto. Kwa mke huduma zinapaswa kuendelea mpaka inapomalizika
eda, lakini kwa watoto lazima ziendelee kwa ukamilifu’’, aliongeza.
Rashid
Said Nassor, Afisa Hifadhi ya Watoto katika Wilaya ya Chake chake
anashangaa iweje inapovunjika ndoa wathirika wakubwa wawe watoto
wakati wao hawakuhusika na kutengana kwa hao wana ndoa?
WATOTO WANASEMAJEE.
Mwanafunzi mmoja wa darasa la kwanza wa Skuli ya Kangagani
nilimkuta akiwa kwao nyumbani kwa takriban wiki mbili akiwa
amepiga kambi kwenye eneyo la uvunjaji wa kokoto, badala
ya kufanya kazi ambayo ndio ya mtoto. Nayo ni ya kusoma na kucheza.
Akinieleza kilichomsibu alisema alilazimika kufanya kazi hio ya sulubu
ili ajipatie mahitaji ya shuleni na nyumbani kwao baada ya baba yao
kutowajali kimaisha, kwa lugha ya siku hizi kuwatelekeza.
‘’Kwa sasa nabanja kokoto ili kujipatia vifaa vya skuli, kama
viatu na sare, kwani mama yangu hapatiwi huduma na baba’’, alisema.
Mtoto huyu alisema ilikuwa ni
mwaka wa saba hajaitia machoni sura ya baba
yake na amekuwa akisikia tu habari zake kutoka kwa mama yake, lakin hamjui huyo
baba yake.
‘’Nasikia baba yangu anaishi Unguja, lakini sijawahi kumuona
wala kupata huduma yake yoyote.
Kwa hivyo ikifika karibu na kipindi cha Sikukuu huenda kubanja
kokoto kwa ajili ya kujinunulia nguo,’’alileza.
Tabaan mtoto anayeishi katika mazingira kama haya huhisi unyonge
na kuathirika kisaikolojia pale anapoona watoto wenzake wapo na baba zao au
wanapewa pesa au kitu na huyo baba.
Pamoja na changamoto hizo zenye maumivu makali huyu mtoto amesema lengo lake ni kusoma kwa bidii ili kuwa daktari wa binadamu na kuisaidia jamii yake.
Mtoto Juma mwenye umri wa miaka [15] mkaazi wa Mjini Wingwi
(hilo sio jina lake halisi) anaefanya kazi ya uvuvi wa samaki,
amesema baba yao amewatelekeza takriban kwa miaka minane
na hawaulizi cha asubuhi wala cha jioni, cha kheri wala cha
shari.
‘’Nimejingiza kwenye shughuli hizi za uvuvi ili nipate pesa kwa
ajili ya matumizi ya nyumbani kwetu na mimi binafsi,’’ameeleza.
Ali Khamis Kombo mwenye umri wa [15] mkazi wa kijiji cha Mijini
Kiuyu aliacha kusoma na kufanya shughuli ndogo ndogo za kibiashara, kwa ajili
ya kumsaidia mama yake.
‘’Nyumbani tuko watoto 9 na mama hana kazi yoyote. Hivyo
nafanya kazi ili niendeshe familia yangu baada ya baba kutupa kisogo cha
kutuhudumia,’’ameeleza.
Asha Ali, mkaazi wa Mjini Kiuyu, mwenye watoto tisa
anasema huduma zote anajitegemea, ingawa bado yuko kwenye ndoa ya
mume alieongeza mke wa pili.
‘’Sio kama naona raha mwanangu kufanya biashara, lakini
nitafanyaje. Sina budi ila kumtaka anisaidie kimaisha,’’anasema.
Bi kombo Khamis mkaazi wa mjini Wingwi anaeleza kuwa mume wake
aliondoka kwenda uvuvini [dago ] Dar es Saalam karibu miaka minane iliopita na
hurudi wkati wa mwezi mtukufu wa Ramadhani tu.
‘’Ameniachia watoto nane [8] na huenda pwani
na watoto wangu kupanda
mwani ili tupate pesa za kujinunulia mahitaji mana baba yao
amenitelekeza,’’anafahamisha.
‘’Ukimuuliza mama kwa nini hawa watoto hawaendi skuli na badala
yake anawapa biahara kuuza anakwambia afanye nini na hana uwezo wa
kuwahudumia,’’anaeleza.
SHERIA ZA
AJIRA KWA WATOTO
Sheria
ya ajira na mahusiano kazini namba 8 ya mwaka 2006 inakataza mtoto mwenye umri
wa chini ya miaka 14 kuajiriwa na kukataza ajira kwa watoto wa chini ya miaka
18 katika maeneo ya migodi, viwanda, ubaharia katika meli au kazi nyingine
yeyote inayotambulika kuwa hatarishi.
Hata
hivyo, sheria inaruhusu ajira kwa watoto wa miaka 14 katika kazi nyepesi ambazo
sio hatarishi kwa afya yake, lakini haiathiri mahudhurio ya
watoto masomoni.
WANAHARAKATI WANASEMAJE
Semeni Ali Khamis, mwanaharakati kutoka Jumuiya ya
Wanawake katika wilaya ya Micheweni ameleza kuwa watoto wengi
wanaojiajiri ni wale ambao kuwa hawapati matunzo kutoka kwa wazazi wao.
‘’Katika kijiji changu cha Konde baadhi ya wanaume
hujiingiza kwenye masuala ya ulevi tu, hawana habari ya kushughulikia familia
zao,’’analeza.
‘’Utawakuta watoto muda wa kuwepo masomoni wamebebeshwa mabakuli ya Mchicha, Kombe, na hata Chaza na kutembeza mitaani, jambo ambalo linasababisha kufanyiwa udhalilishaji,’’ anasema.
OFISI YA MUFTI.
Afisa kutoka Ofisi ya Mufti iliopo Pemba, Abdalla Muhamed Abdala
,anasema utelekezaji wa wanawake unachangia kwa kiasi kikubwa watoto kujiingiza
katika ajira.
Kwa bahati mbaya siku hizi kumekuwa na ongezeko la talaka ambapo
kwa kipindi cha Juni hadi Agosti 2023, kupitia
ofisi ya Mufti wamelazimika kutoa talaka 18 na kupokea malalamiko 9 ya
utelekezaji wa familia.
Alisisitiza ni vyema watoto wakapatiwa huduma muhimu na malezi
ya familia ili wakuwe vizuri kwa faida ya taifa kwa ujumla.
Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Watu
Wenye Ulemavu wa Jamuhuri ya Mungano wa Tanzania, Patrobas Katambi,
amesema serikali haitavumilia kuona watoto wanakosa haki zao za
msingi .
‘’Ni
kosa kuajiri watoto kinyume na sheria inavyosema na adhabu inatolewa chini ya
kifungu cha 102 (2) ambacho kinampa Hakimu wa wilaya na mkazi kutoa adhabu sawa
na faini isiyozidi shilingi milioni 5 au kifungo cha mwaka mmoja au vyote,’’
anafafanua.
Kwa mujibu wa takwimu kuna watoto milioni 152 wanatumikishwa duniani hivi sasa na kati yao 25,803 ( asilimia 5.6) wapo katika ajira Zanzibar. Watoto hawa wa umri wa kati ya miaka mitano hadi 17 wameajiriwa au wamejiajiri.
Hali hii imebainishwa katika taarifa ya Waziri
wa Nchi, Afisi ya Rais, Kazi, Uchumi na Uwekezaji, Mudrik Ramadhan Soraga,
katika maadhimisho ya Siku ya Kupambana na Ajira za watoto mjini Zanzibar. Siku
hii huadhimishwa rasmi kila ifikapo Juni 12 ya kila mwaka.
Kwa mujibu wa takwimu za kitengo cha hifadhi ya mtoto Pemba katika wilaya ya Micheweni kwa mwaka 2022, malalamiko yalioripotiwa ya utelekezwaji wa wanawake ni 71, ambapo yamehusisha watoto 185, wanawake 92 na wanaume 93.
Kuanzia
mwezi Januari hadi Agosti mwaka huu malalamiko yaliyopokelwa ni
28,watoto walioripotiwa kutelekezwa ni 84 ( wanaume ni 49 na wanawake
35).
Shirika la Kazi Duniani
[ILO] linakadiria kuwepo watoto 152 milioni katika ajira
duniani na kati yao 73 milioni wamo katika
kazi ambazo ni hatari.
Karibu asilimia 70 ya
ajira hizi za watoto ni katika kilimo na sababu kubwa ni
kutokana na umasikini na ugumu wa wazazi kupata ajira zenye hadhi.
Sheria
ya Elimu Zanzibar ya 1982, kifungu cha 20, cha sharia hiyo kinamtaka
kila mzazi kuhakikisha anampatia mtoto wake elimu ya lazima pale anapofikia
umri wa miaka saba..
Katiba ya
Zanzibar ya 1984 inaeleza wazi katika kifungu cha 15[1] kuwa kila mtu ana
stahili kuheshimiwa na kupata hifadhi kwa nafasi yake; maisha yake binafsi naya
nyumbani kwake, na pia heshima na hifadhi ya maskani yake na mawasiliano yake.
Pia kifungu cha 12[1]
watu wote wapo sawa mbele ya sharia, na wanayo haki, bila ya ubaguzi wowote,
kulindwa na kupata haki sawa mbele ya sheria.
MKATABA WA AFRIKA.
Kwa mujibu wa Mkataba
wa Afrika wa Haki na Ustawi wa Mtoto [1999], kipengele cha 15, kinaeleza mtoto
ana haki ya kulindwa dhidi ya kazi au ajira zitakazoathiri afya, elimu na
maendeleo yake.
Serikali inatakiwa
kuweka sheria za kima cha chini cha mshahara, muda wa kufanya kazi,
mazingira ya kazi na adhabu kwa wasio tekeleza haki hii.
Pia inawajibu wa kutoa
elimu kwa jamii juu ya athari za kazi au ajira mbaya kwa watoto.
MKATABA WA UMOJA WA
MATAIFA.
Mkataba wa Umoja wa
Mataifa wa Haki za Mtoto [1989] kipengele cha 32, kinaeleza mtoto ana haki ya
kulindwa dhidi ya kazi au ajira zitakazoathiri afya au elimu yake.
Comments
Post a Comment