VIKUNDI VYA USHIRIKA VYAOMBA KUUNGWA MKONO
NA
FATMA HAMAD PEMBA
Wanakikundi
cha Mapambano Co-Oparative
kinachojishuhulisha na ufugaji wa Samaki, Kaa na Kamba kilichopo Sizini
wilaya ya Michewemi mkoa wa Kaskazini Pemba wameiomba Serikali ya Mapinduzi
Zanzibar, pamoja na asasi nyengine kuviangalia na kuviunga mkono vikundi vya
ushirika, ili viweze kwenda samba mba na Sera ya Serikali ya Uchumi wa Buluu.
Wakizungumza
na mwandishi wa habari hizi huko kwenye Kikundi chao
Sizini Wilaya ya Micheweni walisema sera ya Serikali ya Uchumi wa Buluu
ni kuhakikisha wanaviinuwa
vikundi vya ushirika ili viweze
kutoa tija na kuondokana na umasikini.
Alisema wamekuwa
wakipata faida kubwa kwani tayari
wameshapata pesa za kuendeshea maisha
yao kupitia mavuno waliovuna
msimu uliopita.
‘’ Tumeamua kufuga, Kamba na Samaki jambo ambalo litatuwezesha kujingizia kipato,
hivyo twaiomba Serikali ituunge mkono kihali na mali ili kutimiza malengo ya
Serikali juu ya uchumi wa buluu,’’ walieleza wanakikundi.
Mapema Naibu katibu wa kikundi hicho Thamrat Suleiman Said aliwataka wanakikundi
wenzake wasikatishwe tamaa na maneno ya
watu bali waendelee kupambana
wakiendeleze kikundi chao.
“ Sisi kama vijana wa kike ni lazima tujiamini,
tupambane ili tuweze kukiendeleza
kikundi chetu jambo ambalo litatusaidia kupata kipato cha halali, “
alifahamisha.
Akitoa nasaha kwa wanakikundi hao Meneja wa mipango ya Bahari na Pwani kutoka Shirika la International Union for
Conservation of Nature ( IUCN ) Elinasi Monga, alisema ni vyema kwa
wanakikundi hao kuendeleza mradi wao
huo wa ufugaji wa Samaki na Kamba kwani sasa hivi Duniani kote wamelekeza nguvu
zao kwenye bahari.
“ Mukiitumia bahari vizuri mtaweza kuondokana na
Umasikini, mtakuza uchumi wa nchi pamoja na kuondokana na mabadiliko ya tabia
ya nchi’’, alifahamisha Meneja.
Alisema endapo watajipanga
na kuachana na migogoro wataweza kujipatia kipato ambacho kitaweza kuendesha maisha yao sambamba na kujipatia
ajira.
Nae Ofisa mdhamini wizara ya Uchumi wa Buluu Dk, Salim Moh’d
Hamza aliwataka kuendeleza ushirika wao kwani kutawawezesha kupata fursa mbali
mbali za kimaendeleo zilizopo Nchini
kupitia sekta ya Uvuvi.
“Serikali ya Zanzibar
inalengo la kuekeza zaidi kwenye sekta ya bahari, hivyo ni vyema mjitoe
ili kuendana na soko la dunia,’’ alisema Ofisa mdhamini.
Alisema wizara itaendelea
kuwasaidia wanakikundi wanaojishuhulisha na masuala ya baharini ili
waweze kuenda na Sera ya Serikali ya Uchumi wa buluu.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa kikundi hicho Khalfan Hamad
Khalfan alisema kikundi hicho kilianzishwa mwaka 2013, kilianza na wanachama 10
wanawake 5 na wanaume 5, na sasa kinawanachama 17 wanaume 8, wanawake 9 tayari
walishawahi kuvuna mara tatu.
Hata hivyo alieleza kwa msimu huu wameingiza vifaranga vya Kaa
kilo 150, wenye thamani ya shilingi Laki tisa (900,000) Samaki vifaranga Elfu
kumi na moja mia tano na nne (11,504) wenye thamani shilingi milioni Nne Elfu ishirini na Sita na
mia nne (4,026,400) na Kamba ndoo mia tisa wenye thamani ya shilling Milioni Saba (7,000,000).
Comments
Post a Comment