KILIMO MSITU TARAJIO LA KUJIKOMBOA NA UMSKINI
NA FATMA
HAMAD, PEMBA
MKURUGENZI
WA Jumuia ya uhifadhi Mazingira Pemba CFP Mbarouk Mussa Omar amezitaka kamati zinazosimamia masuala ya
uhifadhi wa mazingira kuhakikisha wanaendeleza shughuli hizo ikiwemo kilimo
msitu, ili kuona wanajipatia kipato.
Mkurugenzi huyo ameyasema hayo wakati akizungumza na
wanakamati hao ambao ni kutoka shehia za Chwale, Kambini kichokochwe, Kiuyu na
Mchangamdogo katika mafunzo ya siku mbili ya kuweka mikakati madhubuti ya
kuendeleza shughuli za uhifadhi mazingira,yaliofanyika Ofisi za CFP huko
Minyenyeni mkoa wa Kaskazini Pemba.
Alisema kilimo ndio
tegemeo kubwa la Taifa, hivyo ni vyema wanakamati hao kuendelea kulima kilimo
msitu, waweze kuzalisha mazao ambayo yatawasaidia kupata chakula pamoja na pesa
ambazo zitaendesha maisha yao.
‘’Ndugu zangu shughuli hizi za kulima kilimo msitu msifanye
kwa sababu tu ya mradi, bali ifanyeni
kama ni kazi yenu ya kila siku, kwani mukifanya hivyo mtapata mazao
mtakula nyumbani na mengine mtauza mtapata pesa mtasomeshea watoto
wenu,’’aliwanasihi.
Aidha alisema endapo watajiendeleza na shughuli hizo
wataondokana na utegemezi sambamba kujipatia kipato na sio kukaa na kusubiri
ajira serikalini.
Kwa upande wake Afisa kilimo Msitu na usawa wa kijinsia Sada
Juma Segeja alisema lengo la mafunzo hayo kwa kamati hizo ni kuwahamasisha
suala zima la usawa wa kijinsia katika masuala uhifadhi wa mazingira.
Alisema wanaiwezesha kamati hiyo kutoa elimu kwa jamii kuona
mwanamke anamiliki ardhi yake mwenyewe, aweze kulima kilimo msitu apate mazao
ambayo yatamuezesha kuendesha maisha yake bila kumtegemea mtu.
‘’Kwa kweli lengo hasa la kuundwa kwa kamati hizi ni kwenda
kuibadilisha jamii kuacha fikra potofu na kumpa fursa mwanamke aweze kumiliki
adhi ili weze kutunza mazingira kama anavyofanya mwanamme,’’alisema.
Nao baadhi ya wanakamati hao walisema watahakikisha elimu
hiyo wanaifikisha katika jamii zao na kuona wanawake wanapata fursa mbalimbali
ikiwemo uongozi, kumiliki ardhi sambamba na kutunza mazingira.
MWISHO.
Comments
Post a Comment