MRADI WA SWIL ULIVYOLETA MABADILIKO KWA WANAWAKE WENYE ULEMAVU PEMBA
NA FAMA HAMAD, PEMBA
Mradi
wa kuwawezesha wanawake kudai haki zao za uongozi , demokrasia
na siasa (SWIL) umeandika historia mpya katika visiwa vya Zanzibar,
umeleta nuru na matumaini kwa wanawake, hususan wale wenye ulemavu, waliokuwa
kwa muda mrefu wakihisi kusahaulika katika safari ya maendeleo na uongozi.
Mradi huo
ulizinduliwa rasmi mwaka 2020 na unatarajiwa kumalizika Disemba 2026 umeonekana
na mafaniko makubwa katika hatuwa mbalimbali za utekelezaji wake.
Utekelezaji huo wa (SWIL)
ni ushirikiano kati ya TAMWA-Zanzibar, ZAFELA, JUWAUZA, na PEGAO, umewafikia
wanawake zaidi ya 4,000 katika
wilaya za Pemba na Unguja, ukiwajengea uwezo, ujasiri, ari na ya kugombea
nafasi mbalimbali za uongozi.
Lengo kuu la mradi ni
kuongeza ushiriki wa wanawake, ikiwa ni pamoja na wanawake wenye ulemavu,
katika michakato ya uongozi, siasa na demokrasia Zanzibar (Unguja na Pemba)
hivyo kuwawezesha kuwa “watendaji hai” badala ya kuwa katika pembezoni.
Utekelezaji
wa mradi huo kwa sasa umeshawafikia na
kuwawezesha zaidi ya wanawake 6000 kwa zanzibar, Unguja na Pemba katika kudai
haki zao ili nao waweze kuwawezesha wengine, ambapo tayari umeonyesha njia kwa
Wanawake Wenye Ulemavu katika kufikia
hatuwa ya kudai haki zao za uongozi.
Mradi
huo wa SWIL unafadhiliwa na ubalozi wa
Norway unatekelezwa maeneo mbalimbali ambapo kwa upande wa Pemba
tayari umeshawafikia wastani wa wanawake 4000.
Katika
hatuwa za kufanikisha lengo la mradi la kuwawezesha wanawake kudai haki zao za
uongozi demokrasia na siasa kumeundwa kamati za Wilaya za kuhamasisha wanawake
kudai haki zao za uongozi.
Kamati
hizo zinajulikana kwa jina la kiutaalamu 'citizen brigged' asilimia 60 ni
wanawake na 40 ni wanaume ambao ndio walengwa wakuu wa kutowa ushirikiano
kufikia malengo ya mradi huo.
Wanawake wenye ulemavu
waliunganishwa zaidi na mradi kupitia Jumuiya ya Wanawake Wenye Ulemavu
Zanzibar (JUWAUZA), waliweza kupata mafunzo na kutambuliwa kama wanaharakati na
haki zao.
Hivyo (JUWAUZA) Ofisi ya
Pemba imetoa ushuhuda wa wanawake wenye ulemavu ambao kupitia mafunzo ya SWIL waliyoyapata
waliweza kuhamasika, na katika uchaguzi
mkuu wa 2025 walijitokeza kwa wingi majimboni ambapo walikua ni 12, kwa Pemba
pekee, ingawa hawakubahatika kuyakamata majimbo hayo.
JUMUIA YA WANAWAKE WENYE
ULEMAVU INASEMANINI JUU YA HILO
Hidaya
Mjaka Ali kutoka jumuia ya wanawake wenye Ulemavu kisiwani Pemba anasema Mradi
wa SWIL umewanufaisha wanawake wenye Ulemavu, kwani katika Uchaguzi wa mwaka
huu 2025 Wanawake wenye ulemavu kisiwani
Pemba wamehamasika na wamejitokeza kugombea nafasi mbalimbali za uongozi,
ikiwemo Ubunge, Uwakilishi na Udiwani, ambapo haijawahi kutokea katika chaguzi
zilizopita.
Anasema
jambo ambalo limepelekea wanawake hao kujitokeza kwa wingi kuchukua fomu za
kugombea ni kutokana na elimu walioipata kupitia mradi wa SWIL, iliyokua
ikitolewa na Tamwa Zanzibar na Pegao.
‘’Haijawahi
kutokea wanawake wenye ulemavu kujitokeza wengi kugombea nafasi za uongozi na
kufikia idadi ya 12, hivyo napata kusema mradi wa Swil unatusaidia sisi wanawake
wenye ulemavu,’’anasema.
Anasema
katika miaka ya nyuma wanawake wenye ulemavu walikua wakiachwa nyuma katika
fursa mbali mbali, ingawa mradi wa SWIL umewaona, umewasadia na wameweza
kufahamu haki zao na nafasi zao.
Anasema
licha ya kuwepo kwa changamoto ambazo zimekua zikijitokeza kwa wanawake wenye
ulemavu, wamejenga uthubutu wa kuwania nafasi mbali mbali za uongozi.
USHUHUDA WA WANAWAKE
WENYEWE WENYE ULEMAVU
Halima Suleiman Ali mwenye ulemavu wa uoni
hafifu mkaazi wa Mtambile Mkoani Pemba, anasema awali alikosa utayari
katika kushiriki mchakato wa kutafuta
nafasi ya uongozi hususani majimboni.
Anasema kupitia mradi huo ameweza kujiamini na kuongeza uthubutu wa kuwania
nafasi ya Udiwani licha ya kushindwa kutokana na sababu zilizopo katika
michakato ndani ya vyama.
‘’Kutokana na uwelewa na ujasiri nilioupata
nimethubutu kuchukua fomu ya kugombea
Udiwani katika wadi yangu ya Mtambile,’’anasema.
Anasema
katika maisha yake hakua na imani kama kuna siku atachukua fomu na kugombea,
kwani hakua na elimu hiyo, ingawa kupitia SWIL anajivunia kwani ameondokana na
woga na ndio maana 2025, akachukua fomu kwa ajili ya kuusaka Udiwani.
Amina Abdala Said mwenye ulemavu wa viungo mkaazi
wa Changaaweni Mkoani Pemba, anasema mradi
wa SWIL umemjenga kwani amekua na
uthubutu na mwaka huu 2025, amekua Diwani
wa viti maalumu kupitia Chama cha ACT WAZALENDO wadi ya Changaweni.
‘’Baada
ya kupatiwa mafunzo licha ya kua sikujitupa jimboni ila nilingia kwenye
kinyanganyiro cha viti maalumu kuwania udiwani na nashukuru nimefanikiwa
kuikamata nafasi hiyo.
Mwengine ni Katija Mbarouk Ali mwenye Ulemavu
wa viungo mkaazi wa Kiuyu Minungwini wilaya ya Wete Pemba, anasema awali
hakua na uthubutu wa kushiriki katika mchakato wa kutafuta nafasi ya uongozi
hususani katika majimbo, ingawa kupitia mradi huo ameweza kujitolea ,kujiamini
na kuongeza uthubutu kuwania nafasi ingawa hakubahatika kuitia mkononi nafasi.
JAMII
Salim Khamis Juma
(43) mkaazi wa Wingwi Micheweni anasema kabla ya kuja mradi
wa SWIL wanawake hawakujuwa haki zao na ndio maana ikawa nafasi nyingi ilikua zinachukuliwa
na wanaume na wao sikuzote kubakia mkiani.
Anasema hatuwa inayochukuliwa na mradi kupita kila shehia kuweza kutowa elimu hiyo ni ya mfano kwa vile
wanawake wengi walikuwa wamelala katika suala la kudai haki zao hasa za uongozi
na kuwaachia wanaume peke yao.
“Mimi mwenyewe nilikuwa naona kama hakuna umuhimu wa wanawake
kuwa viongozi, ila kumbe tukiwapa
wanawake kuongoza kuna mafanikio mengi yanaweza kupatikana kwa mfano Raisi wetu
Mama Samia ambavyo anapambana tumepata neema kubwa kupitia kwake, kwa vile wao
ni waaminifu kuliko ata sie wanaume
Yumna Khamis Ali (32) wa Kinoe
Konde anasema elimu inayotolewa na mradi wa Swill imeweza kuwafunuwa macho
wanawake wengi na wanaelewa kuwa zipo fursa mbalimbali wanazikosa kutokana na
nafasi nyingi kuchukuliwa na wanaume.
“Huku vijijini zamani tulikua tuko nyuma hasa katika masuala ya uongozi kwani tulikua
tumezoea kwamba mwanamke ni mtu wa kukaa nyumbani tu na si wa kuwa kiongozi,
ingawa kwa sasa mambo yamegeuka,’’anasema.
Anasema uhamasishaji huo haukulenga tu kuwajengea uwezo
wanawake hao kuwa viongozi serikalini wala vyama vya siasa pekee bali hata
ndani ya sekta zilizomo kwenye jamii.
"Wanawake wenye Ulemavu hawatakiwi tu kuingia ndani
ya Serikali bali hata ndani ya vyama, kamati za maendeleo , jumuiya ,
nafasi za usheha na maeneo mengine",alisema.
Anafahamisha kuwa idadi ya wanawake wenye Ulemavu katika
kugombea nafasi za uongozi kwenye uchaguzi wa mwaka 2025, imeongezeka, licha
kwamba katika nafasi za maamuzi bado ni wachache.
‘’Kwa kweli SWIL imeikomboa jamii na
hata wanawake, kwani umepunguza ile dhana potofu kwa jamii kwamba mwanamke
hawezi kuongoza, kazi yake ni mama wa nyumbani tu,’’anasema.
Balozi
wa Norway kutoka Tanzania Tone Tinnes anasema ili kufikia ndoto za wanawake
wenye ulevu juu ya suala la usawa wa kijinsia, ni lazima kwa watekelezaji wa
mradi huo wa SWIL, kuendeleza mapambano ya hali ya juu, bila kujali mitazamo ya
watu wasio watakia mema wanawake hao.
Anasema mabadiliko hayapatikani kwa mara
moja, na kuielimisha Jamii juu ya
masuala ya kijinsia sio jambo rahisi, ni
vyema kuongeza mapambano ya hali ya juu
ili kuhakikisha lengo la usawa linafikiwa.
“Yapo mambo hupaswa wanawake wajiamulie wenyewe na sio busara
kuona mifumo dume inatawala hadi kwa mambo ambayo ni ya pamoja au yanawahusu
wanawake pekee,”alisema.
Robati Migua Ndalami kiongizi wa dini Kwa upande wa Kikristo
kutoka Chakechake anasema hata dini yao haijamktaza mwanamke
kuongoza kwani kuna mabo
ambayo yanawahu na yanatakiwa wayazungumze wenyewe.
Takwimu
Katika Uchaguzi wa mwaka huu 2025, unaweka historia mpya, kwani ni
mara ya kwanza wanawake kujitokeza kwa wingi
Ripoti za vyombo vya habari na mashirika ya jinsia
zinaripoti ongezeko la wanawake wanaogombea mwaka 2025 ikilinganishwa
na uchaguzi uliopita.
Zanzibar pia imeona wanawake wakichukua nafasi kubwa
katika kuingia kwenye nafasi za juu za uongozi,ikiwa ni sehemu ya mwelekeo wa
kitaifa wa kuhamasisha ushiriki wa wanawake katika siasa.
MIKATABA
Tanzania imeridhia Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa Haki za
Watu Wenye Ulemavu (CRPD), wa mwaka 2006 kinahimiza serikali, kuhakikisha
ushiriki sawa wa watu wenye ulemavu katika siasa na maamuzi.
Hata Mkataba wa kimataifa wa haki za kiraia na haki za kisiasa ya
mwaka 1966 ibara ya 25, kila raia ana haki ya kupiga kura na kuchaguliwa,
katika uchaguzi wa kisiasa.
Katiba ya Zanzibar ya 1984,kifungu chake cha 21(1) nacho
kinatambua haki ya kila raia, kushiriki katika shughuli za utawala wa nchi bila
ubaguzi.
Kifungu kidogo cha (3) kinaeleza kwamba, kila mzanzibari anayohaki
ya kushika nafasi yoyote ya kazi na shughuli yoyote iliyoko chini ya mamlaka ya
Zanzibar.
Sheria ya watu enye ulemavu namba 8 ya mwaka 2022, kifungu cha
29 kinaeleza, umuhimu wa watu wenye ulemavu kufikia miundombinu pamoja na
taarifa, mawasiliano na haki zote za kibinadamu.
Katika Nchi ya Nordic ilikua ya kwanza duniani kuanza upendeleo
wa kijinsia wa asilimia 40,kwenye bodi za kampuni zilizoorodheshwa mwaka 2005,
ikianzisha msukumo wa kimataifa wa kulazimisha kampuni kuwa na wanawake wengi
kwenye bodi.
Makampuni makubwa ya binafsi ya Norway lazima yawe na bodi
ambazo zinajumuisha angalau asilimia 40, ya wanawake au yatafungwa serikali
ilipendekeza katika muswada katika msukumo zaidi wa kuvunja dari ya kioo
inayozuia wanawake kufikia nafasi za juu.
Comments
Post a Comment