BISHAMBA ALI ALAWI: MWANAMKE MWENYE UTHUBUTU PEMBA

 


NA FATMA HAMAD, PEMBA

‘’Mwanamke akipewa nafasi ya kumiliki ardhi na akajishughulisha na kilimo, basi haachi nyayo pekee ardhini, bali huacha alama ya mafanikio,’’

Hayo si maneno ya mtu mwengine bali ni mwanamke mpambanaji mkaazi wa shehia Kambini Wilaya ya Wete Pemba, Bishamba Ali Alawi.

Katika mazingira ya kawaida ya vijijini, mwanamke huyo sasa ni kielelezo tosha jinsi kilimo msitu (Agro forest) kinavyombadilisha maisha yake.

Anasema, alipitia ugumu kwenye maisha yake kutokana na kukosa kazi ya maana ya kujikwamua kiuchumi ingawa hakukata tama.

Lakini tangu mwaka 2023 aliposhiriki mafunzo ya kilimo msitu, alianza kuona mabadiliko ya maisha kuwa mazuri kwa upande wake.

Kupitia mafunzo yaliotolewa na Chama cha Wandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) kwaupande wa Zanzibar na Jumuia ya Uhifadhi wa Misitu Pemba (CFP), Bishamba alijifunza kuchanganya aina ya miti mbali mbali kwenye shamba lake.

Walifunzwa kwamba, uchanganyaji wa miti kwenye shamba moja unasaidia kupata mazao kwa ajili ya chakula na biashara, huku wakidhibiti madhara yanayoweza kutokea ikiwemo mmong’onyoko wa ardhi na mabadiliko ya tabianchi.

Katika shamba lake mama huyo amepanda migomba, miparachichi, mboga, njugunyasa, choroko, miembe,mikungu na midimu.

Anasema, hali hiyo pia inapunguza gharama za mbolea na kuongeza mavuna, ambayo inasaidia ustawi bora wa maisha ya mazao hayo.

Anasema, mwakajana alipovuna kwa mara ya kwanza mazao yake, alifanikiwa kupata chakula na mazao mengine aliuza na kupata fedha ambazo zimemuinua kiuchumi.

‘’Siku ile ya Jumapili nilipopata pesa yangu baada ya kuuza mazao, nilijua huu ni mwanzo mpya wa maisha yangu,’’anasimulia kwa tabasamu Bishamba.

Anaeleza, kwa sasa ameboresha vya kutosha shamba lake na limesheheni miti na mazao, hivyo hataabiki kwa chakula, mboga wala pesa za matumizi.

Hadi sasa ameshavuna zaidi ya mara tatu na bado mazao yamejaa shambani, anasubiri yapee aanze kuvuna.

‘’Tangu nianze kulima kilimo hichi sihangaiki wala simsubirii mume wangu arudi na safari zake ndio nipate chakula, kwani ndizi, mboga, mihogo napata shambani kwangu,’’anaeleza.



Anasema kilimo msitu kimekua mkombozi kwake kwani amekua  akijipatia mahitaji yake yote anayoyahitaji, pia amekuwa akiwasaidia wanawake wengine kufanya shughuli hizo, ili nawao wajikomboe kiuchumi  waondokane na umasikini na utegemezi.

‘’Nimeshafundisha wanawake takribani 12 juu ya kilimo hicho, ambapo wengine wamekua viongozi wakulima matioti, wengine  wamekua wakulima wakubwa na wameanza kufaidika’’,anasema.

Anasema, alipoanza shughuli ya kilimo jamii ilimchukulia kama hana kazi na amechanganyikiwa tu maisha, ingawa sasa wanayaona matunda yake na wanatamani kuwa kama yeye.

‘’Mwanzo wananchi walinisimanga, kunikebehi na kuonekana kama sina kazi, ila sasa hivi wananishangaa na kila mmoja amehamasika anataka nimfundishe kwa faida ninayoipata,’’ anasimulia.

KUTOKA SHAMBA HADI UONGOZI

Sasa Bishamba aligombea nafasi ya viti maalumu ingawa hakubahatika kupata, lakini akiwa hai atahakikisha anaingia tena kwenye kinyang’anyiro cha kugombea ifikapo mwaka 2030.

Anasema, mbali na kujipatia pesa na chakula, bali mafunzo hayo yamemjengea uthubutu na ujasiri wa kusimama pahala popote kuzungumza bila woga.

‘’Kabla sijaanza mradi huu wa kilimo msitu ilikuwa siwezi hata kusimama mbele ya watu wawili tu, lakini sasa sina woga, nimekuwa kiongozi kwa sababu nawafahamisha wanawake umuhimu,’’anasema.

‘’Nina miaka 54, sijawahi kujiingiza kwenye harakati za uongozi, lakini mara hii baada ya kujengwa na kuandaliwa kupitia mafunzo hayo, nimejaza fomu ya uwakilishi viti maalumu lakini sikufanikiwa,’’ anaeleza.

Hadithi ya Bishamba sio tu simulizi ya mavuno na mapato bali ni alama ya uthubutu wa mwanamke wa kijijini, anaeamua kusimama imara katika harakati zake za kiuchumi na kisiasa.

Uthubutu huo wa Bishamba unatoa mwanga kwa wanawake wengine wa Pemba na Zanzibar nzima kwamba uongozi na maendeleo endelevu vinaweza kuanzia shambani.



Jirani wa Bishamba, Sharif Hamad Sharif mkaazi wa Kambini Kichokochwe anamuelezea mama huyo kuwa ni wa kawaida tu kijijini, ingawa kwa sasa amekuwa mfano wa kuigwa.

‘’Tulikua tunamchukulia kama mama ambae hana uwezo wowote, ingawa kwa sasa ni mwanamke wa mfano, kutokana na kujituma kwake na ameweza kutuamsha na sisi,’’ anaeleza.

Khadija Ali Faki mkaazi wa Chwale ni mwanamke ambae amejengewa uwezo na uthubutu na Bishamba, amejiingiza kwenye harakati za kilimo msitu na sasa ameondokana na utegemezi katika maisha yake.

Yeye alikuwa ni mama wa nyumbani tu na hakua akijishughulisha na kazi yoyote, hali ambayo ilikua ikimfanya kuishi mazingira magumu.

‘’Nilikua nikimtegemea mume wangu kwa huduma zote, jambo lilikua likiniwia vigumu mana maskini hawezi kuzimudu shida zote,’’ anaeleza.

Anasema, baada kupatiwa elimu na Bishamba, anaamini hali itabadilika, kwani analima kilimo msitu atapata mazao kwa ajili ya chakula na biashara, ili apate pesa za kujitatulia shida zake.

TAMWA WANASEMAJE

Chama cha Wandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA) Zanzibar kimekua mshirika mkuu katika kumuinua Bishamba na wanawake wengine kupitia miradi mbali mbali.

Ambapo, katika tamko lao la Machi 2024, linasisitiza kwamba… ‘Sera za jinsia lazima ziwepo katika sekta zote, ili wanawake wasiachwe nyuma’

‘’Tunataka wanawake washiriki sio tu mashambani bali pia kwenye meza za maamuzi na ndio maana tunawawezesha kwa namna zote ili lengo letu likamilike,’’ anasema Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano kutoka TAMWA Zanzibar, Sofia Ngalapi.

Anasema, katika mradi wao wa  kilimo msitu (ZanzAdapti)  ambao wanautekeleza pamoja na CFP Pemba, CFI kutoka Canada, unawasaidia wanawake wa pwani na visiwani, kuimarisha nafasi zao katika kilimo, mazingira na uongozi.

CFP

Mtetezi wa masuala ya wanawake kutoka Jumuia ya Uhifadhi wa misitu kisiwani Pemba (CFP) Sada Juma Segeja, anasema wanafanya mambo mbali mbali kuhakikisha wanawake wanapiga hatua.

Anasema, moja ya jambo ambalo wanalifanya katika shehia nne wanazotekeleza mradi wa kilimo msitu, ni kuwapa mafunzo ya biashara, ili wawe huru kiuchumi.

Alizitaja shehia hizo kuwa ni Mchangamdogo, Kambini kichokochwe, Chwale na Kiuyu Minungwini.

Anasema, pia wanawapatia mbegu bora na miche ya kisasa, huku wakiunda vikundi vya wanawake vya msaada wa pamoja na biashara.

 TAKWIMU

Kwa mujibu wa utafiti wa CFP wa mwaka 2022 unaonesha kuwa, zaidi ya wanawake 2,500 Pemba wameshiriki katika kilimo msitu.

Ikiwa ni asilimia 60 ya wanawake hao wameripoti kipato cha kaya kuongezeka mara mbili ndani ya miaka mitatu, jambo ambalo ni furaha kwao.

Inaeleza kuwa, zaidi ya miti milioni mbili imepandwa kupitia kwa vitalu vya kijamii.

KILIMO MSITU NA MAPAMBANO DHIDI YA TABIANCHI

Kila shamba linapandwa miti 100-200, inayosaidia kufyonza gesi ukaa na kulinda vyanzo vya maji.

Kwa mujibu wa Shirika la Chakula Duniani (FAO) limeeleza, kilimo msitu kina uwezo wa kupunguza uzalishaji wa gesi chafu kwa asilimia 20, katika vijiji vya Pemba ndani ya miaka kumi ijayo.

MAFANIKIO YA KIMATAIFA

Katika nchi ya Kenya wanawake wa Machakos wamepunguza ukame kwa kupanda miti kupitia kilimo msitu.

Ambapo kwa upande wa Uganda nako wanawake wa kijiji cha Mbale wamepanda zaidi ya miti milioni moja, wakiboresha kipato na mazingira yao.

NINI KIFANYIKE

Mafanikio ya Bishamba yanaonesha kuwa mwanamke akipewa nafasi na msaada sahihi, anaweza kuvuka mipaka ya mazoea na kuwa sauti ya mabadiliko.

Hivyo ipo haja kwa Taasisi na Mashirika mbali mbali kuwasaidia wanawake, wawe na maendeleo bora ndani ya jamii.

                                            MWISHO.  

 

 

 

 

  

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 


Comments

Popular posts from this blog

HIVI NDIVYO UTELEKEZWAJI WA WATOTO UNAVYOATHIRI MALEZI, MAKUZI YAO

‘’KATIBU MKUU ELIMU ‘’TOENI ELIMU YA MALEZI BORA’’

UROHO WA MALI KWA WANAUME UNAVYONYIMA WANAWAKE ARDHI