Unyanyapaa ulimsukuma Maryam kujifungulia nyumbani
Ilikuwa chanzo kumuambukiza mtoto wake VVU
Sasa anao watutu wakiwa salama, kama alivyo muume wake
NA FATMA HAMAD, PEMBA
MIMBA yangu ya kwanza nilijifungulia nyumbani kwani nilikua nanyayapaliwa, na ndio chanzo cha kumuambukiza mtoto wangu VIRUSI vya Ukimwi.
Hayo ni maneno ya Maryam Said mkaazi wa Chake chake mwenye umri wa miaka 38 ambae anaishi na virusi vya ukimwi kwa muda wa miaka 18 sasa.
Anasema alimuambukiza mtoto wake wa mwanzo mambukizi ya virusi vya UKIMWI
Mimba yake ya kwanza, alijifungulia nyumbani, kwa hofu ya kwenda Hospital kwa kuogopa kunyanyapaliwa.
‘’Hadi leo najilaumu, na najutia nafsi yangu, kwa kitendo cha kutokimbilia hospitali kwa ajili ya kwenda kujifungua nikidhani kwamba nyumbani ni salama,’’anasimulia.
Kwa sasa ameshajifungua watoto wengine watatu, ambao wako salama hawana maambukizo ya VVU , baada ya kusikiliza na kutekeleza kwa vitendo ushauri wa watalamu wa afya.
aligundulika na Virusi Vinavyosababisha UKIMWI ( VVU) mnamo tarehe 5/7/2005, wakati alipokwenda Cliniki ya ujauzito, na hapo alianza kupewa ushauri na kuanzishwa kutumia dawa za kupunguza makali ya VVU ( ARV).
Anaeleza baada ya kupata majibu hayo alishikwa na simanzi na huzuni, na hakuweza kutumia dawa hizo, kwani akitaka nyumbani kwao wasijue mtihani huo uliomtokezea.
Na ndio mana ikapelekea mtoto wake huyo wa mwanzo kumuambukiza, kwani hakuwa akitumia dawa za ARV.
‘’Sikufuata ushauri wowote wa daktari nilibakia tu nyumbani kwani nilikua na hofu, ili nisije nikagundulika kama nina VVU,’anasema.
Anasimulia kwamba takriban miaka 18 iliyopita , vitendo vya kuwatenga watu wanaoishi na VVU vilikuwa ni vingi sana.
“Watu wenye maambukizo ya VVU hawakujitokeza hadharani wala kufuata huduma za afya, kila mtu aliogopa kusemwa, ‘’ anasimulia.
CHANGAMOTO AliZOZIPATA BAADA YA KUGUNDULIKA NA VIRUSI VYA UKIMWI.
Baada ya wazazi waeke walipogundua kama ana VVU walimtenga na kumnyanyapaa.
‘Nilipata shida sana kwani nilinyanyapaliwa kutoka kwenye familia yangu hadi kwa majirani, sikuwa na mtu hata mmoja ambae alikua ananipa msaada wowote, ‘’ anaeleza.
Alikua anaishi kwa mateso na dhiki, ilipofika siku ya kujifungua, alijifungulia nyumbani kwao hakuenda Hospitali, kwani hakupata mtu wa kumshughulikia na kumpeleka, na pia alikua ana hofu ya kwenda kunyanyapaliwa.
‘’Nilijifungulia nyumbani kwani sikupata msaada wa mtu wa kunishughulikia na kunipeleka Hospitali, na hapo ndipo nilipomuambukiza mtoto wangu virusi, kwa vile hakupata huduma za kitalamu,’’anasimulia Maryam.
Anasema kitendo hicho cha kumsababishia mtoto wake kupata maambukizi kinamtia huzuni na hatokisahau, na hatoacha kujilaumu maishani mwake.
Wakati akiwa na umri wa miezi miwili, mtoto wake huyo aliumwa na homa na kumpeleka Hospitali, baada ya kupimwa nayeye akagundulika tayari ana VVU.
Hapo alipatwa na uchungu na akahisi kuwa hana tena faida yoyote ya kukaa tena katika dunia.
‘’Sikufichi nilipofika nyumbani nilichukua dawa ya Panya ili nijiuwe, nikataka kuanza kumpa mwanangu ila roho ya uzazi ikanijia, pamoja na rehma za Mungu, sikuweza ile chupa ika anguka chini na dawa ikamwagika.
Baada ya hapo alimchukua mtoto wake na kwenda kwa msamaria mwema kwenda kuomba msaada, ili amuhifadhi kutokana na shida alizonazo.
‘‘Yule mtu alichonisaidia alinichukua na kuniunga katika Jumuiya ya watu wanaoishi na Virusi vya UKIMWI ( ZAPHA+) , ambapo hadi sasa nimekuwa Mwenyekiti wa jumuia hiyo katika wilaya ya Chake chake na hapo ndipo nikaanza kupata elimu na hadi sasa nimekua mshauri mzuri’’.
Maryam kwa sasa ameolewa na mume mwengine ambae hana maambukizi ya VIRUSI vya Ukimwi, ambapo amezaa watoto wengine watatu, na wote wako salama.
‘’Nashukuru sahivi nimeolewa na mume ambae hana mambukizi, yuko salama, kwa vile tunafuata ushauri wa daktari,’anasema.
Anasema jamii isiwanyanyapae watu wanaoishi na VVU, pia wasivunje ndoa au familia, endapo mmoja kati ya mwanandoa atagundulika na virusi, kwani wanaweza kuishi bila kuambukizana.
Utafiti uliofanywa wa kuangalia matendo ya unyanyapaa katika jamii ( Stigma index) uliofanywa na taasisi ya ZAPHA+ mwaka 2019, ulibaini kwamba vitendo vya unyanyapaa bado vipo.
Utafiti umeonyesha bado vitendo hivi vipo katika jamii,kwenye familia, sehemu ya kutolea huduma kwa watu wanaoishi na VVU na mikusanyiko ya jamii.
Pengine kwa Mariam kama visinge kuwepo vitendo vya unyanyapaa kwa watu wanaoishi na VVU kwenye familia, angaliweza kuzuia maambukizo ya VVU ya siende kwa mtoto wake.
‘’Kwa sasa vitendo hivi vimepungua na watu wanapatiwa huduma ,lakini miaka 18 iliyopita haikuwa rahisi kwangu kujitokeza hadharani,’’anasema.
HUDUMA YA KUZUIA MAAMBUKIZO YA VVU KUTOKA KWA MAMA KWENDA KWA WATOTO
Serikali imeanzisha huduma hii kwa ajili ya mama wenye maambukizi ya VVU, wapate huduma na waondoe uwezekano wa kumuambukiza mtoto, wakati wa kujifungua ama kunyonyesha.
Kutoka na taarifa huduma hii kwa sasa ina ufanisi wa matokeo ya zaidi ya asilimia 90 ya kuwalinda watoto wasipate maambukizi.
Mratibu wa Tume ya UKIMWI Pemba, Ali Mbarouk Omar, anasema kwa sasa huduma ya kuzuia maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto, ina ufanisi mkubwa.
‘’Wastani wa mfano wa watoto 100, waliozaliwa na mama wenye maambukizo ya VVU basi 95 kati yao kwa upande wa Zanzibar wanaweza kuzaliwa salama.
Haya ni mafanikio makubwa ya kuzuia maambukizo kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto, ‘’ anasema
FAMILIA YA MARYAM
Hamad Omar Ali (siojina lake halisi) ni kaka wa Maryam alikubali kwamba, kabla hawajapata elimu kuhusu masuala ya UKIMWI, walimtenga na kumsusa ndugu yao huyo.
‘’Ni kweli kwamba mwanzoni kabla hatujapata elimu tulimtenga, hatukilanae, hatukimshirikisha kwa lolote la kifamila,anaeleza.
Anasema kwasasa wamekua nae bega kwa bega amekua msaada mkubwa katika familia yake na hata kwa jirani zao.
JIRANI YAKE
Maryam Salum mkaazi wa Mabaoni Chake chake, ambae pia nayeye anaeishi na VVU anasema kiukweli Maryam Said baada tu familia yake ilipogundua kwamba ana VVU ilimtelekeza.
‘’Maryam alikua akiishi kwa shida na mateso, ambapo hata sisi jirani zake, tulikua tunamuonea huruma.
Anasema anadhani kwamba hali hiyo ilikua ikifanyika kwa kutokana na jamii kwamba, ilikua haijaelimishwa, juu ya masuala hayo, kwani ilikua hayajajulikana kama hivi sasa.
Anaeleza yeye alipogundulika kwamba anaugonjwa wa Ukimwi ilikua tayari wameshakupata elimu hakukumbana na vikwazo kihivyo.
Jirani mwengine ni (Omar ambae sio jina lake halisi) anakiri kwamba maryam mwanzo alipogundulika na Viruzi vya UKIMWI, alikua akiishi kwenye mashaka, kwani familia yake na hata majirani wote walimsusia.
‘’Ijapokua alikua ni mtu hodarai kwa wenzake, lakini hatukuliona hilo sote tulimtenga, na hiyo ni kutokana na kwamba elimu juu ya masuala ya ukimwi ilikua bado hayajakuwepo,’’anaeleza.
MUME WAKE
Sabri Issa anasema ni kweli amemuoa mke wake huyo ambae anaishi na VIRUSI vya Ukimwi, ambapo tayari wameshapata watoto watatu na wakiwa salama.
Anasema wanaume wasiwakatae wanawake ambao wanaishi na VVU, kwani endapo watafuata ushauri wa wataalamu wa afya, wanaweza kuishi kwa furaha na amani na bila ya kuambukizana.
‘’Nimemuoa Maryam akiwa na maambukizi na tumeshazaa watoto watatu na wala hatuna maambukizi tuko salama,’’anaeleza.
Anasema amekua akiangalia afya kila baada ya miezi mitatu, na kwa mara ya mwisho alikwenda mwezi wa nne mwaka huu.
Pia anaeleza kwamba amekua akitumia dawa kinga zinazoitwa PREEP, ambazo hutumika kwa mtu ambae hana mambukizi, ambao wako katika hali rizki.
MTAALAMU WA AFYA
Dokta Rahila Salum Omar ambae ni msimamizi wa vituo vya kutoa huduma kwa watu wenye ‘VVU’ anasema, kiutalamu ni kweli mtu mwenye Virusi vya UKIMWI anaweza kuoa au kuolewa na ambae hana virusi, na wakaishi salama wao na kizazi chao.
Anasema sio vizuri watu kuvunja familia zao wala ndoa zao ikitokezea mmoja, wanaotaka kuoana, kwa sababu mmoja wao amegundulika na mambukizi, na kuvunjika.
‘’Kiutaalamu ni kweli kwamba mtu mwenye VVU anaweza kuoa au kuolewa na alie kua hana na wala wasiambukizane na maisha kuendelea, kama alivyo Maryam’’,anaweka wazi.
Mkakati wa kimataifa wa shirika la Afya dunia (WHO) wa VVU, (2022 hadi mwaka 2030), imelenga kutokomeza ukimwi ifikapo 2030.
Zanzibar inatekeleza mkakati huo kwa kuitika mwito wa kimkakati wa 95 tatu ifikapo 2030. Mkakati huu unalenga juhudi za mapambano za kuifikia dhamira hii ifikapo 2030.
Asilimia 95 ya wazanzibari ifikapo 2030 wanatambua afya zao ( wanaishi ama hawaishi na maambukizo ya VVU, asilimia 95 ya wanaoishi na VVU wawe wanatumia dawa za kupunguza makali ya VVU ifikapo 2030.
Na asilimia 95 ya wanaotumia dawa za kupunguza makali ya VVU virusi viwe vimefubazwa ( Havina madhara ya kuambukiza sana, kusababisha magonjwa nyemelezi ,ama kuongeza kinga ya mwili ).
Tanzania inadhamira ya dhati ya kukomesha janga la VVU iliyowekwa katika ngazi ya kimataifa ndani ya mfumo wa malengo endelevu ya maendeleo (SDGs).
Kwa mujibu wa Tathmini iliyofanyika Dicemba 1 2023, Takwimu nchini Kenya zinaonesha nchi hiyo inashika nafasi ya saba kwenye orodha ya mataifa yenye idadi kubwa ya maambukizi ya virusi vya UKIMWI duniani, huku Rwanda na Tanzania zikitaja kufanikia kudhibiti maambukizo.
MWISHO
.jpg)
Comments
Post a Comment