KERO YA MAJI, TATIZO KWA WANAKIJIJI CHA GOMBEUME

 



                      NA  FATMA HAMAD- PEMBA

WANANCHI WA KIJIJI cha Gombeume Shehia ya Mchangamdogo   Wilaya  ya  Wete  Mkoa wa Kaskazini  Pemba,  wamelalamikia  juu  ya  ukosefu  wa  huduma  ya  Maji  safi  na  salama   kijijini hapo.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi huko kijijini kwao Gombeume mwananchi Bishamba Suleiman Ali na  Fatma Said Haji wamesema huu ni zaidi ya mwaka wa tatu hawapati huduma ya maji katika kijiji chao.

Walisema wamechoka na kadhiya hiyo ambayo inawafanya waende  mabondeni  kufuata huduma ya maji,  kwa  ajili  ya  matumizi  ya  majumbani  mwao.

‘’Kwakweli tuna shida kubwa wananchi wa gombeume, tunakwenda mabondeni kwenye visima vya zamani kuchota maji,  tunaumia na tumechoshwa na shida hiyo,’’walisema.

Walisema wanahofu ya kujakupata  maradhi ya mripuko, kutokana  na kukosa maji ya kutosha ya kufanyia usafi kwenye vyovyao ambavyo wanatumia majumbani mwao  pamoja na misikitini.

‘’Tunashindwa kupata hata maji ya kufanyia usafi majumbani mwetu, mungu tu mwenyewe atulinde na maradhi,’’walisema.

Kwa upande wake  Bi Mtumwa Makame alisema tatizo la maji limekua kubwa na limekua kero, kwani hata wanapopatwa na msiba wanakuwa na hofu ya kupata maji na kuweza kumsitiri mwenzao.

‘’Ni juzi tu alikufa  jiraji nyumba hile pale, ili tubidi tuende mabondeni kubeba maji ya kuja kumsitiri mwenzetu, jee hiyo ni hali kweli,’’alieleza.

Nae mwananchi Bakar Khamis Bakar  alisema kuwa Tatizo  limekua kubwa,  jambo  linalopelekea  wanawake  wa  kijiji hicho  kukosa  kufanya  shughuli  za  uzalishaji,  kwani hupoteza muda mwingi wakiwa visimani,  kwa ajili ya kutafuta  maji.

‘’Tokea kutakapokucha  wanawake wa kijiji hichi  wao ni kuhangaika mabondeni tu na ndoo za maji,  hawapati  kufanya shughulinyengine  yeyote  ya  kujingizia  kipato, tunahitaji kuwangaliwa na kufanyiwa msaada tunaumia,’’alisema.


Afisa wa Mamlaka ya Maji Safi na Salama  Zanzibar (ZAWA ) kisiwani  Pemba  Suleiman  Anass  Masoud  alikiri kuepo kwa tatizo hilo  kijijini hapo.

Alisema  kwa sasa tayari wameshapeleka mashine katika kisima kilichopo kijiji cha kibomani, ambacho kitasambaza maji maeneo yote ya mchangamdogo, na Gombeume.

Hivyo amewataka wananchi kuwa na uvumilivu kwani mafundi wako kwenye matengenezo, ya miundombinu, ili kuona wananchi hao  wanaondokana na kadhya hiyo.

Aidha  Afisa huyo alisema kwa maeneyo  mengi  ambayo yamekua yakikosa maji kutokana na ujenzi wa barabara,  sio tatizo la Mamlaka ya Maji, kwani wao hutoa maelekezo ili kuona  wananchi hawathiriki kwa ajili ya ujenzi huo.

‘’Kwa maeneo yote ambayo wananchi hawapati maji kwa kutokana na ujenzi wa barabara, sisi sio jukumu letu zawa, sisi tunawaeleza vya kutosha watakapojenga wasikate miundombinu ya maji, kwani itakua ni usumbufu kwa wanachi,’’alieleza.






Comments

Popular posts from this blog

HIVI NDIVYO UTELEKEZWAJI WA WATOTO UNAVYOATHIRI MALEZI, MAKUZI YAO

DNA YA THIBITISHA, MTUHUMIWA NDIE BABA MZAZA WA MTOTO