Kilimo msitu tarajio la kuwakomboa wanawake kiuchumi


 







                          Na Fatma Hamad –Pemba

MATARAJIO yangu katika ukulima huu wa  kilimo msitu ni  kujiinua kiuchumi,’’ anasema mnufaika wa mradi wa mabadiliko tabia nchi Asya Abeid Said wa shehia ya Mjini kiuyu wilaya ya Wete Kaskazini Pemba.

Anasema lengo hasa la  kujikita katika kilimo msitu ni kulima mazao ambayo yatamsaidia kujipatia  kipato na kuondokana na umasikini, sambamba na kujikinga na athari zitokanazo na mabadiliko tabianchi.

Kumbe unapolima kilimo msitu unaweza kuvuna mazao ya chakula,  biashara, sambamba na kuifanya ardhi kuwa na rutba wakati wote.

‘’Nitalima  mazao nitauza, na mingine yatanisaidia kapata chakula cha nyumbani na familia,’’anasema.

Hapa matarajio yake ni kulima mazao mengi ya biashara, ili aweze kupata fedha kwa ajili ya kusomeshea watoto wake na kujikimu yale mahitaji ya lazima.

‘’Binafsi nilikwenda kwenye mafunzo Tanazania bara, nikamshuhudia mwanamke kama mimi, amenunua gari kwa kupitia shughuli zake za kilimo msitu, hivyo na mimi nia yangu nataka niwasomeshe watoto wangu,’’anasimulia.


Hidaya Khatib Hamad  mkulima wa kilimo msitu kutoka Mchangamdogo, anasema kilimo msitu kinaweza kumkomboa mwanamke kiuchumi, kwani anaweza kuvuna mazao tofauti, pia  kujiepusha na athari za mazingira.

‘’Unaweza ukavuna Mdalasini ukauza, ukavuna Ndizi ukapata chakula, na pia kupata elimu ya utunzaji wa mazingira,’’ anasema Hidaya.

Anajikita kwenye kilimo mseto ili aweze kujitegemea mwenyewe kimaisha,  na kuepuka kukata miti kiholela hapo baadae kama akihitaji kuni za kupikia.

 ‘’Unapokua na miti yako shambani utapata kuni, utaepukana na usumbufu wa  kwenda masafa ya mbali na kuepusha  uchafuzi wa mazingira,’’ anasema.

Kombo Khatib Bakar mkulima kilimo msitu shehia ya Mjini kiuyu Wilaya ya Wete, anakiri  kwamba kilimo hicho kitawainua wanawake kiuchumi.

Wanapolima kilimo hicho mchanganyiko watapata mazao kwa ajili ya kuuza na pia watapata chakula kwa kipindi karibu miezi 12 ya mwaka.

‘’Watakapolima mazao kama Mananasi, Maparachichi wanaweza kuuza na kjipatia pesa, na wakilima mchicha unaweza kuwasaidia majumbani kwao,’’anafafanua.

Aisha Khamis mwananchi kutoka Mchangamdogo anasema kilimo msitu kitawafanya wanawake kupiga hatua kiuchumi, kwani wanalima mazao tofauti yakiwemo ya biashara na chakula.

‘’ Tunapolima kilimo hichi tutapata mazao kwa ajili ya chakula, tutapata pesa na pia tutaifanya ardhi kuwa na rutba nzuri na kuweza kunawiri vizuri mazao,’’anaeleza.

Fatma Saleh Faki mkulima wa kilimo msitu kutoka shehia ya Mjini kiuyu anasema lengo lake hasa la  kujikita  kwenye  kilimo hicho, ni kulima mazao kwa ajili ya biashara.

‘’Mimi nataka nipande zaidi Mikungu, Mivinje, Minazi, ili nije nipate pesa nimalizie jingo langu,’’anasema.

Anasema unapolima miti kama hiyo ya misitu huifanya Ardhi kuwa na rutba, lakini pia hupelekea mvua kunyesha kwa wingi.

VIONGOZI WA SERIKALI

Afisa  mdhamini wizara ya  kilimo  Umwagiliaji  Maliasili  na Mifugo  Injinia Idris  Hassan Abdulla anasema kilimo msitu kitawapa faida wanawake, kwani kitaifanya ardhi kuwa na rutba na kupatikana mazao kwa wingi.

‘’Unapolima kilimo mchanganyiko kutasaidia kupatikana kwa mvua, na kusaidia kupatikana kwa mazao kwa wingi,’’anaeleza.

Anasema kama wizara wamekua wakitoa elimu kwa vikundi mbalimbali ya utunzaji mazingira, ili kuona wanawake wanapiga hatua kupitia kilimo msitu.


Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba  Salama Mbrouk Khatib anasema, kilimo msitu kitawainua kwa kiasi kikubwa wanawake kiuchumi, kwani watapata mazao ambayo yatawasaidia katika familia zao.

‘’ Ukilima tembere utapata mboga, ukipanda miembe utavuna embe utauza utapata pesa za kununua mahitaji mengine ya nyumbani,’’anafahamisha.

 WANAHARAKATI

Juma Bakar Alawi mdau wa masuala ya mazingir, ambae pia aliwahi kushika nafasi mbalimbali za uongozi katika idara ya mazingira, anasema  wanawake ndio wathirika wakubwa wa athari za mabadiliko ya tabianchi.

Anasema kupitia mradi huo wa uhifadhi mazingira utawasaidia wanawake kujikwamua na umasikini.

‘’Kwakweli jambo wanalolifanya  Jumuia ya upandaji misitu Pemba CFP,  na  upandi  mistu  kimataifa   CFI  la  kuleta mradi huu wa mabadiliko ya tabianchi ni jambo jema, kwani wanawake watajipatia mahitaji ikiwemo kuni, na pesa za kujikimu kimaisha,’’anasema.

Rehema  Abrahman  Alawi  ni  Afisa  misitu kutoka Jumuia  ya upandaji  misitu  Pemba  CFP  anasema  mradi  wao  umelenga zaidi  kwa  wanawake  kwani  wao  ndio  waathirika  wakubwa wa  mabadiliko  ya  tabianchi.

Anasema  wamekuwa  wakiwapatia  elimu  pamoja  na  miche ya miti mbalimbali  wanawake, waweze kulima kilimo msitu kwa ajili ya kujiinua kiuchumi, pamoja na kuepusha kutokea kwa mmon’gonyoko wa ardhi.

‘’Unapomwambia mama apande  miti ya misitu katika shamba lake, atajipatia  mahitaji  muhimu kama vile kuni, miti ya kujengea, na kufahamu athari zitokanazo na mabadiliko ya tabianchi.

Omar Hamad Mjaka katibu wa Jumuia ya ufugaji wa Kuku kisiwani Pemba,  anasema kilimo msitu kitawasaidia wanawake kujikomboa na umasikini.

Wanapolima mazao mchanganyiko katika mashamba yao, watapata chakula,  pesa,  pamoja na kupata hewa safi.

‘’Kwakweli kilimo msitu kitawafanya wanawake wapige hatua, kwani watavuna mazao kwa ajili ya  chakula, biashara, pamoja na kufahamu umuhimu wa kutunza mazingira,’’anafafanua.

ATHARI.

Kisiwa cha Pemba ni moja ya visiwa ambavyo vimekua ni muhanga mkubwa wa masuala ya mabadiliko ya tabianchi, na kwa mujibu wa Afisa  Elimu kutoka Idara ya Mazingira Ofisi ya Pemba Nassor Ali Salim, anasema endapo kama, hakutochukuliwa hatua za makusudi za kukabiliana na athari zinazotokana na  Mabadiliko ya Tabianchi, baada ya miaka 100 kisiwa cha Pemba kitabakia historia, kutokana na maji ya bahari kuingia Nchi kavu.

Anasema kufuatia tatizo hilo la Majichumvi kuingia katika Nchikavu,  kunauwezekano mkubwa wa kupoteza Kilomita za mraba 286, sawa na asilimia 28 ya eneo lote la Pemba.

Anasema watu wanaongezeka na Ardhi inaendelea kupungua, hivyo  kama hakutochukuliwa jitihada za ziada, juu ya kupambana na athari za mabadiliko ya tabianchi, kisiwa cha Pemba kitakua kiko hatarini zaidi, na watu wanaweza kuja kukosa maeneo ya kuishi.

Anasema yapo maeneo yasiyopungua  123 yakiwemo  makaazi ya watu pamoja na mashamba yanayotumika kwa ajili ya kilimo, yameathirika kutokana na uingiaji wa majichumvi.

‘’Tuna maeneo mengi yameathiwa na mabadiliko ya Tabianchi kama vile Kojani, Mjini kiuyu, Mkoani pamoja na Micheweni na hayawezi kutumika kwa sasa,’’anasema. 

Anasema ni jambo la kushukuriwa kwa Jumuia ya uhifadhi wa misitu Pemba ‘CFP’ na wenzao wa kimataifa ‘CFI’ kwa ushirikiano wa karibu na TAMWA Zanzibar kwa kuamua kuleta mradi huu wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kwa wanawake, kwani wao ndo hasaa waaathirika zaidi wa janga hilo.

Mkurugenzi  wa  Jumuia  ya  upandaji   misitu  Pemba  CFP Mbarouk  Mussa  Omar  anasema  kama  hakutochukuliwa jitihada zozote,  juu  ya  mabadiliko  ya  tabianchi, itakuja kusababisha baadhi ya vijiji kuhamwa kutokana na maji ya bahari kupanda kwenye majumba.

‘’Katika kijiji cha Mjini kiuyu kila ifikapo mwezi 13,14, na 15 maji ya chumvi yanaigia ndani ya majumba,’’anasema.




NINI KIFANYIKE

 Ili kukilinda kisiwa cha Pemba na athari za mabadiliko tabianchi niwakati kila mmoja  kuchukua jitihada za utunzaji wa mazingira ikiwemo kulima kilimo msitu ambacho kinajumuisha miti ya muda mrefu na ya muda mfupi sambamba na miti kuacha tabia ya kukata miti kiholela.

  Nairat  Abdulla  Ali  Afisa  kutoka  Chama  cha wandishi  wa  habari  wanawake TAMWA   Zanzibar  anashauri.

Hili ni jambo jema, kwa jamii na wanaouendesha mradi huo ambao ni Jumuia ya uhifadhi wa misitu Pemba ‘CFP’ wakishirikiana na wenzao wa kimataifa ‘CFI’ kwa ushirikiano wa karibu na TAMWA Zanzibar.

 Mradi  ambao  umefadhiliwa  na  Serikali  ya  Canada na kuridhiwa na serikali ya Mapinduzi,  kuona  wanawake wamepiga  hatua katika suala la kukabiliana na mabadiliko tabianchi.

Kwani lengo hasa la  mradi  ni  kuwainua  wanawake kiuchumi,  kupitia  mradi  huo  wa  uhifadhi  wa mazingira.

Uchanganuzi wa Hali Mwaka wa 2023

Uchanganuzi wa Hali Mwaka 2023 inaonyesha kuwa idadi ya watu  wanaoenda  Mahakamani  kukabiliana  na  janga la mabadiliko  ya  taianchi  inaongezeka. 

 Kufikia  Desemba  mwaka   2022,  kumekuwa  na  kesi 2,180  zinazohusiana  na  mazingira,  zilizowasilishwa kwa  taasisi  za  sheria  65  kote duniani:

Ripoti  ya  Benki  ya  Dunia  inasisitiza  umuhimu wa  kuunganisha  masuala  ya  tabianchi  katika mipango  ya  maendeleo  ya  Tanzania  kupitia  Dira  ya  Taifa  ya  Maendeleo  2050

Ambapo moja ya mkakati wa ripoti hiyo ni kusaidia  jamii zilizohatarini,  kuwa  na  uwezo  wa  kuhimili  mishituko ya  tabianchi.

Pia  ripoti  hiyo  imeeleza  kuwa kushindwa  kuchukuliwa hatua  za  mabadiliko  ya  tabianchi,  kunaweza  kupunguza  ukuaji  wa  uchumi wa Tanzania, kwa asilimia  nne  ifikapo  mwaka  2050.

Aidha  kunaweza  kusababisha  watu  Miliono  2.6  kuingia  kwenye  umasikini,  na  wengine  Milioni 13 kulazimika  kuhama  makazi  yao  Nchini. 




 

 

Comments

Popular posts from this blog

KERO YA MAJI, TATIZO KWA WANAKIJIJI CHA GOMBEUME

HIVI NDIVYO UTELEKEZWAJI WA WATOTO UNAVYOATHIRI MALEZI, MAKUZI YAO

DNA YA THIBITISHA, MTUHUMIWA NDIE BABA MZAZA WA MTOTO