Ni ipi nafasi ya familia katika kuwashajiisha watoto wa kike kushiriki michezo.

Na, Fatma Hamad




NA FATMA HAMAD, PEMBA

Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, kupitia idara yake ya michezo, imekuwa ikitoa fursa mbali mbali za kimaendeleo ikiwemo ajira, kushiriki mabonanza nje ya Zanzibar.

Hilo limekuja kwa wazazi kutokuwapa nafasi watoto wa kike kushiriki michezo, kwani bado wanahisi kwa mwanamke ni uhuni na kupelekea siku zote kubaki nyuma kimichezo.

Licha ya Serikali kutoa fursa nyingi za kimaendeleo, bado ushiriki wa wanawake na watoto wa kike, ni mdogo ukilinganisha na wanaume hapa visiwani Zanzibar, hususan kisiwa cha Pemba.

Wazazi na walezi wanayo kila sababu ya kuhakikisha wanawapa nafasi (fursa) watoto wa kike, kushiriki kwenye michezo ili kuona nawao wanajinyakulia fursa zilizomo kwenye Sekta ya michezo.

Kwani wapo wengi wamekuwa ni wachezaji wazuri wakati wanapokuwepo skuli, wanapomaliza vipaji hivyo hupotea.

Makala hii itangazia nafasi ya wanajamii (familia ) katika kuwashajiisha watoto wa kike, kushiriki ipasavyo kwenye michezo.

WATOTO

Mtoto Fatma Mkubwa mwenye umri wa miaka 15 mkaazi wa Mkoani anasema, wazazi wawaruhusu watoto wa kike kushiriki michezo, kwani nawao wanatamani kufika mbali.

‘’Nasisi watoto wa kike tunauwezo wa kucheza na tukaweza kufanya vizuri, hivyo wazazi musituzuie na tunataka kukuza vipaji vyetu,’’anasema.

Anasema anacheza mpira wa mikono katika timu ya watoto wenye ulemavu na ndoto yake siku moja ni kuona amefika nchi za Ulaya, kwa ajili ya michezo.

Aisha Ali mwenye umri wa mika 17 mkazi wa Sizini anasema, anapenda riadha pamoja na mpira wa miguu, ingawa aliishia kucheza tangu akiwa anasoma, familia yake  haimruhusu tena kwani anaonekana akiendelea atahunika.

‘’Natamani siku moja nije niwe mwanamichezo marufu duniani, ila kipaji changu kinadumaa si kupata kuendelezwa,’’anasema.

JAMII.

Kulthum Faki wa Konde, anasema wazazi wawaruhusu watoto wao wa kike kujiunga kwenye michezo kwani, michezo ni moja njia inayopelekea kujipatia ajira.

‘Tumekua tukishuhudia vijana wengi wakipata ajira kama vile vikosi, hivyo wazazi msiwazuie watoto wa kike kujiunga na michezo, na wao wanayo haki ya kupata hizo ajira,’’anaeleza.

Khatib Iddi Mwalimu mkazi wa Mkoroshoni Chake chake, anasema michezo huimarisha afya, hivyo ni vyema  wazazi  kutoa fursa kwa watoto wao wa kike kujiunga na michezo, ili kuwakinga na maradhi na kuwa wakakamavu ambapo itawasaidia kufanya vizuri kwenye masomo yao.

‘’Wazazi wapeni nafasi watoto wa kike wajiunga kwenye michezo, kwani kutawasaidia kuwa na afya njema,’’anaeleza.

Juma Kombo Hija mkaazi wa Chamboni Micheweni amewataka wazazi na walezi kuwa na hamasa ya kuwashajiisha watoto wa kike kushiriki kwenye michezo ili, nawao wajione kama ni sehemu ya jamii ambayo inahitaji kupata maendeleo.

VIONGOZI WA SERIKALI

Afisa Mdhamini wizara ya Habari, Vijana Utamaduni na Michezo Mfamau Lali Mfamau anasema, bado wananchi hususani Pemba, hawajakuwa na mwamko juu ya la michezo kwa mtoto wa kike, kwani wanahisi ni kitendo kinachokwenda kinyume na madili.

‘’Tukiangalia vipaji tunavyo mitaani vya michezo kwa watoto wa kike, ila wazazi hawawaruhusu,’’anaeleza.

Anasema idara ya michezo imekuwa ikitoa fursa nyingi kupitia michezo, hivyo ni wakati kwa wanajamii kuwamka na kuwashirikisha watoto wao wa kike kwenye michezo, ili nawao wafaidike na fursa hizo.

Khamis Hamad Juma Naibu Katibu mkuu wa Shirikisho la mpira wa Miguu Zanzibar (ZFF) Ofisi ya Pemba, anasema ipo haja kwa serikali, pamoja na wadau wa michezo, kuwaelimisha wazazi juu ya  umuhimu wa michezo.

Ansema ili wawaruhusu watoto wao wa  kike kwenye michezo, kwani siku moja inaweza kuja kuwa mkombozi wa maisha yao.

WANAHARAKATI

Fat -hiya Mussa Said anasema bado wazazi wanahitaji kupewa elimu, ili waweze kufahamu umuhimu wa michezo kwa mtoto wa kike, waweze kuwaunga mkono.

Anasema kutokana na itikadi potofu zinazojengeka kwa jamii, kwamba michezo kwa mwanamke  ni uhuni, wanashindwa kuwapa nafasi watoto wao wenye vipaji vya michezo.

‘’Utakuta watoto wa kike wengi wanaishia kucheza michezo wakiwa skuli tu, wakimaliza vipaji hivyo hufa, kwa sababu imejengeka michezo ni kwa wanaume tu,’’anaeleza.

Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 kifungu cha 12 (1) kinafafanua kuwa, watu wote ni sawa mbele ya sheria, na wanayo haki bila ya ubaguzi wowote, kulindwa na kupata haki sawa.

 


Comments

Popular posts from this blog

HIVI NDIVYO UTELEKEZWAJI WA WATOTO UNAVYOATHIRI MALEZI, MAKUZI YAO

DNA YA THIBITISHA, MTUHUMIWA NDIE BABA MZAZA WA MTOTO

‘’KATIBU MKUU ELIMU ‘’TOENI ELIMU YA MALEZI BORA’’