UISLAMU NA UMILIKI WA ARDHI KWA MWANAMKE
Je, ni vipi uislamu unampa nafasi mwanamke kumiliki ardhi? NA FATMA HAMAD, PEMBA Kwa muda mrefu, kumekuwepo na dhana potofu katika baadhi ya jamii, hususan Zanzibar, kwamba mwanamke hana haki ya kumiliki ardhi. Dhana hii imejikita zaidi katika mila na tamaduni kuliko katika misingi ya dini ya Kiislamu. Viongozi wa dini na wanaharakati wa haki za wanawake wamekuwa mstari wa mbele kupinga mtazamo huo, wakisisitiza kuwa Uislamu unamtambua mwanamke kama mmiliki halali wa mali, ikiwemo ardhi. Ingawa viongozi wa dini ya kiislamu wanapinga mtazamo huo, wanaeleza kuwa mwanamke ana haki ya kurithi, kununua, na kutumia mali au ardhi kwa ridhaa yake mwenyewe. Kiongozi wa dini ya kiislamu kutoka kijiji cha Wingwi Njuguni kisiwani Pemba Juma Othman Nahoda anasema ‘’Urithi ni haki ya mwanamke, na si hisani’’ Anasema katika Suratul- Nisa, aya ya saba (7) ‘’wanaume wanafungu katika walichoachiwa na wazazi wao na wanawake pia wanafungu katika walichoachiwa, iwe kidogo au kikubwa, ni fungu l...