WANDISHI WA HABARI WATAKIWA KUEPUKA HABARI ZA UDANGANYIFU


NA FATMA HAMAD, PEMBA

WAANDISHI wa habari wametakiwa kufuata maadili wakati wanapotekeleza majukumu yao sambamba na kuandika habari zenye ukweli, zenye kulinda haki, heshima na utu wa binadamu, hasa katika kipinidi hiki cha kuelekea Uchaguzi mkuu wa Octoba mwakahuu.

Wito huo umetolewa na Kamishna wa Tume ya Haki za Binadamu Zanzibar Khatib Mwinchande wakati akifungua mafunzo ya siku moja kwa waandishi wa habari kuhusu, uzingatiwaji wa haki za Binadamu na Misingi ya Utawala bora katika mchakato wa Uchaguzi Mkuu wa 2025, yaliyofanyika kwenye Ukumbi wa Ofisi hiyo Chake Chake Kusini Pemba.

Alisema, ni vyema waandishi wa habari kufuata miiko na maadili yao wakati wanapotekeleza kazi zao, hasa katika kipindi hiki cha uchaguzi mkuu wa Octoba 2025.

Alifafanua, waandishi wa habari ni wadau muhimu wanaopaswa kuzingatia utekelezaji wa Sheria, kwani kufanya hivyo kutawasaidia kufanyakazi za ukweli, zenye kulinda haki na utu wa binadamu.

Alisema, suala la uchaguzi ni mchakato muhimu katika Nchi, inayozingatia Misingi ya Demokrasia, uhuru, haki na amani, hivyo ni wajibu kwa waandishi wa habari kuandika habari zenye ukweli na zenye kulinda haki za wananchi, ili kuona kwamba wanajitokeza kwa wingi katika haki yao ya kikatiba bila hofu.

‘’Waandishi wa habari andikeni habari zenye kuzingatia haki za binadamu na misingi ya utawala bora, hasa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu, ili wajitokeze kupiga kura na kuchagua viongozi wanaowataka,’’alisema.

Alisema, waandishi wa habari ni wadau muhimu wanaoweza kulinda haki za binadamu na amani ya Nchi, hivyo ni budi kuepuka kuandika habari zenye  kuleta migongano, jambo linaloweza kusababisha vurugu na kuondolewa kwa haki, utu na heshima za wanadamu.

Alisema, kwa kuzingatia Ibara ya 130 (1) (a) ya Katiba ya Jamuhuri ya Mungano wa Tanzania ya mwaka 1977, pamoja na kifungu cha 6 (1), (a), (b) vya Sheria ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora sura ya 391.

Na kifungu cha 8 cha Sheria nambari 12 ya mwaka 2003, Sheria za Zanzibar, Tume ya Haki za Binadamu inajukumu la kuhamasisha hifadhi za haki ya binadamu, wajibu wa jamii na kutoa elimu kwa umma juu ya haki za binadamu.

Alifahamisha, ili uchaguzi ufanyike kwa uhuru na amani ni lazima kuzingatiwa haki, misingi na heshima ya haki za binadamu, hivyo ni vyema waandishi wa habari kupatiwa elimu, ili kuhakikisha kwamba heshima za watu hazikiukwi kwa kisingizio cha uchaguzi.

Kwa upande wake Afisa Mfawidhi kutoka Tume ya Haki za Binadamu Ofisi ya Pemba Suleiman Salum Ahmad alisema, lengo la mafunzo hayo ni kuwakumbusha waandishi wa habari, kuwa waadilifu na wazalendo wa hali ya juu, ili kuibakisha nchi katika hali ya amani na utulivu kabla, wakati na baada ya uchaguzi.

‘’Katika kipindi cha uchaguzi kumekuwa kukijitokeza vitendo vingi ambavyo haviendani na maadili na misingi ya kibinadamu, hivyo waandishi tuweni makini, ili habari zetu ziwe ni zenye kulinda na kuheshimu silka na desturi za nchi yetu ili kuepusha maafa,’’ alifahamisha.

Akiwasilisha mada ya Haki na Wajibu wa Waandishi wa habari wakati wa uchaguzi, Mchunguzi Msaidizi Mwandamizi kutoka Tume hiyo Makaruru Nyarancha, alisema Tume ya Haki za Binadamu imekuja na mafunzo hayo ili kuona wanatoa habari za msingi, ambazo wananchi watapata kufahamu haki na wajibu wao.

Alisema, kwa mujibu wa mikataba ya kimataifa ya haki za kiraia na haki za kisiasa ya mwaka 1966 kifungu cha 25, kila raia ana haki ya kupiga kura na kuchaguliwa katika uchaguzi wa kweli, wa haki na wa mara kwa mara, uliofanywa kwa kura ya siri na kuhakikisha uhuru wa wapiga kura.

Kwa upande wake Mratibu wa Habari Maelezo Pemba Jamila Abdala Salim aliwataka wandishi wa habari kuyatumia mafunzo hayo, ili waandike habari zenye migogoro na zenye kuepusha kuvunjwa kwa haki za binadamu.

Nao waandishi waliopatiwa mafunzo hayo wameahidi kuyatumia vyema na kuhakikisha wanafuata miiko na maadili ya kazi yao, ili kuibakisha nchi katika hali yake amani kwa wakati wote wa uchaguzi na baada.

                                         

  

 

 

 

Comments

Popular posts from this blog

KERO YA MAJI, TATIZO KWA WANAKIJIJI CHA GOMBEUME

HIVI NDIVYO UTELEKEZWAJI WA WATOTO UNAVYOATHIRI MALEZI, MAKUZI YAO

DNA YA THIBITISHA, MTUHUMIWA NDIE BABA MZAZA WA MTOTO