Dk. Mwinyi ataka usafi kwenye miji uimarike


NA ZUHURA JUMA, PEMBA
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk Hussein Ali Mwinyi amezitaka Halmashauri, Mabaraza ya Miji na Manispaa kudumisha usafi katika miji, ili kuiweka katika mazingira bora na haiba ya kuvutia.

 kizungumza wakati akifungua kituo cha wajasiriamali Kifumbikai Wete pamoja na stendi ya Kinowe Konde Dk. Mwinyi aliziagiza taasisi hizo mambo matano, ikiwa ni pamoja na kufanya usafi katika miji, kujenga masoko, vituo vya ujasiriamali, maegesho na viwanja vya kufurahishia watoto ambayo hayo yatasaidia kuweka mazingira bora na mazuri.

 Alisema kuwa, usafi ni muhimu katika maisha ya mwanadamu, hivyo ni wajibu wao kudumisha katika maeneo ya miji, kwa ajili ya kuweka mandhari nzuri na ya kuvutia.

 "Tumebadilisha ugatuzi ili taasisi hizi ziweze kufanya kazi zake vizuri ikiwa ni pamoja na suala la kuimarisha usafi katika miji yetu, hivyo mna wajibu wa kuyatekeleza kwa vitendo ili kuimarisha maisha ya wananchi," alisema Rais Mwinyi.

 Aidha Dk. Mwinyi alieleza kuwa, kituo hicho cha wajasiriamali pamoja na stendi (maegesho) alizozifungua ni fursa muhimu ya kiuchumi kwa wananchi ambayo watafanya biashara katika maeneo hayo na kujipatia fedha zitakazowakwamua na maisha duni.

 "Wakati nafanya kampeni wajasiriamali walitaka wapatiwe mtaji, maeneo mazuri ya kufanya biashara zao na kodi nafuu, ambapo kwa miaka mitatu ya awamu ya nane tayari imeshatekeleza hayo kwa kiasi kikubwa, kwani jumla ya shilingi bilioni 31 zimetengwa kwa ajili ya kuwapatia mikopo wajasiriamali bila ya riba kupitia benki ya CRDB," alifafanua.

Dk. Mwinyi aliagiza Mamlaka husika kutowatoza kodi miezi mitatu kwa wajasiriamali ambao watakwenda kuuza bidhaa zao kwenye soko hilo, huku akisisitiza kupewa kipao mbele katika suala la kupatiwa mikopo, ili wajipatie mtaji utakaowasaidia katika shughuli zao za ujasiriamali.


Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa Kaskazini Pemba Salama Mbarouk Khatib alisema kuwa, Dk. Mwinyi amefanya mambo makubwa ambayo yataimarisha maisha ya wananchi na kupata maendeleo.

 "Tutayasimamia majengo haya na kudumisha usafi kwenye vituo, masoko na maeneo mengine ya miji ili wafaidike wao na vizazi vijavyo," alieleza Mkuu huyo.

 Nae Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalumu za SMS Massoud Ali Mohamed alisema kuwa, Dk. Mwinyi anatimiza ahadi zake kwa vitendo ambapo kwa miaka mitatu ya uongozi wake ameshajenga vitu 25 kwa wilaya 11 za Zanzibar.

 "Lengo la Rais kujenga vituo hivyo ni kuwainua wananchi kiuchumi ili wawe na kipato kizuri kitakachowakwamua kimaisha na kupata maendeleo endelevu, hivyo mengi yamefanyika katika sekta mbali mbali na yanaendelea kufanyika," alifafanua Waziri huyo.

 Mapema Mkuu wa wilaya ya Wete Dk. Hamad Omar Bakar na Mkuu wa Wilaya ya Micheweni Mgeni Khatib Yahya walisema, wamepata faraja kuzinduliwa kituo cha wajasiriamali na stendi kwani vitaimarisha maisha ya wananchi kiuchumi.

 Mapema wafanyabiashara wa kituo cha wajasiriamali Kifumbikai Wete walisema kuwa wamefurahi sana kwani watajikwamua kimaisha na kuiomba Serikali iwapunguzie kodi ili wanufaike zaidi.

 Ujenzi wa kituo cha wajasiriamali kimegharimu zaidi ya shilingi bilioni 1.5 huku stendi ya Kinowe Konde ikigharimu zaidi ya shilingi bilioni 1.4.

Comments

Popular posts from this blog

UTELEKEZAJI WA WANAWAKE UNAVYOKATISHA NDOTO ZA WATOTO.

Mkuu wa Polisi Jamii Kaskazini Pemba akerwa na wanao wafungia ndani watoto wenye ulemavu.

Mrajisi wa Mahakama Zanzibar ahidi kula sahani moja na Mahakimu wasio wadilifu.