RAIS WA ZANZIBA AMESEMA ONGEZEKO LA WATU NI CHANZO CHA KUONGEZEKA KWA MAHITAJI YA JAMII

*RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amesema ongezeko la watu duniani linachangia kwa kiasi kikubwa kuongezeka kwa mahitaji mbalimbali ikiwemo maji.*

 Amesema tatizo hilo pia husababisha uhaba wa huduma na vifaa mijini na vijijini na kuchangia chachu ya mabadiliko ya matumizi ya ardhi.

 Dk. Mwinyi aliyasema hayo hotel ya Verde Mtoni, mkoa wa Mjini Magharibi, alipofungua kongamano la 24 la maji lililoyashirikisha mataifa kutoka Mashariki na kusini mwa bara la Afrika.

 Alisema, hali hiyo huibua maswala mengi yakiwemo kuzorota kwa vyanzo vya maji, uchafuzi wa mazingira, upotevu wa viumbe hai na upotevu wa afya ya mazingira kwa ujumla. 

 Alisema, ushahidi wa hayo unaonyesha mazingira ya nchi nyingi za bara la Afrika  yanabadilika mara kwa mara kutokana na mabadiliko ya tabia nchi yanayohuhusishwa na mabadiliko ya hali ya hewa husababisha ongezeko la hatari kutokana na hali mbaya ya hewa.

 Rais Dk. Mwinyi pia alieleza, changamoto hizo zinahitaji usimamizi endelevu wa rasilimali za maji ili kukidhi mahitaji ya sasa ya kiikolojia, kijamii na kiuchumi bila kuathiri uwezo wa kukidhi mahitaji hayo kwa siku zijazo.

 

“Tunahitaji kuwa na msimamo thabiti na kuendeleza mikakati ya kupata maji kwa ajili ya watu wetu, uchumi wetu pamoja na mazingira” alisisitiza Rais Dk. Mwinyi.

Alisema, kongamano hilo limekuja wakati mwafaka wakati mataifa ya kusini mwa bara la Afrika yakiendeleza mchakato wa kuharakisha mabadiliko kupitia mbinu za kibunifu na utengamano kwa ajili ya usimamizi endelevu wa rasilimali za maji kwenye mataifa yao. 

 “Tunaamini tunapobadilishana uzoefu na utaalamu baina yetu kupitia mkutano huu kutaleta mawazo mapya na njia za kutumia vyema na kudhibiti maji au kuongeza maji yanayopatikana sasa kupitia suluhu mbadala" alieleza Dk. Mwinyi.


 Alisema, Zanzibar ilianzisha mpango wa uwekezaji maji wa mwaka 2022 hadi 2027 uliolenga kukusanya rasilimali kwa ajili ya uwekezaji wa usalama wa maji kwa ajili ya utekelezaji na uendelevu wa muda mrefu wa usambazaji maji kwa mahitaji ya msingi na miradi ya maji kwa mahitaji ya kiuchumi. 

 Rais Dk. Mwinyi alisema pia mpango huo umezingatia maeneo matano yakiwemo uwekezaji wa maji na fedha kwa ajili ya kuboresha huduma za maji na usafi wa mazingira, Kujenga uwezo wa kuhimili hali ya hewa, Usawa wa kijinsia na ushirikishwaji wa kijamii, Kuimarisha utaratibu wa kitaasisi, pamoja na Uchumi wa bluu na usimamizi endelevu wa rasilimali maji.

 

Halkadhalika, Rais Dk. Mwinyi aliwakaribisha washirikiri na wageni wa kongamano hilo kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii vilivyomo nchini, akiwaeleza sifa za kisiwa maarufu duninani kinachotamba na sifa ya marashi ya karafuu Zanzibar, kutokana na kilimo na usindikaji wa viungo vyenye harufu nzuri za karafuu, manjano, mdalasini, mchaichai, pilipili manga na hoho. Pia aliwataka wageni hao kutembelea  mashamba ya viungo ili kujifunza kuhusu mchakato na historia wa mazao hayo.

 Sambamba na kuwaeleza vivutio vyengine vya utalii vinavyopatikana Zanzibar  ukiwemo utamaduni, mila na silka za kipekee kwenye maeneo ya kihistoria ya hifadhi ya mji Mkongwe wa Zanzibar ambao ni urithi wa dunia, Fukwe zenye mchanga mweupe na maeneo mengine ya hifadhi ya asili.

 Kongamano hilo limewaweka pamoja wataalamu wa kutunga sera, wasomi, watafiti na wadau wa tasnia ya maji kwa lengo la kubadilishana ujuzi na uzoefu ili kuchunguza njia sahihi za kushughulikia changamoto na matarajio ya kimsingi kwa sekta ya maji kwa mataifa ya  Mashariki na Kusini mwa bara la Afrika. 


Akizungumza kwenye mkutano huo, Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Omar Juma Kipanga, alipongeza juhudi zinazochukuiliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kukuza Sekta ya Maji kupitia uchumi wa Buluu.

 Naye, Naibu Waziri wa Maji, Nishati na Madini, Zanzibar Shaaban Ali Othman alisema jitihada kubwa zinaendelea kuchukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuwaondolea changamoto ya maji wananchi wake pamoja na kuhakikisha usalama wa maji safi unaendelea kuatikana maeneo yote ya Zanzibar.

Naye Mwenyekiti wa taasisi ya SADC “Water Net Trust” na Mtaalamu wa mazingira kutoka Namibia, Prof. Nnenesi Kgabi, alieleza mkutano huo ni fursa muhimu ya kubadilishana uzoefu na ushirikiano baina ya washiriki ambao unadumisha uhusiano uliopo baina ya mataifa ya kusini mwa bara la Afrika.

 Kongamano hilo la 24 la maji kwa lililokuwa na lengo la kuvumbua na kushirikiana kwa nia usimamizi endelevu wa rasilimali maji Afrika, lilitoka kaulimbiu isemayo “Kuharakisha Mabadiliko, Kukuza Ubunifu na Utengamano wa Usimamizi Endelevu wa Rasilimali Maji kwa mataifa ya Mashariki na Kusini mwa Bara la Afrika 

Hii ni mara ya tatu kwa Tanzania kuwa mwenyeji wa mkutano huo ikiwemo mara mbili ulifanyika Dar es Salaam na Zanzibar ni mara ya kwanza.

 *IDARA YA MAWASILIANO IKULU, ZANZIBAR*




 

 

 

 

 

Comments

Popular posts from this blog

UTELEKEZAJI WA WANAWAKE UNAVYOKATISHA NDOTO ZA WATOTO.

Mkuu wa Polisi Jamii Kaskazini Pemba akerwa na wanao wafungia ndani watoto wenye ulemavu.

Mrajisi wa Mahakama Zanzibar ahidi kula sahani moja na Mahakimu wasio wadilifu.