Aga Khan Foundation yaihamasisha jamii kupanda miti

                           NA ZUHURA JUMA, PEMBA

JAMII imetakiwa kuwa na utamaduni wa kupanda miti katika maeneo yao wanayoishi, ili kuweka mazingira bora pamoja na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

 Akizungumza kwa niaba ya Afisa Mdhamini Wizara ya Elimu Pemba, mwalimu Harith Bakar Waziri wakati wa upandaji miti kwa ajili ya kutengeneza msitu mdogo, katika skuli ya sekondari ya Hemed Pujini alisema,  Wizara itachukua juhudi za makusudi kuhakikisha msitu huo unatunzwa.

 Alisema kuwa, ni manufaa makubwa kupata msitu huo kwani eneo hilo ni ukanda wa mashariki ambao umeathiriwa sana na mabadiliko ya tabianchi, hivyo utawasaidia sana wanafunzi, walimu na wanajamii kuwa na mazingira bora na mazuri.

 "Muone kuwa kuwepo kwa msitu mdogo hapa ni jambo jema na ni fursa kwenu, hivyo kuna haja kwa jamii kuiga mfano huu na wapande miti maeneo mbali mbali katika mitaa yao," alieleza.

 Aidha aliwataka kuulinda na kuuhifadhi msitu huo ili kuleta manufaa kwao na jamii nzima, jambo ambalo litaigwa na skuli nyengine kutokana na umuhimu wake.

 

Kwa upande wake Mratibu wa mradi wa upandaji miti kwa ajili ya msitu mdogo kutoka taasisi ya Aga Khan Foundation (AKF), Japhet Elly Wangwe alisema, lengo kubwa la mradi huo ni kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.

 Alisema kuwa, wanapanda misitu midogo maeneo mbali mbali, ambapo kwa Dar-es-salaam na Lindi wameshapanda maeneo 70 na Zanzibar ni mawili likiwemo la skuli ya sekondari Hemed Pujini Pemba.

 "Kwa Zanzibar skuli ya kwanza ni hii ya Hemed na kesho tunaenda kupanda kule Unguja, tunafanya hivi kwenye maskuli ili kupambana na hali hii, kwani wanafunzi watajifunza na wataendeleza wakiwa majumbani kwao," alifahamisha.

 Aliishukuru Serikali kwa kuwapa mashirikiano makubwa, ambayo yanawapa msukumo na hamasa ya kuweka mazingira bora ambayo hayataathiriwa na mabadiliko ya tabianchi.


Nae Afisa kutoka Idara ya Misitu Pemba Massoud Bakar Massoud alisema, aliishukuru AKF kwa kuwaletea mradi huo kwani utawasaidia kurudisha asili ya kisiwa cha Pemba kwa kupandaji miti kwenye maeneo mbali mbali.

 "Kwa upande wetu tunao mradi wa kurudisha asili ya kisiwa hiki, hivyo na mradi wa upandaji miti kwa ajili ya misitu midogo itaongeza kasi ya kukabiliana na athari zinazotokana na mabadiliko ya tabianchi," alieleza.

 "Mabadiliko ya tabianchi ni janga kubwa sana, hivyo ili kudhibiti hali hiyo tutashiriki kikamilifu katika kusimamia, kuutunza na kudhibiti kusitokee uharibifu katika eneo hilo," alifafanua.

 Mapema Afisa Maendeleo ya jamii kutoka taasisi ya Malezi na Makuzi Bora ya watoto wadogo (MECP-Z) Haji Ali Hamad, aliwataka wananchi kuona kuwa suala la upandaji wa miti katika skuli hiyo ni jema kwani wanatengeneza fursa kwao na wengine.

 Mwalimu Mkuu skuli hiyo Jamila Ali Saleh alieleza kuwa, watashirikiana na wanafunzi kuona kwamba miti hiyo inakuwa na kunawiri vizuri, ili iweze kuwanufaisha.

 Mwanafunzi Samira Mohamed Nassor na Zahor Said Massoud walisema kuwa, wamejifunza kupanda miti na hivyo wataishughulikia ili kuboreka, kwani wanaamini itawasaidia kupata mazingira bora yenye upepo wa asili na hewa safi.

 Katika utengenezaji wa msitu huo mdogo, zaidi ya miti 200 ya aina mbali mbali imepandwa.

Comments

Popular posts from this blog

UTELEKEZAJI WA WANAWAKE UNAVYOKATISHA NDOTO ZA WATOTO.

Mkuu wa Polisi Jamii Kaskazini Pemba akerwa na wanao wafungia ndani watoto wenye ulemavu.

Mrajisi wa Mahakama Zanzibar ahidi kula sahani moja na Mahakimu wasio wadilifu.