BAADA YA BLOG YA PEMBA YA LEO KUIBUA KERO YA MWALIMU WA MADRASA MWENYE ULEMAVU KOKOSA SEHEMU SALAMA YA KUSOMESHEA SASA APATA UFADHILI WA KUJENGEWA.

 



BAADA YA  BLOG YA PEMBA YA LEO  KUCHAPISHA MAKALA

-Mwalimu mwenye ulemavu   wa viungo ajengewa mdarassa Shumba vyamboni

-Aibuka kuushukuru  mtandao  wa pemba ya leo, mfadhili, wanafunzi wasema jambo

FATMA HAMAD, PEMBA

JUNE  24 , mwaka 2022, Blog ya pemba ya leo, lilichapisha makala, ikielezea changamoto za ukosefu wa madrassa ya kisasa ya mwalimu wa madrasa mwenye ulemavu wa viungo.

Mwalimu huyo Saada Khamis Hamad wa Shumba vyamboni wilaya ya Micheweni mkoa wa kaskazini Pemba, akikabiliwa na changamoto ya ukosefu sehemu rafiki na salama ya kusomeshea wanafunzi wake.

Ndoto zake za kupata madrassa ya kisasa kwa ajili ya kufundishia wanafunzi wake, hakuwa nayo kabisa kwenye akili yake, hasa kwa vile alishasomesha miaka zaidi ya minne katika mazingira magumu.

Kwa kweli alikua na kilio cha siku nyingi, cha kupata ufadhili wa kujengewa madrasa, ndipo mwandishi wa makala kupitia blog ya pemba ya leo Pemba, alipochapisha makala yake na kisha wafadhili kuchomoza.



Nilikua sina tegemeo kama ipo siku moja  nitaondokana na kadhia hii ya kusomesha kibarazani.

‘’Sikua na tamaa kabisa kama na mimi ipo siku nitasomesha nikiwa ndani ya madrsa’’alisema mwalimu.

na mimi natasomesha wanafunzi wangu nikiwa  ndani ya madras

 

MJENZI WA MADRASSA

Msimamizi anaeshughulikia ujenzi wa madrasa hiyo, Mohamed Suleiman kutoka kijiji cha Konde, anasema ujenzi huo ni ufadhili kutoka kwa Jumuia ya Firdausi yenye makao makuu yake jijini Dar-es Salaam.

Baada ya kusikia kwa waumini, ambao nao walisoma kwenye Blog ya Pemba ya  leo, ndipo naye alipochukua juhudi za kuwasiliana na wafadhili hao.

Anaona, kuandikwa kwa habari hiyo juu ya changamoto za mwalimu huyo mwenye ulemavu, kusomesha barazani wanafunzi 75 ni shida.

‘’Kwa hakika, uandishi ule uliofanywa na mwandishi wa makala ya Blog ya Pemba  ya leo ya june  24, mwaka 2022, juu ya shida na dhiki ya makaazi ya wanafunzi wa madrassa,’’anasema.

Hapo kilichofuata, ni kulipima eneo ambalo mwalimu husika ameamua kuwa ndio eneo la madarssa, na baada ya kujua idadi ya wanafunzi wake, ilirahisisha kazi.

‘’Tumejenga madrasa yenye chumba kimoja chenye upana na urefu wa mita nane kwa saba (8/7), pamoja na vyoo viwili kwa ajili ya wanafunzi,’’anasema.

Ingawa kwake anasema haoni sababu ya kutaja gharama halisi za ujenzi huo, anachotaka kuona ni wanafunzi kupata eneo la kudumu la kusomea.

‘’Sisi kwa sasa tunaendelea na ujenzi na umefikia asilimia 95 maana, umeanza kupigwa plasta na wakati wowote, wanafunzi na mwalimu watahamia,’’anasema.

MWALIMU WA MADRASSA

 

 Mwalimu huyo Sada Khamis Hamad, anasema wakati anahojiwa na mwandishi wa makala, hakuwa na fikra ya kuwa inaweza kuwa msaada wa kupatiwa madrassa ya kisasa.

‘’Wengi wameshapita na kunihoji na wakiniahidi kuwa, ntajengewa madrassa ya kisasa, lakini mwisho wa siku hakuna lolote, lakini kwa mwandishi wa Blog ya Pemba ya leo, nashukuru kwa sasa,’’anasema.

Walishasema wahenga kuwa, Mungu si asumani, kwa hakika sasa msemo huu, umejidhihirisha kwa mwalimu Saada mwenye ulemavu aliyekuwa, akiwapatia elimu ya kur-an wanafunzi 75 barazani kwake.


‘’Leo kwa hakika, siku chache zijazo, ntahamia ndani ya madrassa ya kisasa naushukuru mtandao wa Blog ya pemba ya leo, wafadhili, ofisi ya Mufti na wilaya kwa kusambaaza taarifa zangu,’’anasema.

‘’Kwa kweli nimefurahi sana, kuona kwamba kile kilio changu cha miaka minne kimepata ufumbuzi,’’ alisema mwalimu Saada.

‘’Tunu yangu ni kuona na mimi ninasomesha nikiwa katika madrassa kama vile wenzangu na sio juani kama hivi, haya sio mazingira mazuri, kweli nateseka na wanafunzi wangu,’’anasema.

WANAFUNZI WA MADRASSA

Abdala Kombo Rajabu ambae ni mmoja wa wanafunzi wa madrassa hiyo, anasema anayo furaha kubwa kujengewa kwa madrassa ya kisasa, ambayo ilikuwa ndoto yao.

‘’Kwakweli hali hii ya kusomea kwenye kibaraza ni moja ya changamoto ilioikitufanya tusihudhurie madrasaa, lakini sasa twashukuru mno, kwa waandishi na wafadhili wetu,’’anasema.

Mwanafunzi Fatma Juma Hamad, anasema ujenzi wa madrassa yao, ameupokea kwa furaha na bashasha, kwani wataondokana na changamoto ya kusoma kwenye baraza kama zamani.

‘’Tumefurahi kuona kile kilio chetu cha muda mrefu cha kupata sehemu salama ya kusomea sasa, kimepata ufumbuzi,’’anasema mwanaunzi Fatma.

Rehema Haji Seif amewataka wanafunzi wenzake, kuitunza na kuilinda miundombinu ya madrassa hiyo, ili kuwanufaisha wao na wengine hapo baadae.

WAZAZI WA WANAFUNZI

Haji Seif ameeleza kuwa, licha ya msaada huo aliopata mwalimu huyo, watahakikisha nawao wanamuunga mkono, ili kuona anapata nguvu ya kuendeleza, jambo lake hilo, la kuwapatia watoto elimu ya kur-an.

 ‘’Kwa vile mwalimu huyo nguvu zake zote kazielekeza kutusomeshea watoto wetu, na sisi tutahakikisha tunamsaidia japo kwa michango midogo midogo,’’anasema.

Asha Khamis Ali alimshukuru muhisani, ambae alijitolea na kujenga madrassa, baada ya kuona habari iliyorushwa na mwandishi wa habari June 24, mwaka 2022 juu changamoto ya kusoma kwenye barazani.

‘’Tunamuombea duwa muhisani wetu aliewajengea watoto wetu madrassa, Mwenyezi Mungu ampe imani aendelee kuelekeza nguvu zake kwenye mambo ya kheri,’’ anafafanua.

WANAFAMILIA

Assa Khamis Hamad mwenye ulemavu wa viungo ambae ni kaka wa mwalimu huyo, amesema msaada wa ujenzi wa madrassa wameupokea kwa mikono miwili.

Mama mzazi wa mwalimu huyo Hadia Salim Ameir amewashukuru wahisani waliomsaidia mwanawe huyo, kwani wamekua wakija watu wengi wakimuahidi na mwisho wa siku hawaoni lolote.

‘’Kipindi cha nyuma huja watu wakinihoji na kujidai watakuja kunisaidia, ila sioni lolote, sijui ilikua wakifanya kwa ajili ya maslahi yao tu au vipi,’’anaeleza.

OISI YA MUFTI

Sheikh Said Mohamed kutoka Ofisi ya Mufti kisiwani Pemba anasema, amefarijika kuona mwalimu huyo amepata ufadhili wa kujengewa madrassa.

‘’Kama ofisi ya Mufti tumefurahi kuona wafadhili na wahisani wamejitokeza na kumsaidia mwalimu huyo wa madrassa, mwenye ulemavu anaefanya kazi ya kuyasambaza maneno ya Mwenyezi Mungu,’’anaeleza.

WANAHARAKATI

Safia Saleh Sultan kutoka Kituo cha Huduma za Sheria Pemba, anasema moja ya utekelezaji wa haki za binadamu moja ni kuweka mazingira rafiki ya kupata elimu.

Asha Mussa Omar, anasema juhudi za mwalimu huyo, ndio mwelekeo wa TAMWA katika kuthibitisha kuwa wanawake wanaweza kufanya mambo makubwa.

Mjumbe wa kamati tendaji wa Jumuia ya wanawake wenye ulemavu Pemba bi Hidaya Mjaka Ali amesema wanafuraha kuona juhudi za watu wenye ulemavu  zinafanikiwa.

 

KATIBA YA ZANZIBAR YA MWAKA 1984

Kifungu cha 10 (g) kinafafanua ‘kwamba serikali itawekea mazingira rafiki kwa makundi ya wagonjwa, waliojiajiri, wazee, watoto na watu wenye ulemavu’.

Lakini hata kifungu cha 12 (1) kimefafanua kuwa, ‘watu wote ni sawa mbele ya sheria, na wanayo haki, bila ya ubaguzi wowote, kulindwa na kupata haki sawa mbele ya sheria’.’

SHERIA YA WATU WENYE ULEMAVU NO 9/2006

Kifungu cha 9, kinaelezea haki ya kupata elimu kwa watu wote wenye ulemavu na mafunzi mengine kama ilivyo kwa raia wengine. 

MIKATABA YA KIMATAIFA

Mkataba wa kimataifa wa haki za watu wenye ulemavu, kwenye ibara 24 (b) inafafanua kuwa, nchi zilizoridhia mkataba huu, wanatakiwa kuendeleza mtazamao, uwezo na ubunifu pamoja na uwezo wao wa akili na mwili kwa watu wenye ulemavu.

 








Comments

Popular posts from this blog

UTELEKEZAJI WA WANAWAKE UNAVYOKATISHA NDOTO ZA WATOTO.

Mkuu wa Polisi Jamii Kaskazini Pemba akerwa na wanao wafungia ndani watoto wenye ulemavu.

Mrajisi wa Mahakama Zanzibar ahidi kula sahani moja na Mahakimu wasio wadilifu.