ZECO LAWAPA MATUMAINI WANANCHI PEMBA.

 

 

                   NA SAID ABRAHMAN PEMBA.

 SHIRIKA la Umeme (ZECO) tawi la Pemba limesema kuwa litaendelea kushirikiana na wananchi wa Kisiwa hicho ili kuhakikisha nishati hiyo inaenea vijiji vyote vilivyoko huko.

 Hayo yalibainishwa na Ofisa mipango na utafiti wa Shirika hilo Ali Faki Ali wakati alipokuwa akizungumza na Masheha wa Wilaya ya Wete huko katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Wete.

 Alieleza kuwa Kwa Sasa Shirika limefanikiwa kupeleka nishati ya umeme katika vijiji vipatavyo 417 kati ya 424  huku Shirika hilo likipeleka nishati hiyo katika Visiwa vyote 8 vilivyomo ndani ya Pemba ikiwa ni pamoja na Njao, Fundo, Kokota, Uvinje,Kojani, Shamiani,Kisiwa panza na Makoongwe.

 "Kwa Sasa tuna asilimia 98.3 ya vijiji vyote ambavyo tayari vimeshapata huduma ya umeme huku asilimia 1.7 tu ndivyo ambavyo vimebaki havina umeme, Shirika limo mbioni kuhakikisha navyo vinapata umeme mwaka huu," alieleza Ofisa Ali 

 Ofisa huyo alivitaja vijiji ambavyo havijafika na huduma ya umeme Hadi sasa ni pamoja na Kijiji Cha Kivumoni Mtambwe pamoja na Kijiji cha Mtakao Kilichopo Shehia ya Mlindo Kwa upande wa Wilaya ya Wete.

 "Ama Kwa upande wa Wilaya ya Micheweni ni Kiuyu mbuyuni ambako Kuna vijiji vitatu navyo ni Mkwaju panda, Makombani na Mkondoni huku Wilaya ya Mkoani ni Mtadoda iliyopo katika Shehia ya Minazini pamoja na Kijiji Cha Alikoni Kilichopo Shehia ya Chumbageni Mkoani," alieleza Ali.

  "Jukumu la Shirika la umeme ni kuwafikishia wananchi wote huduma ya nishati ya umeme, hivyo katika mikakati yetu tumedhamiria kuona wananchi wananufaika na huduma hii," alisema Ofisa huyo.

 Nae Ofisa Mipango na utafiti wa Shirika hilo Pemba Hafidh Tahir Silima aliwafahamisha Masheha hao kuwa Kwa Sasa hakuna gharama yeyote ambayo anatozwa mwananchi Kwa kununua nguzo ya umeme.

 "Serikali ya awamu ya nane (8) chini ya Dkt, Hussein Ali Hassan Mwinyi umeondoa gharama ya kuchangia nguzo Kwa wananchi wake,lakini pia hata gharama za kuunga umeme pia zimepunguzwa Hadi kufikia Tsh, 200,000/- (laki mbili),"alieleza Hafidh.

 Hata hivyo Ofisa huyo aliwatoa wananchi ambao tayari wameshalipa gharama za kuungiwa umeme katika maeneo yao lakini Hadi sasa huduma hiyo haijawafikia wasiwe na wasiwasi Shirika limo mbioni kuona nao wananufaika na huduma ya umeme.

 "Tulikuwa na tatizo la vifaa ila Kwa Sasa muarubaini umepatikana kwani meli ambayo ilibeba mzigo wa vifaa hivyo tayari imeshafunga nanga katika bandari ya Unguja na mzigo umeshaanza kupakuliwa, hivyo tutahakikisha wale ambao wameshalipa fedha zao wanapata huduma,"  alisema Hafidh.

 Nae Mohammed Said Sound aliwata Masheha kuwashajihisha wananchi wao kufika ofisini wenye wao wakati wanapotaka kuunga umeme bila ya kumtuma mtu mwengine ili kuepusha rushwa.

 "Tuwatake wananchi wetu pale ambapo watakuwa wanataka kuunga umeme ni vizuri kuja wenyewe ofisini kwetu ili kuepusha rushwa," alisema Mohammed.

 Mapema akifungua kikao hicho, Katibu Tawala Wilaya ya Wete Mkufu Faki Ali aliupongeza uongozi wa Shirika la umeme Pemba Kwa mashirikiano yao kwani wamekuwa karibu sana na wananchi wake.

 Alisema kuwa kikao hicho ni utaratibu wa Shirika hilo uliojipangia ili kuonana nao na kupata takwimu sahihi za vijiji ambavyo Hadi sasa havijapata huduma ya umeme.

 Aidha Katibu huyo alifahamisha kuwa Shirika hilo limepewa jukumu na Serikali kuhakikisha wananchi wote wanapata huduma ya umeme bila ya ubaguzi wowote ule.

 "Tunalishukuru Shirika la umeme Kwa kuwa nasi karibu sana kwani pale ambapo panatokezea tatizo lolote watendaji wake hufika katika eneo na kuweza kulitatua Kwa muda muafaka," alisema Mkufu.

 Nae Mwenyekiti wa Masheha Wilaya ya Wete ambae pia ni Sheha wa Shehia ya Mtambwe Kusini Othman Ali Khamis amelipongeza Shirika la Umeme (ZECO) Kisiwani Pemba Kwa mashirikiano yao wanayowatoa Kwa wananchi wao.

 "Tunaliomba Shirika kuendelea kushirikiana na sisi ili tuweze kupiga hatua ya maendeleo katika maeneo yao," alisema Sheha Othman.

 

               

 

Comments

Popular posts from this blog

UTELEKEZAJI WA WANAWAKE UNAVYOKATISHA NDOTO ZA WATOTO.

Mkuu wa Polisi Jamii Kaskazini Pemba akerwa na wanao wafungia ndani watoto wenye ulemavu.

Mrajisi wa Mahakama Zanzibar ahidi kula sahani moja na Mahakimu wasio wadilifu.