WANANCHI WAHIMIZWA KUCHUKUA TAHADHARI JUU YA KUJIKINGA NA UGONJWA WA UKO19

 

NA FATMA HAMAD PEMBA

AFISA Mdhamini wizara ya Afya, ustawi wa jamii, wazee, jinsia na watoto Pemba Yakoub Mohamed Shoka, amewataka waandishi wa habari kuelimisha jamii kwa kutilia mkazo suala la unawaji wa mikono ndani ya jamii zao zilizowazunguka.

Alisema, hivi sasa takwimu za kidunia zinasema kati ya nchi 60 zenye maambukizi ya Corona katika kiwango kikubwa kila watu wawili kati ya watatu kwenye watu Bilioni 1 ambao wameshapata maambukizi wamekosa huduma safi ya mikono majumbani mwao kwa kunawa maji tiririka na sabuni. 

Akisoma hotuba kwa niaba ya Afisa mdhamini huyo Afisa uwezeshaji kinga na elimu ya afya Pemba Khamis Bilali Ali alisema, matumizi ya maji yamehimizwa na kutajwa hata katika vitabu vya dini hivyo aliitaka jamii kujenga utamaduni wa kunawa mikono ili kuepuka maradhi yanayoambukizwa.

Aliyasema hayo katika mkutano uliowashirikisha waandishi wa habari ikiwa ni katika kuelekea maadhimisho ya siku ya unawaji mikono Zanzibar uliofanyika ukumbi wa hoteli ya Archipilago Tibirinzi Chake chake.

Alisema, kutokana na taarifa za hivi karibuni watu waliowengi hususani kwa nchi zilizoendelea ikiwemo Zanzibar ipo katika uwezekano mkubwa wa kupata maambukizi yanayotokana na kutokunawa mikono.

“Tunaweza kupata maambukizi ya magonjwa ya kipindupindu na Corona sababu kuu ikiwa ni kutoendeleza tabia na utamaduni wa kunawa mikono na nusu ya wanaopata madhara ni watoto, katika maeneo ya skuli kukosa nyenzo”, alisema.

Aidha alisema, iwapo jamii inataka kujizuia na maradhi hayo ni lazima itoe kipaumbele katika suala la usafi wa mikono na huduma zake zipatikane wa wote.

Hata hivyo alisema, Wizara ya afya hivi sasa inahitajika kuunganisha nguvu zake kwa wafadhili wa kimataifa, kitaifa, sekta za serikali na binafsi pamoja na asasi za kiraia ili kuhakikisha kunakuwa na nguvu za pamoja za upatikanaji wa nyenzo na huduma rahisi watu wanazoweza kuzimudu.

Mapema Mratibu wa kitengo cha elimu ya afya Pemba Abeid Ali Ali alisema, lengo la kuandaa mkutano huo kwa waandishi wa habari ni kupeleka elimu kwa jamii.

“Waandishi wa habari ni kiunganishi kizuri kati ya jamii na jamii nyengine hivyo tumefarajika sana kukutana nanyi katika mkutano huu matumaini yetu mutafikisha taarifa kwa jamii kama inavyotakiwa”, alisema.

Nae Mtaalamu wa afya ya jamii kitengo cha afya na mazingira Halima Ali Khamis alisema, mipango ya wizara katika kuelekea siku ya unawaji mikono jambo la kwanza ni kuelimisha jamii licha ya kuwa jamii ni ngumu kulingana na tabia zilizojengeka za kutokunawa mikono kwa maji tiririka.

“Wizara ina mipango mingi katika kulifanikisha jambo hili iliwemo kutoa elimu kwa jamii, kupitia gari za matangazo, vipeperushi, video, lazima jamii ifahamu kwamba kunawa mikono ni njia ya kujikinga na maradhi mbali mbali” alisema.

Siku ya kuosha mikono huadhimishwa kila ifikapo Oktoba 15 ya kila mwaka lakini kutokana na sababu mbali mbali maadhimisho hayo yalilazimika kusogezwa mbele na kutarajiwa kufanyika Kitaifa Febuari 8 mwaka huu kauli mbiu yake ikiwa ni “OSHA MIKONO OKOA MAISHA”.

                                           

Comments

Popular posts from this blog

UTELEKEZAJI WA WANAWAKE UNAVYOKATISHA NDOTO ZA WATOTO.

Mkuu wa Polisi Jamii Kaskazini Pemba akerwa na wanao wafungia ndani watoto wenye ulemavu.

Mrajisi wa Mahakama Zanzibar ahidi kula sahani moja na Mahakimu wasio wadilifu.