SERIKALI YATAKIWA KUJENGA VINDA ABAVYO VITATOA AJIRA KWA VIJANA

 

NA SAID ABRAHMAN PEMBA.

 JAMII imeiomba Serikali kujenga viwanda vya kusindikia samaki ili kwenda sambamba na dhana ya uchumi wa bluu.

 Wakijadili mada juu ya uchumi wa bluu katika kikao kilichoandaliwa na taasisi ya Action aid, huko Kojani Mkoa wa Kaskazini Pemba, wananchi wa Kisiwa hicho walisema kuwa ni vyema kwa Serikali kuanzisha viwanda hivyo ili waweze kunufaika na mazao yanayotokana na bahari na kufikia azma ya uchumi wa bluu.

 Walieleza kuwa wananchi wananchi walio wengi hawajawa na uelewa sahihi juu ya dhana ya uchumi wa bluu, hivyo ni vyema kwa Wizara husika kutoa taaluma kwa wananchi ili waweze kuelewa maana yake.

 Hamad Juma mjumbe wa Kikundi Cha Mduara alisema kuwa ili Serikali iweze kukuza uchumi wa bluu na kukuza hali za maisha ya wananchi lazima iweze kujenga viwanda vya kusindikia samaki ili iweze kwenda sambamba na azma yenyewe ya Uchumi wa bluu.

 Alieleza kuwa endapo Serikali itaweza kujenga viwanda hivyo wananchi wengi wataweza kunufaika ikiwa ni pamoja na kupata ajira ambazo zitainua hali zao za kiuchumi.

 "Serikali ikiweza kufanya jambo hili la kuweka viwanda vya kusindikia samaki naamini wananchi wengi wataweza kupata nafasi za ajira katika viwanda hivyo,lakini pia hata wale samaki ambao watavuliwa wataweza kuhifadhika kiurahisi zaidi," alisema Hamad.

 Nae Mohammed Juma Ali mkaazi wa Kojani aliwaomba watendaji wa Wizara husika kushuka chini kwa wananchi ili kuelimisha mantiki ya uchumi wa bluu ili wananchi waweze kufahamu dhana hiyo.

 Aidha Mohammed aliiomba Wizara hiyo kuandaa mikakati maalum ambayo itatekelezeka na kutoa ufanisi mzuri kwa watendaji wake ili wananchi waweze kufaidika na uchumi wa bluu.

 Mapema Mohammed alieleza kuwa katika bahari Kuna faida nyingi ambazo zinapatikana ikiwemo uvuvi, kilimo Cha mwani, ufugaji wa majongoo, mapambo ya nyumbani,madini pamoja na mafuta ambavyo vyote vina faida kwa jamii na taifa kwa ujumla.

 "Katika bahari Kuna faida nyingi sana ambazo zinapatikana na zinaleta tija kwetu ikiwemo kilimo,ufugaji, mapambo na madini", alieleza Mohammed.

 Nae Mwenyekiti wa Kikundi Cha Mduara Kombo Hamad Kombo aliiomba Serikali kutilia maanani suala zima la upatikanaji wa bima kwa wavuvi.

 Alisema kuwa imekuwa ni shida kubwa kwa wavuvi wakati wanapopata matatizo wakiwa katika harakati zao za uvuvi.

 "Mara nyingi sisi wavuvi tunaovua maeneo ya mbali huwa tunapata matatizo mbali mbali ikiwemo kupotelewa na nyavu zetu au hata mashine zetu, hivyo tunaiomba Serikali kufanya jitihada za makusudi ili kuona wavuvi wanapatiwa bima ambayo itaweza kuwasaidia pale wanapitokezewa na matatizo,"alisema Mwenyekiti Kombo.

 

Comments

Popular posts from this blog

UTELEKEZAJI WA WANAWAKE UNAVYOKATISHA NDOTO ZA WATOTO.

Mkuu wa Polisi Jamii Kaskazini Pemba akerwa na wanao wafungia ndani watoto wenye ulemavu.

Mrajisi wa Mahakama Zanzibar ahidi kula sahani moja na Mahakimu wasio wadilifu.