TATIZO LA MAJI LILILOKUWA LINAIKABILI KITUO CHA AFYA WESHA SASA LAPATA UFUMBUZI
NA FATMA HAMAD, PEMBA
Septemba 21 mwaka huu Blog ya Pemba ya leo iliibua
changamoto ya kukosekana kwa huduma ya Maji safi na salama katika kituo cha
Afya cha Wesha wilaya ya Chake chake Pemba, ambapo kilio hicho kimepatiwa
ufumbuzi kwa sasa.
Wakizungumza na mwandishi wa
habari huko kituo cha afya wesha Safinia Said na Rukia Khamis ambao ni
wajawazito waliokwenda kupata huduma kituoni hapo walisema zaid ya miezi 3
kulikuwa hakuna maji kituoni hapo.
Walisema kwa sasa shida ya Maji imepungua kwani Maji yanapatikana ijapokuwa hayatoki siku zote ni kwa mgao.
''kwa sasa hatuendi na
madumu ya Maji tunapokwenda kujifungua kwani Maji ya zawa ikifika zamu ya
kutoka huwa yanapatikana hapa kituoni,, walisema
Hivyo tunaiomba Wizara ya
Maji iyongeze juhudi ili kuona Maji yanapatikana masa yote 24 kwani suala la uzazi
ni kitu cha kila siku jambo ambalo litaondosha usumbufu kwa mama wajawazito pamoja
na wazazi wanaokwenda kujifungulia kituoni hapo.
Kwa upande wake Yusra Amour
Juma aliejifungulia kituoni hapo alisema alihudumiwa vizuri na hakupata shida
iyoyote kwani Maji yalikuwa yanatoka kwa wingi kwa siku hiyo aliyokwenda kujifungua.
''Nashukuru nilipokwenda
kujifungua sjakwenda na dumu langu la Maji, kwani ilikua hapo kituoni yanatoka,
alieleza.
Ali Juma Na Haji Khamis
walisema kipindi cha nyuma wakilazimika kuchukuwa Maji yao wakati wanapokwenda
kuwapeleka wake zao kujifungua, ila kwa sasa tatizo hilo limeondoka.
Alisema kwa kipindi hiki Maji yanatoka, licha
ya kuwa hayatoki siku zote bali yanatoka kwa mgao.
''Licha ya changamoto ya
Maji kuwa haijaondoka moja kwa moja lakini imepungua, Kwani kwa sasa hivi ndani
ya wiki moja tunapata Maji siku mbili au tatu, hiyo ni afadhali, alisema.
Alisema changamoto
inayowakabili kwa sasa kituoni hapo ni kukosekana kwa Tenki la kuhifadhia Maji.
''Tenki tunalotumia ni dogo,
ni la lita 2000 na pia linavujisha Maji hayakai, alieleza.
Hivyo ameomba kupatiwa tenki
lenye ujazo wa lita 5000 ili Maji
yaweze kufika angalau kwa siku tatu, jambo ambalo litaondosha moja kwa moja
tatizo hilo kituoni hapo hususan kwa vile hayatoki siku zote.
Alieleza kwa mwezi wamekuwa
wakizalisha wajawazito kati ya 12 hadi 14, ambapo idadi imeongezeka
ukilinganisha na kipindi cha nyuma ambacho Maji yalikuwa hayapatikani moja kwa
moja.
Alieleza kuwa tayari mafundi wao wako katika hatua za mwisho kufanya ukarabati katika sehemu zilizo haribika, hivyo wananchi wakae tayari kwani muda wowote shida hiyo itamalizika na kuona wanajifunguwa kituoni hapo kwa hali ya utulivu.
Nae Afisa mdhamini wizara ya Afya Pemba Khamis Bilali Ali ameupongeza uongozi wa wizara ya Maji kwa jitihada walioifanya ya kuhakikisha Maji yanapatikana kituoni hapo, jambo ambalo litapunguza changamoto za Wauguzi, wajawazito pamoja na wazazi wanaojifungulia kituoni hapo.
Samba mba na hilo amesema watahakikisha wanaondosha changamoto mbali mbali zilizopo kituoni hapo ikiwemo kuweka Tenki lenye ujazo wa Lita 5000, jambo ambalo litasaidia upatikanaji wa huduma ya Maji mda wowote.
Sharif Hamad Khatib ambae ni Daktari mkuu wa Afya wilaya ya Chake chake alisema ni kweli kwa sasa hawajafanikiwa kuweka Tenki la uhakika la kuhifadhia Maji kituoni hapo.
Alisema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kipaombele chake cha mwanzo ni kuhakikisha inapunguza vifo vya Mama na Mtoto, hivyo sehemu yoyote ambayo Mama anakwenda kupata huduma ikiwemo ya Clinik,Uzazi, pahala hapo panatakiwa kupewa kipaumbele zaid kihuduma.
Aidha Daktari huyo amewataka Makampuni binafsi pamoja na wadau mbali mbali kujitokeza na kuwasaidia kujenga mnara wa kuekea Tenki pamoja na kuwajengea Kisima kituoni hapo, ili kuona huduma ya Maji inapatikana wakati wowote na sio kutegemea tu Maji ya Zawa.
Sera ya Wizara ya Afya ya Zanzibar ya mwaka 1990 ni kuhakikisha inaimarisha huduma ya afya ya mama na mtoto, ili kupunguza Vifo vitokanavyo na uzazi pamoja na vya watoto wachanga.
Sekta ya Maji inakumbwa na
ongezeko la mahitaji ya Maji kunakochochewa na ongezeko la idadi ya watu, Uvamizi
wa vianzio vya Maji.
Kwa mujibu wa ripoti kutoka Umoja wa Mataifa [UN] ya machi 22/2023 inasema duniani kote watu Bilioni mbili hawana huduma ya Maji safi ya kunywa, na Bilioni 3.6 wanakosa huduma za usafi zinazosimamiwa kwa usalama.
Comments
Post a Comment