KIJANA ASSA MWENYE ULEMAVU WA VIUNGO AOMBA MSAADA APATIWE MTAJI

 



NA FATMA  HAMAD, PEMBA.

KIJANA Assaa Khamis Hamad mwenye umri wa miaka 35 mkaazi wa Shumba Vyamboni wilaya ya Micheweni Pemba ameomba Serikali pamoja na wahisani wamsaidie mtaji ili aendeleze biashara zake ambazo humpatia kipato cha kuhudumia familia yake.

Kijana huyo mwenye ulemavu wa viungo anafanya biashara ndogo ndogo ikiwa ni pamoja na  njugu nyasa na Vocha kwa lengo la kujipatia kipato kitakacho msaidia na familia yake.  

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwenye machimbo ya mchanga huko Shumba Vyamboni Assaa alisema, hawezi kufanya kazi ngumu kutokana na hali yake kwani  ulemavu alionao ni wa miguu na mikono.

Alisema kuwa, kwa sasa hafanyi biashara hizo kutokana na kukosa fedha za kununulia vocha pamoja na njugu, jambo ambalo anashindwa kuihudumia familia yake.

“Naiomba Serikali, wahisani na taasisi zinazosaidia, wanipatie mtaji angalau wa shilingi milioni mbili ili nifanye biashara kubwa itakayonitatia kipato kikubwa kitachonikwamua kimaisha”, alisema kijana huyo.

Alieleza kuwa, ameamua kuanzisha biashara ili kujikimu kimaisha inagawa anakwama kutokana na kukosa fedha ya kununulia bidhaa hizo, jambo ambalo linamuhuzunisha sana.

“Natoka nyumbani kwangu kwa kigari (wheelchair) hadi kwenye machimbo ya mchanga kuuza njugu na vocha, wateja wangu ni madereva na wanaochimba mchanga, lakini inafika miezi miwili sina nimekaa tu sina biashara yeyote, naiomba Serikali inisaidie mtaji”, alisema.

Alieleza kuwa, hana mtu wa kumsaidia kutokana na kuwa wazazi wake hawana uwezo kwani wamezaliwa wanne wakiwa na ulemavu kama wake.

“Nina ndungu zangu wawili wenye ulemavu wa viungo kama mimi na mmoja alikufa kwani tulikuwa wanne, hivyo sina wakunisaidia na ndio maana napambana mwenyewe lakini nafikia pahala nashindwa”, alifahamisha Assaa.

Alisema kuwa, ana mke na watoto wawili ambao wanamtegemea, ingawa anashindwa kuwahudumia kutokana na kukwama katika biashara zake hizo ambazo ndizo zinazompatia kipato.

Alisema licha ya hali ya ulemavu anayoishi nayo, lakini hapendi kuishi katika maisha ya utegemezi na ndio maana alijiajiri mwenyewe, hivyo ni vyema wakahurumiwa na kusaidiwa.



Kwa wao vibarua wanaochimba mchanga walisema kuwa, licha ya ulemavu alionao kijana huyo lakini amejiajiri mwenyewe kwa kuuza biashara ya vocha na njugu, ili kujikimu inagawa anakwama kutokana na kukosa mtaji.

“Kwa kweli hali halisi ya kimaisha ya kijana Assaa sio nzuri, anaishi katika hali ngumu huku akiwa mikono yake haina nguvu na wala hawezi kutembea, ambapo hutumia kigari kufika hapa machimboni, hivyo tunaomba wahisani wamsaidie kwani akili yake iko vizuri na hapendi kujituliza”, alieleza.

Nao baadhi ya madereva wanaokwenda kuchukua mchanga katika eneo hilo walisema kuwa, wanamunga mkono kijana huyo kwa kumpatia pesa ili aweze kujisaidia mahitajio yake, ingawa haikidhi mahitaji yake kwani ni kiwango kidogo sana wanachompatia. 

Mratibu Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi Haji Khamis Haji alifahamisha kuwa, wao wanatoa fedha kwa mkopo katika vikundi mbali mbali na sio vyenginevyo.

Nae Mratibu wa Idara ya watu wenye ulemavu  Kisiwani Pemba Mashavu  Juma Mabrouk amesema wanao mfuko maalum ambao wanawawezesha  wajasiriamali  wenye ulemavu.

Amefahamisha kuwa  lengo la kuwepo kwa mfuko huo  ni kuwasaidia   Mtaji watu wenye ulemavu  ambao wanataka kujiajiri wenyewe kwa kuanzisha biashara zao ambazo zitawapatia kipato.

Aidha amefahamisha kua mkopo huo hupewa mtu yoyote  mwenye ulemavu anaeuhitaji kwa ajili ya kuanzisha bila ya kuwepo kwenye kikundi chochote cha ujasiriamali.








Comments

Popular posts from this blog

UTELEKEZAJI WA WANAWAKE UNAVYOKATISHA NDOTO ZA WATOTO.

Mkuu wa Polisi Jamii Kaskazini Pemba akerwa na wanao wafungia ndani watoto wenye ulemavu.

Mrajisi wa Mahakama Zanzibar ahidi kula sahani moja na Mahakimu wasio wadilifu.